Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 14:1-17

  • Daudi aimarishwa kuwa mfalme (1, 2)

  • Familia ya Daudi (3-7)

  • Wafilisti washindwa (8-17)

14  Mfalme Hiramu+ wa Tiro aliwatuma wajumbe kwa Daudi, pamoja na mbao za mierezi, waashi,* na maseremala ili wamjengee Daudi nyumba.*+  Na Daudi alijua kwamba Yehova alikuwa amemwimarisha kabisa kuwa mfalme wa Israeli,+ kwa maana ufalme wake ulikuwa umekwezwa sana kwa ajili ya watu Wake Waisraeli.+  Daudi alichukua wake+ zaidi huko Yerusalemu, na Daudi akazaa wana na mabinti zaidi.+  Haya ndiyo majina ya watoto wake waliozaliwa Yerusalemu:+ Shamua, Shobabu, Nathani,+ Sulemani,+  Ibhari, Elishua, Elpeleti,  Noga, Nefegi, Yafia,  Elishama, Beeliada, na Elifeleti.  Wafilisti waliposikia kwamba Daudi alikuwa ametiwa mafuta kuwa mfalme wa Waisraeli wote,+ Wafilisti wote wakapanda kuja kumtafuta Daudi.+ Daudi aliposikia jambo hilo, akaenda kukabiliana nao.  Kisha Wafilisti wakaja na kuvamia tena na tena katika Bonde la* Refaimu.+ 10  Daudi akamuuliza Mungu: “Je, nipande kwenda kuwashambulia Wafilisti? Je, utawatia mikononi mwangu?” Ndipo Yehova akamwambia: “Panda uende, nami hakika nitawatia mikononi mwako.”+ 11  Basi Daudi akapanda kwenda Baal-perasimu,+ naye akawaua huko. Ndipo Daudi akasema: “Mungu wa kweli amewapasua na kuwapita maadui wangu kwa mkono wangu, kama ufa uliopasuliwa na maji.” Ndiyo sababu walipaita mahali hapo Baal-perasimu.* 12  Wafilisti wakaacha miungu yao hapo, na Daudi alipotoa amri, miungu hiyo iliteketezwa motoni.+ 13  Baadaye Wafilisti wakaja tena na kuvamia bondeni.*+ 14  Daudi akamwomba Mungu ushauri tena, lakini Mungu wa kweli akamwambia: “Usipande moja kwa moja na kuwafuatia. Badala yake, zunguka nyuma yao, uwashambulie mbele ya vichaka vya mibaka.+ 15  Na utakaposikia sauti ya watu wakipiga mwendo juu ya vichaka vya mibaka, washambulie, kwa sababu mimi Mungu wa kweli nitakuwa nimetangulia mbele yako ili kuliua jeshi la Wafilisti.”+ 16  Basi Daudi akafanya kama Mungu wa kweli alivyomwamuru,+ wakaliua jeshi la Wafilisti kuanzia Gibeoni mpaka Gezeri.+ 17  Umaarufu wa Daudi ukaenea katika nchi zote, na Yehova akayafanya mataifa yote yamwogope Daudi.+

Maelezo ya Chini

Au “wajenzi wa kuta.”
Au “jumba la mfalme.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Maana yake “Bwana Anayepasua na Kupita.”
Au “kwenye nchi tambarare ya chini.”