Kitabu cha Pili cha Mambo ya Nyakati 6:1-42

  • Hotuba ya Sulemani (1-11)

  • Sala ya Sulemani ya kuzindua hekalu (12-42)

6  Wakati huo Sulemani alisema: “Yehova alisema kwamba atakaa katika giza zito.+  Sasa nimekujengea nyumba iliyokwezwa, mahali palipofanywa imara ili ukae humo milele.”+  Kisha mfalme akageuka na kuanza kulibariki kutaniko lote la Waisraeli huku kutaniko lote la Waisraeli likiwa limesimama.+  Akasema: “Na asifiwe Yehova Mungu wa Israeli, ambaye kwa kinywa chake mwenyewe alimwahidi baba yangu Daudi, na kwa mkono wake mwenyewe ametimiza, akisema,  ‘Kuanzia siku niliyowatoa watu wangu nchini Misri, sijachagua jiji katika makabila yote ya Israeli na kujenga humo nyumba ili jina langu likae humo,+ nami sijamchagua mwanamume atakayekuwa kiongozi wa watu wangu Waisraeli.  Lakini nimechagua Yerusalemu+ ili jina langu likae humo, nami nimemchagua Daudi awatawale watu wangu Waisraeli.’+  Na moyo wa Daudi baba yangu ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli.+  Lakini Yehova akamwambia Daudi baba yangu, ‘Moyo wako ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina langu, na ulifanya vizuri kutamani jambo hilo moyoni mwako.  Hata hivyo, hutajenga nyumba hiyo, lakini mwana wako mwenyewe utakayemzaa* ndiye atakayeijenga nyumba hiyo kwa ajili ya jina langu.’+ 10  Yehova ametimiza ahadi hiyo aliyoitoa, kwa maana nimechukua mahali pa baba yangu Daudi na kuketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli,+ kama Yehova alivyoahidi.+ Pia nimejenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli, 11  na humo nimeliweka Sanduku lenye agano+ ambalo Yehova alifanya na Waisraeli.” 12  Kisha akasimama mbele ya madhabahu ya Yehova mbele ya kutaniko lote la Waisraeli, akanyoosha mikono yake.+ 13  (Kwa maana Sulemani alikuwa amejenga jukwaa la shaba na kuliweka katikati ya ua.+ Lilikuwa na urefu wa mikono mitano,* upana wa mikono mitano, na kimo cha mikono mitatu; akasimama juu yake.) Akapiga magoti mbele ya kutaniko lote la Waisraeli na kunyoosha mikono yake kuelekea mbinguni,+ 14  akasema: “Ee Yehova Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe mbinguni wala duniani, unayeshika agano na kuwatendea kwa upendo mshikamanifu watumishi wako wanaotembea mbele zako kwa moyo wao wote.+ 15  Umetimiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu.+ Ulitoa ahadi hiyo kwa kinywa chako mwenyewe, na siku ya leo umeitimiza kwa mkono wako mwenyewe.+ 16  Na sasa, Ee Yehova Mungu wa Israeli, timiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ulipomwambia, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli mbele zangu, ikiwa tu wana wako watakazia uangalifu njia yao kwa kutembea katika sheria yangu,+ kama ulivyotembea mbele zangu.’+ 17  Na sasa, Ee Yehova Mungu wa Israeli, acha ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ithibitike kuwa ya kweli. 18  “Lakini Ee Mungu, je, kweli utakaa duniani pamoja na wanadamu?+ Tazama! Mbingu, naam, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha;+ sembuse nyumba hii niliyoijenga!+ 19  Sasa sikiliza sala yangu mimi mtumishi wako na ombi langu la kutaka kibali, Ee Yehova Mungu wangu, sikiliza kilio changu cha kuomba msaada na sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali mbele zako. 20  Macho yako na yatazame nyumba hii usiku na mchana, yatazame mahali ambapo ulisema kwamba utaweka jina lako,+ ili usikilize sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali kuelekea mahali hapa. 21  Nawe usikilize sihi zangu mimi mtumishi wako za kuomba msaada na sihi za watu wako Waisraeli wanaposali kuelekea mahali hapa,+ nawe usikilize katika makao yako, kutoka mbinguni;+ naam, usikilize na kusamehe.+ 22  “Mwanadamu akimtendea dhambi mwanadamu mwenzake, naye aapishwe* na kuwekwa chini ya wajibu wa kiapo hicho,* naye akiwa chini ya kiapo* aje mbele ya madhabahu yako katika nyumba hii,+ 23  basi usikie kutoka mbinguni na kuchukua hatua na kuwahukumu watumishi wako kwa kumlipa mwovu na kumwadhibu kwa sababu ya jambo alilotenda*+ na kumtangaza mwadilifu kuwa asiye na hatia* na kumthawabisha kulingana na uadilifu wake mwenyewe.+ 24  “Na watu wako Waisraeli wakishindwa na maadui kwa sababu ya kuzidi kukutendea dhambi,+ nao warudi na kulitukuza jina lako+ na kusali+ na kukusihi wapate kibali mbele zako katika nyumba hii,+ 25  basi usikie kutoka mbinguni+ na kuwasamehe watu wako Waisraeli dhambi yao na kuwarudisha katika nchi uliyowapa wao na mababu zao.+ 26  “Mbingu zikifungwa kusiwe na mvua+ kwa sababu wamezidi kukutendea dhambi,+ nao wasali kuelekea mahali hapa na kulitukuza jina lako na kuacha dhambi yao kwa sababu umewanyenyekeza,*+ 27  basi usikie kutoka mbinguni na kuwasamehe watumishi wako dhambi yao, dhambi ya watu wako Waisraeli, kwa sababu utawafundisha njia nzuri wanayopaswa kutembea ndani yake;+ na ulete mvua+ katika nchi yako ambayo uliwapa watu wako kuwa urithi. 28  “Njaa kali ikitokea nchini,+ au ugonjwa hatari,+ upepo unaochoma, kuvu,+ makundi ya nzige, au parare* wanaokula sana+ au maadui wao wakiwazingira katika jiji lolote nchini*+ au pigo au ugonjwa wa aina yoyote ukitokea,+ 29  sala yoyote,+ ombi lolote la kutaka kibali+ ambalo huenda likatolewa na mtu yeyote au na watu wako wote Waisraeli (kwa sababu kila mmoja anajua mateso yake mwenyewe na maumivu yake mwenyewe)+ wakinyoosha mikono yao kuelekea nyumba hii,+ 30  basi usikie kutoka mbinguni, makao yako,+ nawe usamehe;+ na umthawabishe kila mmoja kulingana na njia zake zote, kwa sababu unajua moyo wake (ni wewe peke yako unayejua vizuri moyo wa mwanadamu),+ 31  ili wakuogope kwa kutembea katika njia zako sikuzote watakazoishi katika nchi uliyowapa mababu zetu. 32  “Pia mgeni ambaye si sehemu ya watu wako Waisraeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako kuu*+ na mkono wako wenye nguvu na mkono wako ulionyooshwa, akija na kusali kuelekea nyumba hii,+ 33  basi usikilize kutoka mbinguni, makao yako, nawe ufanye mambo yote ambayo mgeni huyo anakuomba ufanye, ili watu wote duniani wajue jina lako+ na kukuogopa, kama watu wako Waisraeli wanavyokuogopa, na ili wajue kwamba nyumba hii niliyojenga imeitwa kwa jina lako. 34  “Watu wako wakienda vitani kupigana na maadui wao mahali utakapowaelekeza+ nao wasali+ kwako kuelekea jiji hili ambalo umechagua na kuelekea nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako,+ 35  basi usikie kutoka mbinguni sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao.+ 36  “Wakikutendea dhambi (kwa sababu hakuna mwanadamu asiyetenda dhambi),+ nawe uwakasirikie vikali na kuwaacha mikononi mwa maadui, na waliowateka wawapeleke katika nchi fulani, mbali au karibu,+ 37  nao warudiwe na ufahamu wakiwa katika nchi ya watu waliowachukua mateka, na kukurudia na kukuomba kibali katika nchi walikopelekwa mateka, wakisema, ‘Tumetenda dhambi na kukosea; tumetenda uovu,’+ 38  nao wakurudie kwa moyo wao wote+ na kwa nafsi* yao yote katika nchi walikopelekwa mateka,+ nao wasali kwako kuelekea nchi yao ambayo uliwapa mababu zao na kuelekea jiji ambalo umelichagua+ na nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako, 39  basi usikie kutoka mbinguni, makao yako, sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao+ na uwasamehe watu wako ambao wamekutendea dhambi. 40  “Sasa, Ee Mungu wangu, tafadhali, macho yako yatazame na masikio yako yasikilize kwa makini sala inayotolewa* mahali hapa.+ 41  Na sasa, Ee Yehova Mungu, panda uingie mahali pako pa kupumzikia,+ wewe pamoja na Sanduku la nguvu zako. Makuhani wako, Ee Yehova Mungu, na wavishwe wokovu, na acha washikamanifu wako washangilie kwa sababu ya wema wako.+ 42  Ee Yehova Mungu, usimkatae* mtiwa-mafuta wako.+ Ukumbuke upendo wako mshikamanifu kwa Daudi mtumishi wako.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “mwana wako, atakayetoka katika viuno vyako.”
Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Au “aliyetendewa dhambi akimweka chini ya laana.” Yaani, kiapo kinacholeta laana ikiwa mtu anaapa kwa uwongo au kukosa kutimiza kiapo hicho.
Tnn., “laana.”
Tnn., “laana.”
Tnn., “kuwa mwadilifu.”
Tnn., “kuleta juu ya kichwa chake mwenyewe jambo alilotenda.”
Au “umewatesa.”
Tnn., “katika nchi ya malango yake.”
Au “panzi.”
Au “sifa yako.”
Angalia Kamusi.
Au “inayohusu.”
Tnn., “usiugeuzie mbali uso wa.”