Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 14:1-31

  • Unabii wa Ahiya dhidi ya Yeroboamu (1-20)

  • Rehoboamu atawala Yuda (21-31)

    • Shishaki ashambulia (25, 26)

14  Wakati huo Abiya mwana wa Yeroboamu akawa mgonjwa.  Kwa hiyo Yeroboamu akamwambia mke wake: “Tafadhali, inuka, badili sura yako ili watu wasitambue kwamba wewe ni mke wa Yeroboamu, halafu uende Shilo. Tazama! Nabii Ahiya yuko huko. Yeye ndiye aliyesema kwamba mimi nitakuwa mfalme wa watu hawa.+  Chukua mikate kumi, keki zilizonyunyiziwa kitu, na chupa ya asali, uende kwake. Kisha atakwambia kitakachompata mvulana huyu.”  Mke wa Yeroboamu akafanya mambo aliyoambiwa na Yeroboamu. Akainuka na kwenda Shilo,+ akafika katika nyumba ya Ahiya. Ahiya alikodoa macho yake mbele, lakini hakuweza kuona kwa sababu ya umri wake.  Hata hivyo, Yehova alikuwa amemwambia Ahiya: “Tazama, mke wa Yeroboamu anakuja kutafuta habari kuhusu mwanawe, kwa sababu ni mgonjwa. Nitakwambia mambo utakayomwambia.* Atakapofika ataficha sura yake ili asijulikane.”  Mara tu Ahiya aliposikia sauti ya miguu ya mwanamke huyo alipokuwa akija mlangoni, akasema: “Ingia ndani, mke wa Yeroboamu. Kwa nini unaficha sura yako usijulikane? Nimeagizwa nikupe ujumbe mkali.  Nenda, ukamwambie Yeroboamu, ‘Hivi ndivyo anavyosema Yehova Mungu wa Israeli: “Nilikuinua kutoka miongoni mwa watu wako na kukufanya kuwa kiongozi wa watu wangu Waisraeli.+  Kisha nikaurarua ufalme kutoka katika nyumba ya Daudi na kukupa wewe.+ Lakini hujawa kama mtumishi wangu Daudi, ambaye alishika amri zangu na kunifuata kwa moyo wake wote, akitenda tu yaliyokuwa sawa machoni pangu.+  Lakini umetenda mambo mabaya zaidi kuliko wote waliokutangulia, nawe ulijitengenezea mungu mwingine na sanamu za chuma* ili kunikasirisha,+ mimi ndiye uliyenigeuzia mgongo.+ 10  Kwa sababu hiyo ninailetea msiba nyumba ya Yeroboamu, nami nitamwangamiza kila mwanamume* wa Yeroboamu, kutia ndani wasio na uwezo na walio dhaifu katika Israeli, nami nitaifagia kabisa nyumba ya Yeroboamu,+ kama mtu anavyoondoa kabisa mavi mpaka yote yanapokwisha! 11  Mtu yeyote wa Yeroboamu atakayefia jijini, ataliwa na mbwa; na yeyote atakayefia shambani, ataliwa na ndege wa angani, kwa sababu Yehova amesema hayo.”’ 12  “Sasa inuka; nenda nyumbani kwako. Utakapotia mguu wako jijini, mtoto huyo atakufa. 13  Waisraeli wote watamwombolezea na kumzika, kwa maana ni yeye peke yake katika familia ya Yeroboamu atakayezikwa kaburini, kwa sababu ni yeye tu katika nyumba ya Yeroboamu ambaye Yehova Mungu wa Israeli amepata jambo fulani jema ndani yake. 14  Yehova atajiinulia mfalme wa Israeli atakayeiangamiza nyumba ya Yeroboamu+ kuanzia siku hiyo na kuendelea, naam, hata sasa. 15  Yehova atawapiga Waisraeli kama tete linaloyumba-yumba ndani ya maji, naye atawang’oa Waisraeli kutoka katika nchi hii nzuri aliyowapa mababu zao+ na kuwatawanya ng’ambo ya Mto Efrati,+ kwa sababu walimkasirisha Yehova kwa kutengeneza miti mitakatifu.*+ 16  Naye atawaacha Waisraeli kwa sababu ya dhambi ambazo Yeroboamu alitenda na kusababisha Waisraeli kuzitenda.”+ 17  Basi mke wa Yeroboamu akainuka na kwenda zake, akafika Tirsa. Alipokaribia kizingiti cha mlango, mvulana huyo akafa. 18  Kwa hiyo wakamzika, na Waisraeli wote wakamwombolezea, kama Yehova alivyokuwa amesema kupitia nabii Ahiya, mtumishi wake. 19  Na mambo mengine katika historia ya Yeroboamu, jinsi alivyopigana vita+ na jinsi alivyotawala, yameandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli. 20  Yeroboamu alitawala kwa miaka 22, kisha akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake;+ na Nadabu mwanawe akawa mfalme baada yake.+ 21  Wakati huo, Rehoboamu mwana wa Sulemani alikuwa mfalme wa Yuda. Rehoboamu alikuwa na umri wa miaka 41 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 17 huko Yerusalemu, jiji ambalo Yehova alichagua+ miongoni mwa makabila yote ya Israeli ili kuweka jina lake humo.+ Mama ya Rehoboamu aliitwa Naama, naye alikuwa Mwamoni.+ 22  Na watu wa Yuda walikuwa wakitenda maovu machoni pa Yehova,+ na kwa dhambi zao walimkasirisha kuliko walivyofanya mababu zao.+ 23  Pia waliendelea kujijengea mahali pa juu, nguzo takatifu, na miti mitakatifu*+ juu ya kila kilima kirefu+ na chini ya kila mti wenye majani mengi.+ 24  Kulikuwa pia na wanaume makahaba wa hekaluni katika nchi.+ Watu walitenda mambo yote yenye kuchukiza yaliyofanywa na mataifa ambayo Yehova alikuwa ameyafukuza kutoka mbele ya Waisraeli. 25  Katika mwaka wa tano wa Mfalme Rehoboamu, Mfalme Shishaki+ wa Misri alishambulia Yerusalemu.+ 26  Akachukua hazina za nyumba ya Yehova na hazina za nyumba ya mfalme.*+ Alichukua kila kitu, kutia ndani ngao zote za dhahabu ambazo Sulemani alikuwa ametengeneza.+ 27  Basi Mfalme Rehoboamu akatengeneza ngao za shaba zichukue mahali pa ngao hizo, akaziweka chini ya ulinzi wa mkuu wa walinzi,* aliyelinda mlango wa nyumba ya mfalme. 28  Wakati wowote ambapo mfalme alikuja katika nyumba ya Yehova, walinzi walizichukua, kisha walizirudisha katika chumba cha walinzi. 29  Na mambo mengine katika historia ya Rehoboamu, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda?+ 30  Kulikuwa na vita daima kati ya Rehoboamu na Yeroboamu.+ 31  Kisha Rehoboamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ Mama yake aliitwa Naama, naye alikuwa Mwamoni.+ Na Abiyamu* mwana wake+ akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Au “Utamwambia hivi na hivi.”
Au “sanamu za kuyeyushwa.”
Tnn., “mtu yeyote anayekojoa ukutani.” Huu ni msemo wa Kiebrania wa kuwadharau wanaume.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Au “jumba la mfalme.”
Tnn., “wakimbiaji.”
Anaitwa pia Abiya.