Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Vipi Ikiwa Sipendi Shule?

Vipi Ikiwa Sipendi Shule?

 Walimu ni wakali. Kushinikizwa na marafiki. Mitihani yenye kuchosha akili, na rundo la masomo ya shule ya kufanyiwa nyumbani. Huenda una sababu nzuri unaposema hupendi shule. a Tineja anayeitwa Rachel b anasema hivi:

 “Laiti ningeweza kuwa mahali pengine popote isipokuwa shuleni. Laiti ningeweza kuwa ufuoni mwa bahari au pamoja na rafiki zangu au hata ningekuwa nikiwasaidia wazazi wangu kupika au kufanya usafi!”

 Ikiwa unahisi kama Rachel, basi unahisi kana kwamba uko jela na unalazimika kungoja mpaka kifungo chako kiishe wakati unapohitimu shule. Je, unaweza kuuona wakati unaotumia shuleni kwa njia bora zaidi?

 Je, wajua? Unapositawisha maoni yanayofaa kuhusu shule, unaweza kudhibiti hisia zako na kuacha kuiona kama mahali pa kuvumiliwa tu. Shule inaweza kukupatia fursa ya kukuza stadi utakazohitaji ukiwa mtu mzima.

 Ili kuwa na mtazamo mzuri kuhusu shule, jaribu kukazia fikira mambo yafuatayo:

 Elimu yako. Kadiri unavyojifunza, ndivyo kadiri utakavyoweza kutatua matatizo yako ya wakati ujao kazini na katika sehemu nyingine za maisha yako badala ya kuwategemea wengine sikuzote. Jiulize, ‘Hata kama kuna mambo ambayo sipendi shuleni, ni manufaa gani ninayopata kutokana na elimu yangu?’

 Kanuni ya Biblia: “Ilinde hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri.”​—Methali 3:21.

 Ili kupata habari zaidi, ona makala yenye kichwa “Nifanye Nini Ikiwa Ninaanguka Mitihani?

 Tabia zako. Tabia nzuri unazojifunza shuleni zinaweza kukufundisha kusimamia vizuri wakati wako, kuwa mwenye kuwajibika, na kuwa mfanyakazi mwenye bidii—hizo ni sifa utakazohitaji utakapokuwa mtu mzima. Jiulize: ‘Ni katika njia gani kwamba tabia nzuri ninazojifunza shuleni zinanisaidia kuwa mtu mwenye kuwajibika na mfanyakazi mzuri? Ninaweza kuboreshaje tabia hizo?’

 Kanuni ya Biblia: “Kila aina ya kazi ngumu ina faida.”​—Methali 14:23.

 Ili kupata habari zaidi, ona makala yenye kichwa “Ninaweza Kutumiaje Vizuri Muda Wangu?

 Uhusiano wako na wengine. Kuchangamana na wanafunzi wenzako kunaweza kukusaidia uwe mwenye huruma na uwaheshimu wengine. Kijana anayeitwa Joshua anasema, “kujifunza kuwasiliana na watu ni muhimu kama vile tu kujifunza historia na sayansi. Ni ustadi utakaoutumia katika maisha yako yote.” Jiulize, ‘Nimejifunza masomo gani shuleni kuhusu kuishi vizuri na wengine—hata wale ambao malezi yao au dini yao ni tofauti na yangu?’

 Kanuni ya Biblia: “Fuatilieni amani pamoja na watu wote.”​—Waebrania 12:14.

 Ili kupata habari zaidi, ona makala yenye kichwa “Ninaweza Kuboreshaje Ustadi Wangu wa Kuzungumza?

 Wakati wako ujao. Shule inaweza kukusaidia utambue mambo unayoweza kufanya vizuri na uweke malengo kulingana nayo. Msichana anayeitwa Brooke anasema hivi: “Hata huenda ukapata ustadi fulani hususa, kama nilivyopata mimi. Ujuzi huo utakusaidia kupata kazi unapohitimu.” Jiulize: ‘Nitajitegemezaje baada ya kuhitimu? Ninaweza kuhakikishaje kwamba ninajifunza yale yatakayonisaidia kupata kazi hiyo?’

 Kanuni ya Biblia: “Fikiria njia utakayochukua.”​—Methali 4:26, Biblia Habari Njema.

a Kanuni nyingi zinazozungumziwa kwenye makala hii pia zitawasaidia vijana wanaosomea nyumbani.

b Baadhi ya majina yamebadilishwa.