Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 1:1-17
1 Sulemani mwana wa Daudi alizidi kuimarika katika utawala wake, na Yehova Mungu wake alikuwa pamoja naye, akamfanya kuwa mkuu sana.+
2 Sulemani aliagiza Waisraeli wote wakusanywe, wakuu wa maelfu na wa mamia, waamuzi, na viongozi wote wa Israeli, viongozi wa koo.*
3 Kisha Sulemani na Waisraeli wote wakaenda mahali pa juu kule Gibeoni,+ kwa maana hema la mkutano la Mungu wa kweli lilikuwa huko, hema ambalo Musa mtumishi wa Yehova alitengeneza nyikani.
4 Hata hivyo, Daudi alikuwa amelipandisha Sanduku la Mungu wa kweli kutoka Kiriath-yearimu+ na kulileta mahali ambapo Daudi alikuwa ametayarisha kwa ajili yake; alikuwa amepiga hema kwa ajili ya Sanduku hilo huko Yerusalemu.+
5 Na ile madhabahu ya shaba+ ambayo Bezaleli+ mwana wa Uri mwana wa Huru alikuwa ametengeneza ilikuwa imewekwa mbele ya hema la ibada la Yehova; na Sulemani na Waisraeli wote walikuwa wakisali mbele yake.*
6 Kisha Sulemani akamtolea Yehova dhabihu mahali hapo, alitoa dhabihu 1,000 za kuteketezwa kwenye madhabahu ya shaba+ ya hema la mkutano.
7 Usiku huo Mungu akamtokea Sulemani na kumwambia: “Niombe unachotaka nikupe.”+
8 Basi Sulemani akamwambia Mungu: “Umemtendea Daudi+ baba yangu kwa upendo mwingi mshikamanifu, nawe umeniweka kuwa mfalme baada yake.+
9 Sasa, Ee Yehova Mungu, ahadi uliyompa Daudi baba yangu na ithibitike kuwa ya uaminifu,+ kwa maana umeniweka kuwa mfalme juu ya watu wengi sana kama chembe za mavumbi ya dunia.+
10 Sasa nipe hekima na ujuzi+ ili niwaongoze watu hawa,* kwa maana ni nani anayeweza kulihukumu taifa hili lako lililo kubwa?”+
11 Kisha Mungu akamwambia Sulemani: “Kwa sababu moyo wako unatamani jambo hilo, nawe hukuomba mali, utajiri, wala heshima wala hukuomba wale wanaokuchukia wafe, wala hukuomba maisha marefu,* lakini umeomba hekima na ujuzi ili uwahukumu watu wangu ambao nimekuweka uwe mfalme wao,+
12 nitakupa hekima na ujuzi; lakini nitakupa pia mali na utajiri na heshima, kuliko mfalme yeyote kabla yako na mfalme yeyote baada yako.”+
13 Basi Sulemani akatoka mahali pa juu huko Gibeoni,+ kutoka mbele ya hema la mkutano, akaja Yerusalemu; naye akatawala Israeli.
14 Sulemani akaendelea kukusanya magari ya vita na farasi;* akawa na magari 1,400 ya vita na farasi* 12,000,+ naye aliwaweka katika majiji ya magari ya vita+ karibu naye huko Yerusalemu.+
15 Mfalme alifanya fedha na dhahabu huko Yerusalemu iwe nyingi kama mawe,+ na mbao za mierezi ziwe nyingi kama mikuyu katika Shefela.+
16 Farasi wa Sulemani waliletwa kutoka Misri,+ na wafanyabiashara wa mfalme walinunua makundi ya farasi* kwa bei moja.+
17 Kila gari kutoka Misri lilinunuliwa kwa vipande 600 vya fedha, na farasi alinunuliwa kwa vipande 150; kisha waliwauzia wafalme wote wa Wahiti na wafalme wa Siria.
Maelezo ya Chini
^ Yaani, ukoo wa upande wa baba.
^ Au “walikuwa wakitafuta ushauri Wake hapo.”
^ Tnn., “nitoke nje mbele ya watu hawa na kurudi ndani.”
^ Tnn., “siku nyingi.”
^ Au “wapanda farasi.”
^ Au “wapanda farasi.”
^ Au labda, “kutoka Misri na kutoka Kue; wafanyabiashara wa mfalme waliwanunua kutoka Kue,” huenda ni Kilikia.