Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 12:1-40

  • Waliounga mkono utawala wa Daudi (1-40)

12  Hao ndio wanaume walioenda kumwona Daudi kule Siklagi+ wakati ambapo hakuwa na uhuru wa kutembea popote kwa sababu ya Sauli+ mwana wa Kishi, nao walikuwa miongoni mwa mashujaa hodari waliomuunga mkono vitani.+  Walijihami kwa upinde, nao waliweza kutumia mkono wa kulia na mkono wa kushoto+ kurusha mawe kwa kombeo+ au kupiga mishale kwa upinde. Walikuwa wazao wa ndugu za Sauli, kutoka Benjamini.+  Kiongozi wao alikuwa Ahiezeri, pamoja na Yoashi, wote wawili walikuwa wana wa Shemaa Mgibea;+ Yezieli na Peleti wana wa Azmavethi,+ Baraka, Yehu Mwanathothi,  Ishmaya Mgibeoni,+ shujaa hodari miongoni mwa wale 30+ na kiongozi wa wale 30; pia Yeremia, Yahazieli, Yohanani, Yozabadi Mgedera,  Eluzai, Yerimothi, Bealia, Shemaria, Shefatia Mharifu,  Elkana, Ishia, Azareli, Yoezeri, na Yashobeamu, Wakora;+  na Yoela na Zebadia wana wa Yerohamu wa Gedori.  Baadhi ya Wagadi walienda kujiunga na Daudi katika ngome kule nyikani;+ walikuwa mashujaa hodari, wanajeshi waliozoezwa kwa ajili ya vita, waliosimama tayari wakiwa na ngao kubwa na mkuki, nao walikuwa na nyuso kama za simba na walikimbia mbio sana* kama swala milimani.  Ezeri ndiye aliyekuwa kiongozi wao, wa pili Obadia, wa tatu Eliabu, 10  wa nne Mishmana, wa tano Yeremia, 11  wa sita Atai, wa saba Elieli, 12  wa nane Yohanani, wa tisa Elzabadi, 13  wa kumi Yeremia, wa kumi na moja Makbanai. 14  Hao walikuwa wazao wa Gadi,+ viongozi wa jeshi. Mwenye uwezo mdogo zaidi angeweza kuwashinda watu 100, na mwenye uwezo mkubwa zaidi angeweza kuwashinda watu 1,000.+ 15  Hao ndio wanaume waliovuka Yordani katika mwezi wa kwanza wakati kingo za mto huo zilipokuwa zimefurika, nao waliwafukuza watu wote waliokuwa wakiishi mabondeni, upande wa mashariki na wa magharibi. 16  Baadhi ya wanaume wa Benjamini na Yuda walikuja pia kwa Daudi katika ngome yake.+ 17  Kisha Daudi akatoka na kuwaambia: “Ikiwa mmekuja kwangu kwa amani ili kunisaidia, moyo wangu utaungana nanyi. Lakini ikiwa mmekuja kunisaliti kwa maadui wangu wakati mikono yangu haijatenda kosa lolote, Mungu wa mababu zetu na aone hilo na kuhukumu.”+ 18  Kisha roho ikamjia* Amasai,+ kiongozi wa wale 30, akasema: “Sisi ni wako, Ee Daudi, nasi tuko pamoja nawe, Ee mwana wa Yese.+ Amani, amani iwe yako, na amani iwe na yule anayekusaidia,Kwa maana Mungu wako anakusaidia.”+ Basi Daudi akawakaribisha na kuwaweka wawe miongoni mwa viongozi wa wanajeshi. 19  Baadhi ya watu wa kabila la Manase walitoroka pia na kujiunga na Daudi alipokuja pamoja na Wafilisti kupigana na Sauli; lakini hakuwasaidia Wafilisti, kwa sababu baada ya watawala wa Wafilisti+ kushauriana, walimfukuza wakisema: “Atatoroka na kwenda kwa Sauli bwana wake, na jambo hilo litahatarisha vichwa vyetu.”+ 20  Alipoenda Siklagi,+ watu hawa wa kabila la Manase walitoroka na kujiunga naye: Adna, Yozabadi, Yediaeli, Mikaeli, Yozabadi, Elihu, na Zilethai, viongozi wa maelfu katika kabila la Manase.+ 21  Walimsaidia Daudi kupigana na kundi la wavamizi, kwa sababu wote walikuwa wanaume hodari walio jasiri,+ nao wakawa wakuu katika jeshi lake. 22  Siku baada ya siku watu waliendelea kuja kumsaidia Daudi+ mpaka kambi yake ikawa kubwa kama kambi ya Mungu.+ 23  Hii ndiyo idadi ya viongozi wa wale waliojihami kwa ajili ya vita ambao walijiunga na Daudi kule Hebroni+ ili kumpa utawala wa Sauli kulingana na agizo la Yehova.+ 24  Wanaume wa Yuda waliobeba ngao kubwa na mkuki walikuwa 6,800, waliojihami kwa ajili ya vita. 25  Kutoka kwa Wasimeoni, kulikuwa na wanajeshi 7,100, wanaume jasiri na hodari. 26  Kutoka kwa Walawi, 4,600. 27  Yehoyada+ alikuwa kiongozi wa wana wa Haruni,+ naye alikuwa pamoja na watu 3,700, 28  na pia Sadoki,+ kijana aliyekuwa hodari na jasiri, pamoja na wakuu 22 kutoka katika ukoo wake.* 29  Kutoka kwa Wabenjamini, ndugu za Sauli,+ kulikuwa na wanaume 3,000, ambao wengi wao, hapo awali, walikuwa wakilinda masilahi ya nyumba ya Sauli. 30  Kutoka kwa Waefraimu, kulikuwa na wanaume hodari 20,800, waliokuwa jasiri na maarufu katika koo zao.* 31  Na kutoka kwa nusu ya kabila la Manase, kulikuwa na wanaume 18,000 waliotajwa kwa majina ili waje kumweka Daudi kuwa mfalme. 32  Kutoka kwa kabila la Isakari, kulikuwa na viongozi 200 ambao walielewa nyakati na kujua yale ambayo Waisraeli walipaswa kufanya, na ndugu zao wote walikuwa chini ya uongozi wao. 33  Kutoka kwa Zabuloni, kulikuwa na wanaume 50,000 walioweza kutumikia jeshini, waliojipanga kivita wakiwa na silaha zote za vita, wote walijiunga na Daudi kwa ushikamanifu usiogawanyika.* 34  Kutoka kwa Naftali, kulikuwa na wakuu 1,000, nao walikuwa pamoja na wanaume 37,000 wenye ngao kubwa na mkuki. 35  Kutoka kwa Wadani, wale waliojipanga kivita walikuwa 28,600. 36  Na kutoka kwa Asheri, wale walioweza kutumikia jeshini na kujipanga kivita walikuwa 40,000. 37  Kutoka ng’ambo ya Yordani,+ kutoka kwa Warubeni, Wagadi, na nusu ya kabila la Manase, kulikuwa na wanajeshi 120,000 waliokuwa na aina zote za silaha za vita. 38  Hao wote walikuwa wanaume wa vita, walioungana pamoja vitani; walikuja Hebroni kwa moyo kamili ili kumweka Daudi kuwa mfalme wa Israeli yote, na pia Waisraeli wengine wote walikuwa na nia moja ya* kumweka Daudi kuwa mfalme.+ 39  Nao walikaa huko pamoja na Daudi kwa siku tatu, wakila na kunywa, kwa kuwa ndugu zao walikuwa wamefanya matayarisho kwa ajili yao. 40  Pia majirani wao, na hata wale waliokuwa mbali kufikia Isakari, Zabuloni, na Naftali, walikuwa wakileta vyakula kwa punda, ngamia, nyumbu, na ng’ombe—walileta unga, keki za tini zilizoshinikizwa na keki za zabibu kavu, divai, mafuta, na ng’ombe na kondoo wengi sana, kwa maana watu walishangilia nchini Israeli.

Maelezo ya Chini

Au “walikuwa wepesi.”
Tnn., “ikamvaa.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Au “wote waliojiunga na Daudi hawakuwa na mioyo miwili.”
Tnn., “walikuwa na moyo mmoja katika.”