Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 19:1-19

  • Waamoni wawatendea vibaya wajumbe wa Daudi (1-5)

  • Daudi awashinda Waamoni na Wasiria (6-19)

19  Baadaye Nahashi mfalme wa Waamoni akafa, na mwanawe akawa mfalme baada yake.+  Ndipo Daudi akasema: “Nitamtendea kwa upendo mshikamanifu+ Hanuni mwana wa Nahashi, kwa sababu baba yake alinitendea kwa upendo mshikamanifu.” Basi Daudi akawatuma wajumbe ili wamfariji baada ya kufiwa na baba yake. Lakini watumishi wa Daudi walipofika katika nchi ya Waamoni+ kumfariji Hanuni,  wakuu wa Waamoni wakamwambia Hanuni: “Je, unafikiri kwamba Daudi anawatuma wafariji kwako ili kumheshimu baba yako? Je, watumishi wake hawajaja kwako ili kufanya uchunguzi kamili na kukupindua wewe na kuipeleleza nchi?”  Kwa hiyo Hanuni akawachukua watumishi wa Daudi, akawanyoa,+ akakata nguo zao katikati kwenye matako na kuwafukuza.  Daudi alipoambiwa kuhusu wanaume hao, mara moja akawatuma wanaume wengine waende kukutana nao, kwa sababu wanaume hao walikuwa wameaibishwa sana; mfalme akawaambia: “Kaeni Yeriko+ mpaka ndevu zenu zitakapoota, kisha mrudi.”  Baada ya muda Waamoni wakaona kuwa wananuka mbele ya Daudi, kwa hiyo Hanuni na Waamoni wakatuma talanta 1,000 za fedha* ili kukodi magari ya vita na wapanda farasi kutoka Mesopotamia,* Aram-maaka, na Soba.+  Basi wakakodi magari 32,000 ya vita, pamoja na mfalme wa Maaka na watu wake. Kisha wakaja na kupiga kambi mbele ya Medeba.+ Waamoni wakakusanyika pamoja kutoka katika majiji yao, wakaja ili kupigana vita.  Daudi aliposikia habari hizo, alimtuma Yoabu+ na jeshi lote, kutia ndani mashujaa wake hodari zaidi.+  Nao Waamoni wakatoka na kujipanga kivita kwenye lango la jiji huku wafalme waliokuja wakiwa peke yao uwanjani. 10  Yoabu alipoona kwamba anashambuliwa upande wa mbele na wa nyuma, alichagua baadhi ya wanajeshi bora Israeli na kuwapanga kivita ili wapigane na Wasiria.+ 11  Wanaume waliobaki aliwaweka chini ya usimamizi wa* Abishai ndugu yake,+ ili awapange kivita kupigana na Waamoni. 12  Kisha akasema: “Ikiwa Wasiria+ watanizidi nguvu, basi mtaniokoa; lakini Waamoni wakiwazidi ninyi nguvu, nitawaokoa. 13  Ni lazima tuwe imara na jasiri+ kwa ajili ya watu wetu na kwa ajili ya majiji ya Mungu wetu, naye Yehova atafanya yaliyo mema machoni pake.” 14  Kisha Yoabu na wanaume wake wakasonga mbele kwenda kupigana vita na Wasiria, nao wakamkimbia.+ 15  Waamoni walipoona kwamba Wasiria wamekimbia, wakamkimbia pia Abishai ndugu yake na kuingia jijini. Baada ya hayo, Yoabu akarudi Yerusalemu. 16  Wasiria walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli, waliwatuma wajumbe wawaite Wasiria waliokuwa katika eneo la Mto Efrati,+ wakiongozwa na Shofaki mkuu wa jeshi la Hadadezeri.+ 17  Daudi alipoambiwa habari hiyo, akawakusanya Waisraeli wote mara moja, wakavuka Yordani na kuwafikia, wakajipanga kivita ili kupigana nao. Daudi alijipanga kivita ili kupigana na Wasiria, nao wakapigana naye.+ 18  Lakini Wasiria waliwakimbia Waisraeli; Daudi akawaua Wasiria 7,000 walioendesha magari ya vita na wanajeshi 40,000 waliotembea kwa miguu, akamuua Shofaki mkuu wa jeshi. 19  Watumishi wa Hadadezeri walipoona kwamba wameshindwa na Waisraeli,+ mara moja wakafanya amani na Daudi, wakawa watumishi wake;+ na Wasiria hawakutaka kuwasaidia tena Waamoni.

Maelezo ya Chini

Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “Aram-naharaimu.”
Tnn., “mikononi mwa.”