Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Kumfundisha Mtoto Wako Kuwa Mstahimilivu

Kumfundisha Mtoto Wako Kuwa Mstahimilivu

 Je, umewahi kumsikia mtoto wako akisema, “Nimeshindwa! Ni kazi ngumu sana! Siwezi kuelewa!”? Unatambua kwamba anaelekea kuacha kushughulikia jambo fulani gumu. Wewe hupendi kumwona akitaabika, lakini ungependa ajifunze kukabiliana na changamoto. Je, hilo linamaanisha unapaswa kuharakisha kumsaidia tatizo hili? Je, umwache tu akate tamaa? Au je, unaweza kumfundisha kuwa na ustahimilivu?

Unachopaswa kujua

 Ustahimilivu ni muhimu. Wazazi wanapomfundisha mtoto wao kunoa uwezo wake kwa kufanya kazi ngumu, inaelekea atafanya vizuri shuleni, atakuwa na afya nzuri ya kihisia na ya kimwili, na atakuwa na mahusiano mazuri pamoja na wengine. Kwa upande ule mwingine, wazazi wanapomwendekeza mtoto wao asipatwe na magumu au changamoto, yaelekea atashuka moyo, atajihisi hafai, na ataishi maisha yasiyoridhisha akiwa mtu mzima.

 Ustahimilivu unaweza kuimarishwa. Hata watoto wadogo wanaweza kuimarisha azimio lao la kupambana na changamoto na kutatua matatizo yao. Katika uchunguzi mmoja, watafiti waligundua kwamba watoto wenye umri wa miezi 15 walijitahidi zaidi kufanya jambo gumu walipomwona mtu mzima aking’ang’ana kufanya kazi ngumu kuliko walipomwona akifaulu bila jitihada yoyote.

 “Nakumbuka nikiwafundisha binti zangu jinsi ya kufunga kamba za viatu vyao. Si ujuzi wa kujifunza siku moja. Kila mara walipofunga viatu vyao waliketi kwa dakika 10 hadi 15 wakijaribu kukumbuka jinsi ya kufanya hivyo. Kisha ningewasaidia. Iliwachukua miezi michache na nyakati nyingine hata walilia lakini hatimaye walifaulu. Ningefanya kazi yangu iwe rahisi kwa kuwanunulia viatu visivyokuwa na kamba. Lakini, nyakati nyingine, hata sisi tukiwa wazazi, tunahitaji ustahimilivu ili kuwafundisha watoto wetu kuwa wastahimilivu.”​—Colleen.

 Ustahimilivu unaweza kudhoofishwa. Huenda wazazi fulani bila kukusudia wakadhoofisha uwezo wa watoto wao wa kustahimili. Jinsi gani? Baadhi ya wazazi huogopa watoto wao watajihisi hawafai, kwa hiyo, wao hufanya haraka “kuwaokoa” ili watoto wao wasifadhaike au kuhisi wameshindwa kufanya jambo fulani. Lakini kufanya hivyo kunaweza kuwa na madhara. Mwandishi Jessica Lahey anasema hivi: “Kila wakati tunapowaokoa . . . watoto wetu kutokana na changamoto fulani, tunawaonyesha wazi kwamba tunaona kuwa hawafai, hawana uwezo, na hatuwaamini.” a Matokeo ni nini? Huenda watoto wakakata tamaa haraka zaidi wanapokabili changamoto, wakiamini kwamba wanahitaji mtu mzima ili awaokoe.

Badala ya “kumwokoa” mtoto wako asifanye kazi ngumu, unaweza kutumia fursa hiyo kumfundisha ustahimilivu

Unachoweza kufanya

 Watie moyo kufanya kazi ngumu. Wazazi wanaweza kuwafundisha watoto wao ustahimilivu kwa kuwapa kazi wanazoweza kufanya kulingana na umri wao. Kwa mfano, watoto ambao bado hawajaanza kwenda shuleni wanaweza kuchambua nguo zinazohitaji kufuliwa na kuweka vizuri vitu vyao vya kuchezea. Watoto wakubwa kidogo wanaweza kusaidia kupanga vitu vilivyonunuliwa, kupanga sahani mezani na kuondoa zilizotumika, kupeleka takataka nje, na kusafisha uchafu kidogo uliomwagika chini. Matineja wanaweza kufanya kazi ngumu zaidi zinazohusisha kufanya usafi, udumishaji, na kazi ya kurekebisha vitu vilivyoharibika. Huenda watoto wasipende kufanya kazi sikuzote, lakini watanufaika wazazi wao wakiwapa majukumu nyumbani tangu wanapokuwa na umri mdogo. Watoto watanufaika jinsi gani? Watakapokuwa watu wazima watakuwa wamejifunza kupambana kukamilisha kazi za lazima licha ya kwamba ni ngumu.

 Kanuni ya Biblia: “Kila aina ya kazi ngumu ina faida.”​—Methali 14:23.

 “Usiwape kazi ili tu wawe na kitu cha kufanya. Hakuna mtu ambaye hupenda hivyo, hata watoto. Wape kazi muhimu wakusaidie. Ikiwa mtoto wako ni mdogo, mpe kazi ya kupangusa vitu anavyoweza kufikia. Ikiwa unaosha gari, mwombe ashughulikie sehemu za chini ambazo ni vigumu kwako kufikia. Kisha mpongeze kwa kazi yake ngumu.”​—Chris.

 Mwongoze mtoto wako anapofanya kazi ngumu. Nyakati nyingine watoto hukata tamaa kwa urahisi kwa sababu hawajui jinsi ya kukamilisha kazi fulani. Kwa hiyo, unapomfundisha mtoto wako aina mpya ya kazi, unaweza kufuata njia ifuatayo. Kwanza, fanya kazi hiyo ili mtoto wako akutazame unapoifanya. Kisha, fanyeni kazi hiyo pamoja. Halafu, mtazame mtoto wako anapofanya kazi hiyo na umpe mapendekezo yatakayomnufaisha. Mwishowe, acha mtoto wako aifanye na kuikamilisha kazi hiyo yeye mwenyewe.

 Kanuni ya Biblia: “Nimewawekea kielelezo, ili mfanye kama nilivyowafanyia.”​—Yohana 13:15.

 “Nimejionea mwenyewe kwamba sisi wazazi tunapaswa kuweka mfano mzuri ikiwa tutataka watoto wetu wasitawishe ustahimilivu. Ni lazima tuonyeshe sifa tunayotaka wasitawishe.”​—Doug.

 Msaidie mtoto wako kukubali kwamba kila mtu hukosea. Mweleze mambo magumu uliyopambana sana kufanya lakini ukanufaika kwa sababu hukukata tamaa. Mweleze mtoto wako kwamba ni jambo la kawaida kuona jambo fulani kuwa gumu unapolifanya kwa mara ya kwanza na kwamba kukosea kutamsaidia kujifunza. Mhakikishie mtoto wako kwamba bado unampenda hata ikiwa atashindwa kufanya jambo fulani. Kama tu misuli inavyojengwa kwa kufanyishwa kazi, ndivyo uwezo wa kustahimili wa mtoto wako unavyositawi unapomruhusu akabiliane na changamoto. Kwa hiyo, mtoto wako anapokabili changamoto, badala ya kuingilia kati mara moja, mwache aendelee kung’ang’ana. Kitabu How Children Succeed kinasema, “njia bora zaidi ya kijana kukomaa ni kwa kujaribu kufanya jambo ambalo kuna uwezekano mkubwa wa kushindwa kulifanya.”

 Kanuni ya Biblia: “Ni vema mtu kujifunza uvumilivu tangu wakati wa ujana wake.”​—Maombolezo 3:27, Biblia Habari Njema.

 “Watoto hunufaika unawaporuhusu wapambane kufanya jambo gumu kwa kadiri fulani, huku wakijua kwamba Mama na Baba watawasaidia. Baada ya muda, watazoea kulifanya na watakuwa wamepata ustadi na pia watatambua kwamba kustahimili kuna faida.”​—Jordan.

 Sifu jitihada, si werevu. Kwa mfano, badala ya kusema, “Umefanya vizuri sana kwenye mtihani huo! Wewe ni mwerevu sana,” unaweza kusema, “Umefanya vizuri sana kwenye mtihani huo! Nimefurahishwa sana na jinsi ulivyojitahidi kusoma.” Kwa nini ni muhimu kusifu bidii kuliko werevu? Dakt. Carol Dweck anasema: “Kusifu werevu wa watoto kunawafanya wasijiamini wanapokabili jambo gumu au mambo yanapoenda mrama.” Anaendelea kusema hivi: “Ikiwa wazazi wanataka kuwapa watoto wao zawadi bora, jambo zuri wanaloweza kufanya ni kuwafundisha kupenda kukabiliana na changamoto, kujifunza kutokana na makosa yao, kufurahia kutia jitihada, kutafuta mbinu mpya za kufanya mambo, na kuendelea kujifunza. Kwa njia hiyo, watoto wao hawatakuza mwelekeo wa kutaka tu kusifiwa.” b

 Kanuni ya Biblia: “Mtu hupimwa kwa sifa anayopokea.”​—Methali 27:21.

a Kutoka kwenye kitabu The Gift of Failure.

b Kutoka kwenye kitabu Mindset.