Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 20:1-43

  • Wasiria wapigana vita dhidi ya Ahabu (1-12)

  • Ahabu awashinda Wasiria (13-34)

  • Unabii dhidi ya Ahabu (35-43)

20  Basi Mfalme Ben-hadadi+ wa Siria+ akakusanya jeshi lake lote pamoja na wafalme wengine 32 wakiwa na farasi wao na magari yao ya vita; akapanda kwenda kuzingira+ jiji la Samaria+ na kupigana nalo.  Kisha akawatuma wajumbe kwa Mfalme Ahabu+ wa Israeli jijini, akamwambia: “Ben-hadadi anasema,  ‘Fedha yako na dhahabu yako ni yangu, na pia wake zako warembo zaidi na wana wako ni wangu.’”  Ndipo mfalme wa Israeli akasema: “Kama ulivyosema bwana wangu mfalme, mimi ni wako pamoja na vitu vyangu vyote.”+  Baadaye wajumbe hao wakarudi na kusema: “Ben-hadadi anasema, ‘Nilituma ujumbe huu kwako: “Utanipa fedha yako, dhahabu yako, wake zako, na wana wako.”  Lakini kesho wakati kama huu nitawatuma watumishi wangu kwako, nao wataichunguza kwa makini nyumba yako na nyumba za watumishi wako, watachukua vitu vyako vyote vinavyotamanika na kwenda navyo.’”  Ndipo mfalme wa Israeli akawaita wazee wote wa nchi na kuwaambia: “Angalieni, tafadhali, na mjue kwamba mtu huyu anakusudia kuleta msiba, kwa maana alitaka nimpe wake zangu, wanangu, fedha yangu, na dhahabu yangu, nami sikukataa agizo lake.”  Ndipo wazee wote na watu wote wakamwambia: “Usitii, wala kukubali.”  Kwa hiyo akawaambia wajumbe wa Ben-hadadi: “Mwambieni bwana wangu mfalme, ‘Mambo yote ambayo ulitaka mwanzoni mimi mtumishi wako nifanye nitafanya, lakini siwezi kufanya jambo hili.’” Basi wajumbe hao wakaenda zao, wakampelekea ujumbe huo. 10  Kisha Ben-hadadi akatuma ujumbe huu kwake: “Miungu na iniadhibu, tena vikali, ikiwa kuna mavumbi ya kutosha Samaria hivi kwamba kila mtu anayenifuata anaweza kupata konzi moja!” 11  Mfalme wa Israeli akajibu hivi: “Mwambieni, ‘Anayevaa silaha zake hapaswi kujigamba kama mtu anayezivua.’”+ 12  Mara tu Ben-hadadi aliposikia jibu hilo, yeye na wale wafalme walipokuwa wakinywa katika mahema yao,* akawaambia watumishi wake: “Jitayarisheni kushambulia!” Basi wakajitayarisha kushambulia jiji hilo. 13  Lakini nabii fulani akaenda kwa Mfalme Ahabu+ wa Israeli na kumwambia: “Yehova anasema, ‘Je, umeuona umati huu wote mkubwa? Tazama, ninautia mikononi mwako leo, kisha utajua kwamba mimi ni Yehova.’”+ 14  Ahabu akauliza: “Kupitia nani?” Nabii huyo akasema: “Yehova anasema hivi: ‘Kupitia watumishi wa wakuu wa mikoa.’”* Ndipo Ahabu akamuuliza: “Ni nani atakayeanzisha vita?” Nabii huyo akasema: “Ni wewe!” 15  Kisha Ahabu akawahesabu watumishi wa wakuu wa mikoa, nao walikuwa 232; halafu akawahesabu wanaume wote wa Israeli, walikuwa 7,000. 16  Wakaondoka wakati wa adhuhuri Ben-hadadi alipokuwa akinywa na kulewa katika mahema* pamoja na wale wafalme 32 waliokuwa wakimsaidia. 17  Watumishi wa wakuu wa mikoa walipotoka kwanza, mara moja Ben-hadadi akawatuma wajumbe. Wakamletea habari hii: “Wanaume wamekuja kutoka Samaria.” 18  Ndipo akasema: “Ikiwa wamekuja kwa amani, waleteni wakiwa hai; ikiwa wamekuja kwa ajili ya vita, bado mnapaswa kuwaleta wakiwa hai.” 19  Lakini watu hao walipotoka jijini—watumishi wa wakuu wa mikoa na majeshi yaliyokuwa yakiwafuata— 20  kila mmoja wao akamuua adui yake. Ndipo Wasiria wakakimbia,+ na Waisraeli wakawafuatia, lakini Mfalme Ben-hadadi wa Siria akapanda farasi na kutoroka pamoja na baadhi ya wapanda farasi. 21  Lakini mfalme wa Israeli akatoka na kuendelea kuwaua maadui waliopanda farasi na magari, naye akapata ushindi mkubwa dhidi ya Wasiria.* 22  Baadaye nabii huyo+ akaenda kwa mfalme wa Israeli na kumwambia: “Nenda, jiimarishe na ufikirie jambo utakalofanya,+ kwa maana mwanzoni mwa mwaka ujao* mfalme wa Siria atakuja kukushambulia.”+ 23  Sasa watumishi wa mfalme wa Siria wakamwambia: “Mungu wao ni Mungu wa milima. Ndiyo sababu walitushinda nguvu. Lakini tukipigana nao kwenye nchi tambarare, tutawashinda nguvu. 24  Fanya hivi pia: Waondoe wafalme wote+ katika nafasi zao, na mahali pao uweke magavana. 25  Kisha ukusanye* jeshi linalolingana na jeshi ulilopoteza, farasi kwa farasi na gari kwa gari. Acha tupigane nao kwenye nchi tambarare, na hakika tutawashinda nguvu.” Basi akasikiliza ushauri wao na kufanya kama walivyosema. 26  Mwanzoni mwa mwaka,* Ben-hadadi akawakusanya Wasiria, akapanda kwenda Afeki+ ili kupigana na Waisraeli. 27  Waisraeli pia walikusanywa kwa ajili ya vita na kupewa vitu walivyohitaji, nao wakatoka kwenda kukabiliana nao. Waisraeli walipopiga kambi mbele yao, walikuwa kama vikundi viwili vidogo vya mbuzi, lakini Wasiria walijaa kote nchini.+ 28  Kisha yule mtu wa Mungu wa kweli akaenda kwa mfalme wa Israeli na kumwambia: “Yehova anasema hivi, ‘Kwa sababu Wasiria wamesema: “Yehova ni Mungu wa milima, wala si Mungu wa nchi tambarare,” nitautia umati huu wote mkubwa mkononi mwako,+ na hakika utajua kwamba mimi ni Yehova.’”+ 29  Wakaendelea kupiga kambi wakielekeana kwa siku saba, na katika siku ya saba vita vikaanza. Kwa siku moja, Waisraeli wakawaua wanajeshi 100,000 Wasiria wanaotembea kwa miguu. 30  Wanajeshi waliobaki wakakimbilia Afeki,+ ndani ya jiji. Lakini ukuta ukawaangukia wanaume 27,000 kati ya wale waliokuwa wamebaki. Ben-hadadi pia akakimbia na kuingia jijini, akajificha katika chumba fulani cha ndani. 31  Kwa hiyo watumishi wake wakamwambia: “Tazama, tumesikia kwamba wafalme wa nyumba ya Israeli ni wafalme wenye rehema.* Tafadhali, turuhusu tuvae nguo za magunia viunoni na kufunga kamba vichwani kisha twende kwa mfalme wa Israeli. Huenda akakuacha hai.”*+ 32  Basi wakavaa nguo za magunia viunoni na kufunga kamba vichwani, wakaenda kwa mfalme wa Israeli na kumwambia: “Mtumishi wako Ben-hadadi anasema, ‘Tafadhali, niruhusu niishi.’”* Akasema: “Je, angali hai? Yeye ni ndugu yangu.” 33  Basi watu hao wakaliona jambo hilo kuwa ishara njema, na bila kukawia wakaamini maneno yake, wakamwambia: “Ben-hadadi ni ndugu yako.” Kwa hiyo akasema: “Nendeni mkamlete.” Kisha Ben-hadadi akatoka na kwenda kwake, mfalme akampandisha garini. 34  Sasa Ben-hadadi akamwambia: “Majiji ambayo baba yangu alichukua kutoka kwa baba yako nitayarudisha, nawe unaweza kujianzishia masoko* Damasko, kama baba yangu alivyofanya Samaria.” Ahabu akamwambia, “Kwa msingi wa makubaliano haya,* nitakuruhusu uende.” Basi akafanya makubaliano naye na kumruhusu aende zake. 35  Kwa neno la Yehova, mmoja wa wana wa manabii*+ akamwambia mwenzake: “Tafadhali, nipige.” Lakini mtu huyo akakataa kumpiga. 36  Basi akamwambia: “Kwa sababu hukuisikiliza sauti ya Yehova, mara tu tutakapoachana, simba atakuua.” Walipoachana, simba akatokea na kumuua. 37  Akamkuta mtu mwingine na kumwambia: “Tafadhali, nipige.” Mtu huyo akampiga na kumjeruhi. 38  Kisha nabii huyo akaenda na kumsubiri mfalme kando ya barabara, akafunika macho yake kwa kitambaa ili aufiche uso wake. 39  Mfalme alipokuwa akipita, akamlilia mfalme akisema: “Mimi mtumishi wako nilienda sehemu ambayo mapambano yalikuwa makali vitani, na mtu fulani alikuwa akitoka vitani akaniletea mwanamume mmoja na kuniambia, ‘Mlinde mtu huyu. Akitoroka, utalipia uhai wake kwa uhai wako,*+ la sivyo utalipa talanta moja* ya fedha.’ 40  Na mimi mtumishi wako nilipokuwa nikishughulika hapa na pale, kwa ghafla mtu huyo akatoroka.” Mfalme wa Israeli akamwambia: “Hivyo ndivyo utakavyohukumiwa; umejihukumu mwenyewe.” 41  Kisha akaondoa haraka kitambaa kilichofunika macho yake, na mfalme wa Israeli akatambua kwamba alikuwa mmoja wa manabii.+ 42  Mtu huyo akamwambia mfalme: “Yehova anasema hivi: ‘Kwa sababu umemwacha atoroke kutoka mikononi mwako mtu ambaye nilisema anapaswa kuuawa,+ utalipia uhai wake kwa uhai wako,*+ na watu wako watachukua mahali pa watu wake.’”+ 43  Ndipo mfalme wa Israeli akaenda nyumbani Samaria,+ akiwa amesononeka na kuvunjika moyo.

Maelezo ya Chini

Au “vibanda vyao.”
Au “wilaya za utawala.”
Au “vibanda.”
Au “akawachinja Wasiria wengi.”
Yaani, majira yajayo ya kuchipua.
Tnn., “hesabu.”
Yaani, majira ya kuchipua.
Au “upendo mshikamanifu.”
Au “huenda akaiacha hai nafsi yako.”
Au “iruhusu nafsi yangu iishi.”
Au “kujichagulia mitaa.”
Au “agano hili.”
Inaonekana maneno “wana wa manabii” yanarejelea shule ya kuwafundisha manabii au chama cha manabii.
Au “nafsi yake kwa nafsi yako.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Au “nafsi yake kwa nafsi yako.”