Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniachi Nifurahie Maisha?

Kwa Nini Wazazi Wangu Hawaniachi Nifurahie Maisha?

 Rafiki zako wamekualika kwenye sherehe mwisho juma huu. Unawaomba wazazi wako ruhusa ya kwenda, lakini wanajibu kwa uthabiti, “Hapana.” Jibu lao halikushangazi, kwa sababu walikupa jibu hilohilo wakati uliopita.

Katika makala hii

 Kwa nini sikuzote wazazi wangu husema hapana?

 Ikiwa unaona ni kana kwamba sikuzote wazazi wako wanakataa maombi yako, huenda ukahisi hawataki ufurahie maisha.

 Msichana mmoja anayeitwa Marie alihisi hivyo mara ya kwanza alipopata simu ya mkononi. Anasema hivi: “Baba aliniwekea sheria nyingi kuhusu ni programu zipi ningepakua, ningewasiliana na akina nani, na ningezungumza nao hadi muda gani. Hata hivyo, rafiki zangu waliruhusiwa kufanya chochote walichotaka!”

 Jambo la kufikiria: Je, baba ya Marie alikuwa akijaribu kumzuia asifurahie maisha kabisa? Huenda ni nini kilichomhangaisha baba yake?

Sheria ya kudhibiti mwendo barabarani inakunyima uhuru kwa kadiri fulani, lakini pia inakulinda usipatwe na madhara; ni hivyo pia kuhusu sheria ambazo wazazi wanaweka

 Jaribu kufanya hivi: Wazia kwamba wewe ni mzazi, na una kijana ambaye amepata simu ya mkononi. Wewe ungekuwa na wasiwasi upi? Wewe ungemwekea sheria zipi ili kumlinda kijana wako? Wewe ungesema nini ikiwa kijana wako angelalamika kwamba hutaki afurahie maisha?

 “Sikuzote baba alisema, ‘Jiwazie jinsi ambavyo ungehisi ikiwa wewe ungekuwa mzazi.’ Kufanya hivyo kulinisaidia kuona faida ya sheria alizoweka na pia sababu ya kuziweka. Ikiwa ningekuwa na watoto, ningetarajia wafuate sheria zilezile ambazo baba yangu aliniwekea.”​—Tanya.

 Nifanye nini ili wazazi wangu waseme ndiyo?

 Usifanye hivi: Usinune, usilalamike, wala usibishane.

 “Huwezi kutimiza chochote ukilalamika, na kufanya hivyo kunaweza kukuchosha wewe na wazazi wako kihisia. Ukibishana, wazazi wako watahisi kwamba bado hujakomaa na hustahili kupata uhuru zaidi.”​—Richard.

 Jaribu kufanya hivi: Jipatie muda wa kutafakari. Chunguza hali hiyo kwa maoni ya wazazi wako. Jiulize, je, tatizo ni kwamba hawakuamini, au je, ni kwamba hawapendi mazingira unayojiingiza au watu utakaokuwa nao? Kwa nini usizungumze nao kuhusu jambo hilo kwa utulivu, ili uelewe maoni yao?

 “Sikuzote wazazi wangu wana nia nzuri ya kuweka sheria. Si eti wanajaribu kunizuia kufurahia maisha; wangependa tu nifurahie kwa njia nzuri ambayo haitaniletea matatizo.”​—Ivy.

 Kanuni ya Biblia: “Mtu mpumbavu humwaga hisia zake zote, lakini mwenye hekima huzizuia kwa utulivu.”​—Methali 29:11.

 Usifanye hivi: Usifanye kwa siri jambo ambalo wazazi walikukataza.

 “Nilijaribu kukwepa kutii sheria ambazo baba aliweka kuhusiana na matumizi ya simu. Nilijaribu kutafuta njia za kuwatumia rafiki zangu ujumbe usiku sana au kupakua programu ambazo baba hakuniruhusu niwe nazo. Lakini baadaye aligundua tu, naye akaniwekea sheria kali zaidi kwa sababu sasa hakuniamini. Si hekima kukwepa kufuata sheria.”​—Marie.

 Jaribu kufanya hivi: Waonyeshe wazazi wako kwamba unaunga mkono sheria walizoweka na hivyo wakuamini zaidi.

 “Uwe na subira. Huenda ikachukua muda mrefu kwa wazazi wako kubadili sheria fulani, lakini wakiona unatii sheria walizoweka tayari, huenda wakakupa uhuru zaidi.”​—Melinda.

 Kanuni ya Biblia: “Watiini wazazi wenu katika kila jambo.”​—Wakolosai 3:20.

 Usifanye hivi: Usijaribu kuwashinikiza wazazi wako, labda kwa kuwaambia mambo ambayo watoto wengine wa umri wako wanaruhusiwa kufanya.

 “Kung’ang’ania jambo lako hakutafanya maisha yako yawe rahisi wala hakutakusaidia kupata unachotaka.”​—Natalie.

 Jaribu kufanya hivi: Tumia daftari lenye kichwa “Kutafakari Kuhusu Sheria za Nyumbani” ili kukusaidia kuzungumzia jambo hilo pamoja na wazazi wako.

 “Wazazi wangependa kuona kwamba una uwezo wa kufanya maamuzi mazuri. Kwa hiyo ninapozungumza nao, mimi hujaribu kutumia hoja kuunga mkono mawazo ninayotoa badala ya kutumia hisia. Ninapofanya hivyo, mara nyingi mimi hufanikiwa kuwasadikisha.”​—Joseph.

 Kanuni ya Biblia: “Mheshimu baba yako na mama yako.”​—Waefeso 6:2.