Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Nifanye Nini Ikiwa Wazazi Wangu Wanatalikiana?

Nifanye Nini Ikiwa Wazazi Wangu Wanatalikiana?

 Mojawapo ya hali zenye mkazo zaidi ambazo vijana wanaweza kukabiliana nazo ni kutalikiana kwa wazazi wao. Unaweza kufanya nini ili kukabiliana na huzuni?

Katika makala hii

 Mambo matatu unayopaswa kuepuka

 1. Kujilaumu

 “Pindi moja mama yangu aliniambia kwamba matatizo yote kati yake na baba yalianza nilipozaliwa, kwa hiyo, nilijiambia mimi ndiye niliyesababisha ndoa ya wazazi wangu ivunjike.”​—Diana.

 Kumbuka jambo hili: Wazazi wako hawatalikiani kwa sababu yako. Wanatalikiana kwa sababu ya matatizo yao wenyewe. Si wewe uliyeyasababisha na huwezi kuyatatua. Wao wenyewe ndio wanaopaswa kushughulikia matatizo ya ndoa yao.

 “Kila mtu ataubeba mzigo wake mwenyewe.”​—Wagalatia 6:5.

 2. Kufunga kinyongo

 “Nilimkasirikia sana baba kwa kukosa kuwa mwaminifu kwa mama yangu. Itakuwa vigumu sana kwangu kumwamini tena.”​—Rianna.

 Kumbuka jambo hili: Huenda umekasirishwa na mambo yanayowapata wazazi wako, na una sababu nzuri ya kukasirika. Lakini kufunga kinyongo kunaweza kudhuru afya yako. Kunaweza kukuumiza wewe kimwili na kihisia. Na ndiyo sababu kufunga kinyongo ni sawa na kumeza sumu halafu kumsubiri mtu mwingine awe mgonjwa. a

 “Acha hasira na uache ghadhabu.”​—Zaburi 37:8.

 3. Kuwa na shaka ikiwa wewe utakuwa na ndoa yenye furaha

 “Ninaogopa sana kwamba nitatenda kama baba yangu alivyotenda. Ninaogopa kwamba nikiolewa na kupata watoto, nitajikuta katika hali ileile iliyowaongoza wazazi wangu kutalikiana.”​—Jessica.

 Kumbuka jambo hili: Kwa sababu tu ndoa ya wazazi wako ilivunjika, hakumaanishi kwamba ndoa yako haitafanikiwa. Ukweli ni kwamba unaweza kujifunza masomo muhimu kutokana na hali ambayo wazazi wako walikabili. Kwa mfano, unaweza kuwa makini zaidi unapochunguza sifa za mtu unayetaka kufunga ndoa naye. Pia, ndoa iliyovunjika ya wazazi wako inaweza kukuchochea kusitawisha sifa ambazo zitakufanya uwe mume au mke bora zaidi.

 “Kila mmoja na achunguze matendo yake mwenyewe.”​—Wagalatia 6:4.

Kukubaliana na talaka ya wazazi wako ni kama kupona mfupa uliovunjika. Hisia za maumivu zitapona kadiri muda unavyopita

 Mambo matatu unayoweza kufanya

 1. Wasiliana. Ni rahisi kwa watu wanaofungia hisia mbaya kuanza kujihusisha katika mazoea yenye kudhuru, kama vile kutumia kileo vibaya au dawa za kulevya. Badala ya kufanya hivyo, jaribu kufanya mambo yafuatayo:

 Zungumza na wazazi wako. Ikiwa mmoja wa wazazi wako au wote wawili wanajaribu kukuhusisha katika matatizo yao, mweleze kwa upole lakini kwa uthabiti jinsi jambo hilo linavyokuathiri. Ikiwa ni vigumu kwako kuzungumza naye uso kwa uso, unaweza kumwandikia barua mmoja wao au wote wawili.

 Zungumza na rafiki anayetumainika. Unaweza kupata kitulizo kikubwa ikiwa una mtu wa kukusikiliza. Biblia inasema kwamba “rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”​—Methali 17:17.

 Zungumza na Muumba wako. Sikuzote Yehova Mungu, ambaye ndiye “Msikiaji wa sala,” yuko tayari kukusikiliza. (Zaburi 65:2) Biblia inasema kwamba unaweza ‘kutupa mahangaiko yako yote juu yake, kwa sababu yeye anakujali.’​—1 Petro 5:7.

  •   Unaweza kuzungumza na mzazi yupi kwa utulivu?

  •   Ni rafiki yupi (aliye na umri wako au umri mkubwa) unayeweza kumtumaini ili akusaidie kuvumilia hali hii?

  •   Unaweza kusali kuhusu mambo gani hususa?

 2. Badilikana kulingana na hali

 Talaka ya wazazi wako inaweza kukulazimu uishi katika makao mapya, shule mpya, uzoee kupata matunzo ya kiwango kidogo zaidi cha pesa, au hata marafiki wapya. Ni wazi kwamba hilo linaweza kukukasirisha na kukuletea mkazo, na huenda ukahisi kwamba maisha yako yamebadilika kabisa kwa njia mbaya. Ni nini kinachoweza kufanya badiliko hilo liwe rahisi zaidi? Jaribu kukazia fikira jinsi ya kubadilika kulingana na hali mpya.

  •   Talaka ya wazazi wako imekuletea badiliko gani kubwa zaidi?

  •   Umechukua hatua zipi ili kubadilika kulingana na hali?

 “Hata hali zangu ziweje nimejifunza kuridhika.”​—Wafilipi 4:11.

 3. Tambua uwezo wako

 Ingawa talaka ya wazazi wako inaweza kukusababishia mahangaiko mengi, inaweza pia kukufundisha kutambua uwezo wako. Inaweza pia kukusaidia kusitawisha sifa mpya. Jeremy ambaye alikuwa na umri wa miaka 13 wazazi wake walipotalikiana anasema hivi: “Talaka ya wazazi wangu ilinifanya nianze kuwajibika zaidi. Mimi ndiye niliyekuwa mkubwa miongoni mwa watoto, kwa hiyo nilihitaji kumsaidia mama yangu zaidi na pia kumsaidia ndugu yangu mdogo.”

Talaka ya wazazi wako inaweza kukuchochea kuwajibika zaidi nyumbani

  •   Hali ya wazazi wako imekusaidia kutambua una sifa zipi?

  •   Ungependa kusitawisha sifa zipi?

 “Kila Andiko limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida . . . kwa kunyoosha mambo.”​—2 Timotheo 3:16.

a Ili ujifunze mengi zaidi soma makala yenye kichwa “Ninawezaje Kudhibiti Hasira Yangu?”