Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 5:1-18

  • Mfalme Hiramu ampa Sulemani vifaa vya ujenzi (1-12)

  • Wafanyakazi wa Sulemani walioandikishwa (13-18)

5  Mfalme Hiramu wa Tiro+ aliposikia kwamba Sulemani ametiwa mafuta kuwa mfalme baada ya baba yake, aliwatuma watumishi wake kwa Sulemani, kwa maana sikuzote Hiramu alikuwa rafiki ya Daudi.*+  Naye Sulemani akamtumia Hiramu ujumbe huu:+  “Unajua vizuri kwamba baba yangu Daudi hakuweza kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wake kwa sababu ya watu waliopigana vita naye pande zote, mpaka Yehova alipowaweka maadui wake chini ya nyayo za miguu yake.+  Lakini sasa Yehova Mungu wangu amenipumzisha pande zote.+ Hakuna yeyote anayenipinga na hakuna jambo lolote baya linalotendeka.+  Kwa hiyo ninakusudia kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wangu, kama Yehova alivyomwahidi baba yangu Daudi, akisema: ‘Mwana wako ambaye nitamweka kwenye kiti chako cha ufalme baada yako ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu.’+  Sasa waamuru watu wako wanikatie mierezi ya Lebanoni.+ Watumishi wangu watafanya kazi pamoja na watumishi wako, nami nitawalipa watumishi wako mishahara kulingana na kiwango utakachoweka, kwa maana unajua kwamba hakuna yeyote kati yetu anayejua kukata miti kama Wasidoni.”+  Hiramu aliposikia maneno ya Sulemani, akashangilia sana na kusema: “Yehova na asifiwe leo, kwa maana amempa Daudi mwana mwenye hekima atawale taifa hili kubwa!”*+  Basi Hiramu akampelekea Sulemani ujumbe huu: “Nimepokea ujumbe ulionitumia. Nitatimiza mambo yote unayotaka ili upate mbao za mierezi na za miberoshi.+  Watumishi wangu watateremsha magogo kutoka Lebanoni hadi baharini, nami nitayafunga magogo hayo mafungu-mafungu ili yaelee baharini mpaka mahali utakaponiambia. Nitaagiza yafunguliwe, kisha unaweza kuyabeba. Na wewe utanipa chakula nitakachoomba kwa ajili ya nyumba yangu.”+ 10  Basi Hiramu akampa Sulemani mbao zote za mierezi na za miberoshi ambazo Sulemani alihitaji. 11  Naye Sulemani akampa Hiramu kori 20,000* za ngano kuwa chakula kwa ajili ya nyumba yake na kori 20 za mafuta bora sana ya zeituni.* Hivyo ndivyo vitu ambavyo Sulemani alimpa Hiramu mwaka baada ya mwaka.+ 12  Yehova akampa Sulemani hekima, kama Alivyokuwa amemwahidi.+ Na kulikuwa na amani kati ya Hiramu na Sulemani, nao wakafanya mkataba* kati yao. 13  Mfalme Sulemani aliwaandikisha wanaume kutoka katika Israeli yote ili wafanye kazi ya kulazimishwa; wanaume 30,000 waliandikishwa.+ 14  Alikuwa akiwapeleka wanaume 10,000 Lebanoni kila mwezi kwa zamu. Walikaa Lebanoni kwa mwezi mmoja na kukaa nyumbani kwa miezi miwili; na Adoniramu+ aliwasimamia wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa. 15  Sulemani alikuwa na vibarua* 70,000 na watu 80,000 waliokata mawe+ milimani,+ 16  na pia wakuu wasaidizi+ 3,300 waliowasimamia wafanyakazi. 17  Kwa agizo la mfalme, walichimbua mawe makubwa, mawe yenye thamani,+ ili yachongwe+ na kutumiwa kujenga msingi+ wa nyumba hiyo. 18  Kwa hiyo wajenzi wa Sulemani na wajenzi wa Hiramu na Wagebali+ walikata mawe, na kutayarisha mbao na mawe ya kujengea nyumba hiyo.

Maelezo ya Chini

Au “alimpenda Daudi.”
Au “lenye watu wengi sana.”
Tnn., “za mafuta yaliyopondwapondwa.”
Kori moja ilikuwa sawa na lita 220 (kilogramu 170 hivi). Angalia Nyongeza B14.
Au “agano.”
Au “wabeba mizigo.”