Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 12:1-16

  • Shishaki ashambulia Yerusalemu (1-12)

  • Mwisho wa utawala wa Rehoboamu (13-16)

12  Mara tu baada ya utawala wa Rehoboamu kuimarika kabisa,+ naye akawa na nguvu, aliiacha Sheria ya Yehova,+ na Waisraeli wote pia wakaiacha.  Katika mwaka wa tano wa utawala wa Mfalme Rehoboamu, Mfalme Shishaki+ wa Misri alishambulia Yerusalemu, kwa maana hawakuwa waaminifu kwa Yehova.  Alikuwa na magari 1,200 ya vita, wapanda farasi 60,000, na idadi isiyohesabika ya wanajeshi waliokuja pamoja naye kutoka Misri—Walibya, Wasukii, na Waethiopia.+  Aliyateka majiji yenye ngome ya Yuda na mwishowe akafika Yerusalemu.  Nabii Shemaya+ akaja kwa Rehoboamu na wakuu wa Yuda waliokuwa wamekusanyika Yerusalemu kwa sababu ya Shishaki, akawaambia: “Yehova anasema hivi, ‘Mmeniacha mimi, nami pia nimewaacha ninyi mikononi+ mwa Shishaki.’”  Ndipo wakuu wa Israeli na mfalme wakajinyenyekeza+ na kusema: “Yehova ni mwadilifu.”  Yehova alipoona kwamba wamejinyenyekeza, neno la Yehova likamjia Shemaya likisema: “Wamejinyenyekeza. Sitawaangamiza,+ na baada ya muda mfupi nitawaokoa. Sitalimwagia jiji la Yerusalemu ghadhabu yangu kupitia Shishaki.  Lakini watakuwa watumishi wake, ili wajue tofauti kati ya kunitumikia mimi na kuwatumikia wafalme wa* nchi nyingine.”  Basi Mfalme Shishaki wa Misri akashambulia Yerusalemu. Akachukua hazina za nyumba ya Yehova+ na hazina za nyumba ya* mfalme. Alichukua kila kitu, kutia ndani ngao za dhahabu ambazo Sulemani alikuwa ametengeneza.+ 10  Basi Mfalme Rehoboamu akatengeneza ngao za shaba zichukue mahali pa ngao hizo, akaziweka chini ya ulinzi wa mkuu wa walinzi,* aliyelinda mlango wa nyumba ya mfalme. 11  Wakati wowote ambapo mfalme alikuja katika nyumba ya Yehova, walinzi waliingia ndani na kuzichukua, kisha walizirudisha katika chumba cha walinzi. 12  Kwa sababu mfalme alijinyenyekeza, hasira ya Yehova iliacha kuwaka dhidi yake,+ naye hakuwaangamiza kabisa.+ Isitoshe, kulikuwa na mambo fulani mema yaliyopatikana nchini Yuda.+ 13  Mfalme Rehoboamu aliimarisha mamlaka yake jijini Yerusalemu na kuendelea kutawala; Rehoboamu alikuwa na umri wa miaka 41 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 17 huko Yerusalemu, jiji ambalo Yehova alichagua miongoni mwa makabila yote ya Israeli ili kuweka jina lake humo. Mama yake aliitwa Naama, naye alikuwa Mwamoni.+ 14  Lakini alitenda maovu, kwa maana hakuwa ameazimia moyoni mwake kumtafuta Yehova.+ 15  Na historia ya Rehoboamu, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, je, haijaandikwa katika maandishi ya nabii Shemaya+ na mwonaji Ido+ katika kumbukumbu za ukoo? Kulikuwa na vita daima kati ya Rehoboamu na Yeroboamu.+ 16  Kisha Rehoboamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi;+ na Abiya+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Tnn., “kutumikia falme za.”
Au “jumba la.”
Tnn., “wakimbiaji.”