Hamia kwenye habari

NOVEMBA 5, 2021
VENEZUELA

Vitabu Vitano vya Kwanza vya Biblia Vimetolewa Katika Lugha ya Ishara ya Venezuela

Vitabu Vitano vya Kwanza vya Biblia Vimetolewa Katika Lugha ya Ishara ya Venezuela

Oktoba 30, 2021, vitabu vya Biblia vya Mathayo na Yohana vilitolewa katika Lugha ya Ishara ya Venezuela. Zaidi ya ndugu na dada 2,200 walisikiliza kupitia mtandao programu hiyo iliyorekodiwa mapema. Ndugu Miguel Guillén, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Venezuela, alitoa vitabu hivyo vya Biblia. Tawi hilo limetafsiri mistari 7,000 hivi ya Biblia katika Lugha ya Ishara ya Venezuela tangu 2006, lakini hii ndiyo mara ya kwanza vitabu vizima vya Biblia vinapatikana katika lugha hiyo.

Picha inayoonyesha ndani ya ofisi ya tafsiri

Watafsiri wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya walianza kwa kutafsiri vitabu vya Injili ya Mathayo na Yohana kwa sababu masimulizi hayo yanayohusu maisha ya Yesu yanajulikana sana na pia muundo wa masimulizi unayafanya yawe rahisi kutafsiri kuliko vitabu vingine vya Biblia.

Kutaniko la kwanza la lugha ya ishara lilianzishwa mwaka wa 2003 katika jiji la Cabimas, magharibi mwa Venezuela. Leo, kuna wahubiri 1,204 katika makutaniko 53 ya lugha ya ishara nchini kote. Viziwi wengi nchini Venezuela wanatamani kujifunza Biblia lakini hawaelewi vizuri Lugha ya Ishara ya Kihispania, ambayo inatofautiana sana na lugha yao.

Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi: “Mwanamume mmoja kiziwi alipata Biblia katika lugha ya Kihispania, lakini alipoisoma hakuelewa chochote. Alimwomba Mungu msaada. . . . Alipoelezwa kwamba angeweza kujifunza Biblia kwa kutumia Lugha ya Ishara ya Venezuela, mwanamume huyo alikubali funzo la Biblia bila kusita.”

Watafsiri sita walifanya kazi kwa miezi kumi ili kutokeza tafsiri hiyo. Walishauriana na kikundi cha ndugu saba ambao ni viziwi kutoka sehemu mbalimbali za nchi hiyo ambao walikagua tafsiri hiyo. Hatua hiyo iliwasaidia watafsiri kuhakikisha kwamba watu kutoka maeneo mbalimbali wangeelewa tafsiri hiyo.

Kwa sababu ya janga la COVID-19, watafsiri walilazimika kufanya kazi wakiwa maeneo tofauti kupitia video mtandaoni. Wakati mwingine huduma za Intaneti hazikupatikana na hiyo ikafanya kazi yao kuwa ngumu zaidi. Mtafsiri mmoja alisema hivi: “Haikuwa rahisi, lakini Yehova alitusaidia kushinda magumu hayo.”

Tunasali kwamba ndugu na dada zetu wote nchini Venezuela watafaidika kikamili kutokana na “fedha iliyosafishwa” ya Neno la Yehova katika lugha yao.—Zaburi 12:6.