Kitabu cha Pili cha Samweli 9:1-13

  • Daudi amtendea Mefiboshethi kwa upendo mshikamanifu (1-13)

9  Kisha Daudi akauliza: “Je, kuna yeyote aliyebaki katika nyumba ya Sauli ninayeweza kumtendea kwa upendo mshikamanifu kwa ajili ya Yonathani?”+  Basi kulikuwa na mtumishi wa nyumba ya Sauli aliyeitwa Siba.+ Kwa hiyo wakamwita aje kwa Daudi, na mfalme akamuuliza: “Je, wewe ni Siba?” Akajibu: “Ni mimi mtumishi wako.”  Mfalme akaendelea kumuuliza: “Je, kuna yeyote aliyebaki katika nyumba ya Sauli ninayeweza kumtendea kwa upendo mshikamanifu wa Mungu?” Siba akamjibu hivi mfalme: “Bado kuna mwana mmoja wa Yonathani; amelemaa miguu yote miwili.”*+  Mfalme akamuuliza: “Yuko wapi?” Siba akamjibu mfalme: “Yuko katika nyumba ya Makiri+ mwana wa Amieli kule Lo-debari.”  Mara moja Mfalme Daudi akaagiza aletwe kutoka katika nyumba ya Makiri mwana wa Amieli kule Lo-debari.  Mefiboshethi mwana wa Yonathani mwana wa Sauli alipofika mbele ya Daudi, mara moja alianguka chini kifudifudi na kumwinamia. Daudi akasema: “Mefiboshethi!” naye akajibu: “Mimi hapa, mtumishi wako.”  Daudi akamwambia: “Usiogope, kwa maana hakika nitakutendea kwa upendo mshikamanifu+ kwa ajili ya Yonathani baba yako, nami nitakurudishia ardhi yote ya Sauli babu yako, nawe utakula chakula* mezani pangu sikuzote.”+  Basi akainama na kusema: “Mimi mtumishi wako ni nani, hivi kwamba umenitendea kwa fadhili* mbwa mfu+ kama mimi?”  Sasa mfalme akaagiza Siba mtumishi wa Sauli aitwe, akamwambia: “Kila kitu ambacho kilikuwa cha Sauli na nyumba yake yote ninampa mjukuu wa bwana wako.+ 10  Wewe na wana wako na watumishi wako mtamlimia shamba lake, nanyi mtayakusanya mavuno ya shamba hilo ili watu wa nyumbani mwa mjukuu wa bwana wako wapate chakula. Lakini Mefiboshethi, mjukuu wa bwana wako, atakula chakula mezani pangu sikuzote.”+ Siba alikuwa na wana 15 na watumishi 20.+ 11  Ndipo Siba akamwambia mfalme: “Mimi mtumishi wako nitafanya mambo yote ambayo bwana wangu mfalme unaniamuru mimi mtumishi wako nifanye.” Basi Mefiboshethi akawa akila kwenye meza ya Daudi* kama mmoja wa wana wa mfalme. 12  Sasa Mefiboshethi pia alikuwa na mtoto mdogo wa kiume aliyeitwa Mika;+ na watu wote walioishi katika nyumba ya Siba wakawa watumishi wa Mefiboshethi. 13  Naye Mefiboshethi aliishi Yerusalemu kwa maana sikuzote alikula mezani pa mfalme;+ na miguu yake ilikuwa imelemaa.+

Maelezo ya Chini

Au “ni kiwete.”
Tnn., “mkate.”
Tnn., “umegeuza uso wako kuelekea.”
Au labda, “meza yangu.”