Hamia kwenye habari

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Matumizi Mabaya ya Kileo Katika Ndoa

Matumizi Mabaya ya Kileo Katika Ndoa

 Je, mwenzi wako wa ndoa amelalamika kuhusu mazoea yako ya kunywa kileo? Ikiwa ndivyo, kuna mambo fulani unayopaswa kuzingatia.

Katika makala hii

 Matumizi mabaya ya kileo huharibu ndoa

 Matumizi mabaya ya kileo yanaweza kutokeza matatizo mengi ya afya kutia ndani, ugonjwa wa moyo, kunyauka kwa ini, na kansa. Lakini matumizi mabaya ya kileo hayaathiri afya tu. Yanaathiri ndoa kwa kutokeza jeuri nyumba, matatizo ya kiuchumi, ukosefu wa uaminifu, na talaka.

 Biblia inasema kwamba kileo “huuma kama nyoka, nayo hutoa sumu kama nyoka kipiri” inapotumiwa vibaya. (Methali 23:32) Utajuaje ikiwa wewe ni mraibu wa kileo?

 Je, umekuwa mraibu wa kileo?

 Maswali yafuatayo yanaweza kukusaidia utambue dalili za uraibu:

  •   Je, una tatizo la kudhibiti kiasi unachokunywa?

  •   Je, mara nyingi unafikiria kuhusu wakati utakapokunywa tena?

  •   Je, unaendelea kunywa licha ya matatizo yanayosababishwa na kileo maishani mwako—kutia ndani katika ndoa yako?

  •   Je, unajisikia mgonjwa unapojaribu kuacha kunywa?

  •   Je, wewe na mwenzi wako hubishana kuhusu kiasi cha kileo ambacho unakunywa?

  •   Je, sasa unaweza kunywa kiasi kikubwa zaidi cha kileo kuliko ulivyofanya zamani?

  •   Je, wewe hunywa kisiri au kuficha kileo nyumbani au kazini?

 Ikiwa jibu lako ni ndiyo kwa swali moja au zaidi huenda umekuwa mraibu wa kileo.

 Kubali kwamba una tatizo

 Je, mwenzi wako wa ndoa amelalamika kuhusu kiasi unachokunywa? Ikiwa ndivyo, huenda umejaribu kumwambia kwamba si tatizo kubwa au kujitetea kwa njia nyingine. Huenda umewalaumu wengine, kutia ndani mwenzi wako wa ndoa, kwa kusema mambo kama vile:

  •   “Ikiwa ungekuwa unanitendea vizuri, nisingehitaji kunywa.”

  •   “Ikiwa ungekuwa na mwajiri kama wangu, hata wewe ungekunywa kama mimi.”

  •   “Najua watu wengi wanaokunywa kuliko mimi.”

 Ikiwa unasema maneno kama hayo, je, inawezekana kwamba unatanguliza kileo na si kuwa na ndoa yenye furaha? Ni nini kinachopaswa kuwa muhimu zaidi?

 Kanuni ya Biblia: “Mwanamume aliyeoa huhangaikia . . . jinsi anavyoweza kupata kibali cha mke wake.”​—1 Wakorintho 7:33.

Badala ya ukuta unaokufanya ukatae kutambua kwamba una tatizo, weka dirisha linalokuwezesha kuona mahangaiko ya mwenzi wako vizuri zaidi

 Unachoweza kufanya

  •   Chukua kwa uzito mahangaiko ya mwenzi wako. Hata kama inaonekana kwamba mwenzi wako anahangaika kupita kiasi, kwa nini usifanye mabadiliko fulani? Ikiwa huwezi kufanya hivyo, yaani, ukiendelea kunywa licha ya kwamba unaona mwenzi wako anahangaishwa na jambo hilo, huenda hiyo ikiwa dalili una tatizo la kunywa kileo.

     Kanuni ya Biblia: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.”​—1 Wakorintho 10:24.

  •   Jielimishe. Ili kushinda vita, mwanajeshi anahitaji kujua mbinu za adui yake. Wewe unakabili adui kama huyo. Ili ushinde tatizo lako unahitaji kujifunza mambo yote kuhusu uraibu na jinsi unavyowanasa watu. Pia, utahitaji kujifunza mbinu za kukusaidia kushinda uraibu wa kileo na za kukusaidia usirudie zoea hilo tena.

     Kanuni ya Biblia: “Mwendelee kujiepusha na tamaa za mwili, ambazo hupigana vita nanyi.”​—1 Petro 2:11.

  •   Tafuta msaada. Kuna huduma mbalimbali za afya zinazotolewa kwa ajili ya watu walio na matatizo ya kutumia kileo vibaya. Pia unaweza kuzungumza na rafiki mkomavu ambaye anaweza kukusaidia kutambua sababu zilizojificha zinazokufanya uwe mraibu wa kileo. Kisha wasiliana na mtu huyo unapopatwa na hisia za kutamani kurudia zoea hilo.

    Tafuta msaada wa wataalamu wa afya

     Kanuni ya Biblia: “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”​—Methali 17:17.

 Matumizi mabaya ya kileo ni tatizo tata ambalo haliwezi kutatuliwa kwa kusoma makala fupi, au kwa kusema tu, “Nitajaribu kupunguza kiasi ninachokunywa.” Hata hivyo, unapaswa kutambua kwamba jinsi unavyolishughulikia hakutaathiri tu afya yako—kutaathiri pia ndoa yako.

 Ili upate habari zaidi: Soma makala zifuatazo ili ujifunze jinsi wengine walivyoshinda tatizo la kutumia kileo vibaya.

 “Mimi Si Mkatili Tena”

 “Sasa Sioni Aibu Tena”

 “Niliishi Mitaani”

 Pia, tazama video yenye kichwa ‘Nilichoshwa na Maisha Yangu’