Hamia kwenye habari

JUNI 6, 2019
VENEZUELA

Habari za Karibuni Kutoka Venezuela: Utendaji wa Kiroho Waongezeka Licha ya Changamoto

Habari za Karibuni Kutoka Venezuela: Utendaji wa Kiroho Waongezeka Licha ya Changamoto

Matatizo ya kijamii na kiuchumi yaendelea nchini Venezuela. Ni vigumu sana kupata chakula, maji, mafuta, na dawa kwa sababu ya upungufu uliopo na ongezeko kubwa la bei. Umeme unakatwa kwa ukawaida na kufanya tatizo la upungufu wa chakula liwe baya zaidi, kwa kuwa wanashindwa kuhifadhi chakula katika jokofu. Wizi ni tatizo kubwa linaloendelea.

Licha ya hali hizo ngumu, wahubiri zaidi ya 136,500 nchini Venezuela wanaendelea kuhubiri kwa bidii. Kwa mfano, ingawa idadi ya wahubiri ilipungua kwa watu 7,000 nchini humo ikilinganishwa na mwaka uliopita, mwezi wa Januari 2019 saa 90,000 zaidi zilitumiwa katika utumishi wa shambani. Mwezi wa Aprili 2019, mafunzo zaidi ya 195,600 yaliongozwa. Idadi ya mapainia wa kawaida iliongezeka na kuwa zaidi ya 30,000. Wakati wa kampeni ya pekee ya duniani pote inayofanywa katika majira ya Ukumbusho wa kifo cha Kristo, idadi ya mapainia wasaidizi iliongezeka hadi 20,400. Bidii yao ilikuwa na matokeo mazuri, watu 471,000 walihudhuria Ukumbusho—idadi hiyo ni mara tatu ya idadi ya wahubiri. Kwa kuongezea, watu wengi huhudhuria mikutano, kwa kuwa ndugu zetu wanaendelea kutangaza ujumbe wa Biblia kwa watu wanaotafuta suluhisho linalotegemeka kwa matatizo yao yote.

Ofisi ya tawi ya Venezuela inaendelea kusimamia kazi ya kutoa msaada ili ndugu zetu wapate chakula wanachohitaji. Kila mwezi, kwa msaada wa ofisi za tawi jirani na michango inayotolewa kwa ukarimu kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, ofisi ya tawi ya Venezuela inasambaza chakula kingi kwa wahubiri 75,000 katika makutaniko 1,595.

Ndugu zetu nchini Venezuela wanakabiliana na changamoto nyingi, lakini tunatiwa moyo kuona wakiendelea ‘kushangilia katika Yehova; na kuwa na shangwe katika Mungu wa wokovu wao.’—Habakuki 3:17, 18.