Hamia kwenye habari

AGOSTI 30, 2017
VENEZUELA

Mashahidi wa Yehova Nchini Venezuela Wanaendelea Kufundisha Biblia Licha ya Hali Ngumu Kiuchumi

Mashahidi wa Yehova Nchini Venezuela Wanaendelea Kufundisha Biblia Licha ya Hali Ngumu Kiuchumi

NEW YORK—Vyombo vya habari ulimwenguni pote vimekuwa vikiripoti kuhusu hali zinavyoendelea kuzorota nchini Venezuela kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi. Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Venezuela inasema kwamba ndugu na dada pia wameathiriwa na hali hizo. Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova linahangaishwa sana na habari hizo.

Majambazi wenye silaha wameingia kwenye Majumba ya Ufalme wakati wa mikutano ili kuiba vifaa vya kielektroni na vitu vingine vyenye thamani. Isitoshe, nyakati fulani mikutano inafanywa kwenye nyumba za watu binafsi kwa sababu vurugu zinazotokea mitaani zinawazuia kufika kwenye Majumba ya Ufalme. Ndugu na dada kadhaa ni miongoni mwa wale waliopoteza kazi kwa sababu viwanda vyao vilifungwa. Wengine wanaomiliki biashara wamevamiwa na majambazi na magenge ya wahalifu na kwa sababu hiyo, wamelazimika kuuza biashara zao na kukimbilia nchi nyingine. Inasikitisha kwamba kwa miaka michache iliyopita ndugu na dada 680 hivi wametekwa nyara, zaidi ya 13,146 wameibiwa, na 144 wamebakwa au wameponea chupuchupu kubakwa. Kwa kuhuzunisha, kufikia Agosti 10, 2017, ndugu na dada 47 walikuwa wameuawa. Wengine pia wamekufa kwa sababu hawakupata matibabu waliyohitaji.

Baraza Linaloongoza linafuatilia kwa ukaribu jinsi hali ilivyo, ikitumia michango iliyotolewa kuwasaidia ndugu na dada wanaohitaji mambo ya msingi. Baraza Linaloongoza pia linawasiliana na ofisi nyingine za tawi ulimwenguni pote ili kuhakikisha njia bora zaidi za kuwategemeza ndugu na dada nchini Venezuela, kwa kuwa kuandaa msaada moja kwa moja kunaweza kuwa hatari.

Halmashauri ya Ofisi ya Tawi ya Venezuela imeanzisha kamati ya kutoa msaada inayosimamia kamati nyingine 24 ili kutunza mahitaji ya ndugu zetu. Licha ya kuvumilia majaribu makali katika ‘siku hizi za mwisho,’ wahubiri zaidi ya 149,000 waliopo nchini Venezuela wanaongeza jitihada za kuwahubiria majirani wao ujumbe wa Biblia wenye kufariji. (2 Timotheo 3:1-5; 2 Timotheo 4:2) Luis R. Navas, msemaji wa ofisi ya tawi ya Venezuela, anaeleza hivi: “Hatajawahi kuwa matajiri hivyo kiroho. Watu wengi zaidi wanahudhuria mikutano yetu. Wahubiri wengi zaidi ni mapainia wa kawaida na wakati uleule wanakuwa waangalifu zaidi katika huduma. Kwa kuwa majirani wetu wanajua kwamba hatuungi mkono upande wowote na kwamba hatushiriki matendo ya uhalifu yanayoendelea nchini, wanafurahi kupokea ujumbe wa Biblia wenye tumaini na faraja tunaowahubiria.”

Mashahidi wa Yehova nchini Venezuela wataendelea kuhangaikiana na kuwafariji majirani wao. Ulimwenguni pote, ndugu na dada zao wataendelea kuwategemeza na kusali kwa niaba yao.—Waroma 12:12, 13; 2 Wakorintho 1:3, 4.

Wanahabari Wanaweza Kuwasiliana na:

David A. Semonian, Ofisi ya Habari za Umma, simu +1-845-524-3000

Venezuela: Luis R. Navas, simu +58-244-400-5000