Hamia kwenye habari

APRILI 7, 2014
UZBEKISTAN

Kuna Tumaini kwa Mashahidi wa Yehova Nchini Uzbekistan?

Kuna Tumaini kwa Mashahidi wa Yehova Nchini Uzbekistan?

Mashahidi wa Yehova nchini Uzbekistan wanatumaini kwamba wenye mamlaka wa Uzbekistan watawaruhusu wafurahie uhuru wa ibada bila kuvurugwa. Igor Yurchenko, mwakilishi wa Mashahidi wa Yehova wa Uzbekistan aliyefanya mikutano kadhaa na maofisa wa nchi hiyo katika mwaka wa 2013, alisema hivi: “Tumejionea mabadiliko mazuri tulipofanya mazungumzo na wenye mamlaka wa Uzbekistan, na inavyoonekana kuna matumaini kwamba watashughulikia suala hilo vizuri. Tunatumaini kwamba mikutano tuliyofanya pamoja nao itazaa matunda.”

Abdubannob Akhmedov

Jambo moja linaloonyesha kwamba wenye mamlaka wa Uzbekistan huenda wakalishughulikia suala hilo vizuri ni lile lililofanyika Machi 2, 2013 wakati walipomwachilia Abdubannob Akhmedov kutoka gerezani. Abdubannob Akhmedov alikuwa atumikie kifungo cha miaka sita na nusu gerezani lakini aliachiliwa baada ya kutumikia kwa miaka minne na nusu tu. Alikuwa mmoja wa Mashahidi waliofungwa gerezani kwa sababu ya kufanya shughuli za kidini kwa amani. Mashahidi wengine wawili waliachiliwa mnamo 2012. Kufikia sasa hakuna Shahidi yeyote wa Yehova aliye gerezani nchini Uzbekistan.

Miezi kadhaa kabla ya kumwachilia Bw. Akhmedov, wenye mamlaka wa Uzbekistan walianza mikakati ya kuhakikisha kwamba wanaheshimu haki za kibinadamu. Julai 5, 2013, serikali ya Uzbekistan iliambia kitengo cha Baraza la Haki za Kibinadamu la Umoja wa Mataifa kinachokagua rekodi za kila nchi mara kwa mara, kwamba itatambua haki inayomruhusu mtu awe na uhuru wa ibada kutia ndani vikundi mbalimbali vya kidini, bila kumbagua yeyote.

Jitihada za Kusajili Makutaniko Mapya

Kwa sasa kuna kutaniko moja lililosajiliwa kisheria nchini Uzbekistan. Kutaniko hilo liko mjini Chirchik katika eneo la Tashkent. Hata hivyo Mashahidi wengi wa Yehova wanaishi katika sehemu nyingine za nchi hiyo. Kwa kuwa tangu mwaka wa 1996 Mashahidi hawajaruhusiwa kusajili makutaniko mapya, hakuna sheria inayowalinda wanapokutana kwa ajili ya ibada, jambo linaloweza kufanya waadhibiwe. Bw. Yurchenko aliendelea kusema: “Tunatumaini kwamba mazungumzo tuliyofanya na wenye mamlaka yatasaidia sana kuboresha hali ili tupate kibali cha kusajili makutaniko ya Mashahidi wa Yehova kotekote nchini Uzbekistan.”

Mashahidi wa Yehova wanatamani sana kuwa na uhuru wa ibada nchini Uzbekistan na wanatumaini kwamba wenye mamlaka nchini humo watasajili makutaniko yote mapya hivi karibuni.