Kitabu cha Pili cha Samweli 24:1-25

  • Dhambi ya Daudi ya kuwahesabu watu (1-14)

  • Ugonjwa hatari wasababisha vifo vya watu 70,000 (15-17)

  • Daudi ajenga madhabahu (18-25)

    • Hatatoa dhabihu ambazo hazimgharimu (24)

24  Hasira ya Yehova ikawaka tena dhidi ya Waisraeli+ mtu fulani alipomchochea Daudi* atende kinyume chao kwa kumwambia: “Nenda, ukawahesabu+ watu wa Israeli na Yuda.”+  Basi mfalme akamwambia Yoabu+ mkuu wa jeshi aliyekuwa pamoja naye: “Tafadhali nenda katika makabila yote ya Israeli, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba,+ uwaandikishe watu, ili nijue idadi yao.”  Lakini Yoabu akamwambia mfalme: “Yehova Mungu wako na azidishe idadi ya watu mara 100, na macho yako bwana wangu mfalme na yaone jambo hilo, lakini kwa nini bwana wangu mfalme unataka kufanya jambo la namna hii?”  Lakini neno la mfalme likawa na nguvu kuliko neno la Yoabu na wakuu wa jeshi. Basi Yoabu na wakuu wa jeshi wakaondoka mbele ya mfalme na kwenda kuwaandikisha watu wa Israeli.+  Wakavuka Yordani na kupiga kambi Aroeri,+ upande wa kulia* wa jiji katikati ya bonde, kuelekea kwa Wagadi, na mpaka Yazeri.+  Kisha wakaenda mpaka Gileadi+ na nchi ya Tahtim-hodshi, wakaendelea mpaka Dani-yaani nao wakazunguka mpaka Sidoni.+  Kisha wakaenda kwenye ngome ya Tiro+ na katika majiji yote ya Wahivi+ na ya Wakanaani, mwishowe wakafika Negebu+ ya Yuda kule Beer-sheba.+  Kwa hiyo wakapita katika nchi yote na kurudi Yerusalemu baada ya miezi tisa na siku 20.  Basi Yoabu akampa mfalme idadi ya watu walioandikishwa. Mashujaa wa Israeli waliojihami kwa mapanga walikuwa 800,000, na wanaume wa Yuda walikuwa 500,000.+ 10  Lakini moyo wa Daudi ukajaa* majuto+ baada ya kuwahesabu watu. Basi Daudi akamwambia Yehova: “Nimetenda dhambi+ kubwa kwa kufanya jambo hili. Na sasa, Yehova, tafadhali nisamehe kosa langu mimi mtumishi wako,+ kwa maana nimetenda kwa upumbavu sana.”+ 11  Daudi alipoamka asubuhi, neno la Yehova likamjia nabii Gadi,+ mwonaji wa Daudi, likisema: 12  “Nenda ukamwambie Daudi, ‘Yehova anasema hivi: “Ninakupa mambo matatu ya kuchagua. Chagua jambo nitakalokutendea.”’”+ 13  Basi Gadi akaenda kwa Daudi na kumwambia: “Je, unataka njaa kali ije katika nchi yako kwa miaka saba?+ Au unataka kuwakimbia maadui wako kwa miezi mitatu huku wakikufuatia? + Au unataka nchi yako ikumbwe na ugonjwa hatari kwa siku tatu?+ Sasa fikiria kwa makini jibu ninalopaswa kumpa Yule aliyenituma.” 14  Kwa hiyo Daudi akamwambia Gadi: “Jambo hilo linanihuzunisha sana. Tafadhali, acha tuanguke mkononi mwa Yehova,+ kwa maana rehema zake ni nyingi;+ lakini usiniache nianguke mkononi mwa mwanadamu.”+ 15  Ndipo Yehova akaleta ugonjwa hatari+ Israeli kuanzia asubuhi mpaka wakati uliowekwa, hivi kwamba watu 70,000 wakafa+ kuanzia Dani mpaka Beer-sheba.+ 16  Malaika alipounyoosha mkono wake kuelekea jiji la Yerusalemu ili kuliangamiza, Yehova akaghairi* kwa sababu ya msiba huo,+ akamwambia malaika aliyekuwa akiwaangamiza watu: “Imetosha! Sasa shusha mkono wako.” Malaika wa Yehova alikuwa karibu na uwanja wa kupuria nafaka wa Arauna+ Myebusi.+ 17  Daudi alipomwona malaika aliyekuwa akiwaangamiza watu, akamwambia Yehova: “Mimi ndiye niliyetenda dhambi, na mimi ndiye niliyekosea; lakini kondoo hawa+—wamefanya nini? Tafadhali, acha mkono wako uniadhibu mimi na nyumba ya baba yangu.”+ 18  Basi Gadi akaenda kwa Daudi siku hiyo na kumwambia: “Panda ukamjengee Yehova madhabahu kwenye uwanja wa kupuria nafaka wa Arauna Myebusi.”+ 19  Basi Daudi akapanda kulingana na neno la Gadi, kama Yehova alivyoamuru. 20  Arauna alipotazama chini na kumwona mfalme na watumishi wake wakija kumwelekea, mara moja Arauna akatoka nje na kumwinamia mfalme kifudifudi. 21  Arauna akamuuliza: “Bwana wangu mfalme kwa nini umekuja kwangu mimi mtumishi wako?” Daudi akamjibu: “Kununua uwanja wako wa kupuria ili nimjengee Yehova madhabahu, ili ugonjwa hatari ambao umewakumba watu ukomeshwe.”+ 22  Lakini Arauna akamwambia Daudi: “Bwana wangu mfalme uchukue na kutoa unachoona ni chema.* Ndio hawa ng’ombe kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa na kifaa cha kupuria nafaka na nira za ng’ombe utakazotumia kama kuni. 23  Ee mfalme, mimi Arauna nimekupa vitu hivi vyote.” Kisha Arauna akamwambia mfalme: “Yehova Mungu wako na akupe kibali.” 24  Hata hivyo, mfalme akamwambia Arauna: “Hapana, ni lazima niununue kwa bei fulani. Sitamtolea Yehova Mungu wangu dhabihu za kuteketezwa ambazo hazinigharimu chochote.” Basi Daudi akanunua uwanja huo wa kupuria nafaka na hao ng’ombe kwa shekeli 50 za fedha.*+ 25  Kisha Daudi akamjengea Yehova madhabahu+ mahali hapo na kutoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika. Ndipo Yehova akakubali maombi ya kusihi yaliyotolewa kwa ajili ya nchi,+ na ugonjwa hatari uliowakumba Waisraeli ukakomeshwa.

Maelezo ya Chini

Au “Daudi alipochochewa.”
Au “kusini.”
Au “dhamiri ya Daudi ikajaa.”
Au “akahuzunika.”
Tnn., “kilicho chema machoni pako.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.