Kitabu cha Pili cha Wafalme 10:1-36

  • Yehu awaua watu wa nyumba ya Ahabu (1-17)

    • Yehonadabu ajiunga na Yehu (15-17)

  • Yehu awaua waabudu wa Baali (18-27)

  • Maelezo kuhusu utawala wa Yehu (28-36)

10  Sasa Ahabu+ alikuwa na wana 70 kule Samaria. Kwa hiyo Yehu akaandika barua, akazituma Samaria kwa wakuu wa Yezreeli, wazee,+ na walezi wa watoto wa Ahabu,* akisema:  “Sasa barua hii itakapowafikia ninyi, wana wa bwana wenu watakuwa pamoja nanyi, na pia mtakuwa na magari ya vita, farasi, jiji lenye ngome, na silaha.  Chagueni mwana bora na anayefaa* kabisa kati ya wana wa bwana wenu na mumweke kwenye kiti cha ufalme cha baba yake. Kisha mpigane vita kwa ajili ya nyumba ya bwana wenu.”  Lakini wakaogopa sana na kusema: “Tazama! Ikiwa wafalme wawili hawakuweza kupigana naye,+ sisi tutawezaje kupigana naye?”  Basi msimamizi wa jumba la mfalme,* gavana wa jiji, wazee, na wale walezi wakamtumia Yehu ujumbe huu: “Sisi ni watumishi wako, nasi tutafanya mambo yote utakayotuambia. Hatutamweka yeyote kuwa mfalme. Fanya jambo lolote unaloona ni jema machoni pako.”  Ndipo Yehu akawaandikia barua ya pili, akisema: “Ikiwa mko upande wangu na mko tayari kunitii, leteni vichwa vya wana wa bwana wenu na mje kwangu kesho wakati kama huu kule Yezreeli.” Wana 70 wa mfalme walikuwa pamoja na wanaume mashuhuri wa jiji waliokuwa wakiwalea.  Mara tu barua hiyo ilipowafikia, wakawachukua wana wa mfalme, wanaume 70,+ na kuwachinja, kisha wakaweka vichwa vyao ndani ya vikapu, wakampelekea kule Yezreeli.  Mjumbe akaenda kwa Yehu na kumwambia: “Wameleta vichwa vya wana wa mfalme.” Kwa hiyo akasema: “Viwekeni katika marundo mawili kwenye lango la jiji mpaka asubuhi.”  Yehu alipotoka asubuhi, alisimama mbele ya watu wote na kuwaambia: “Ninyi hamna hatia.* Naam, nilipanga njama dhidi ya bwana wangu, nikamuua,+ lakini ni nani aliyewaua hawa wote? 10  Basi jueni kwamba hakuna neno hata moja la Yehova ambalo Yehova amesema dhidi ya nyumba ya Ahabu litakalokosa kutimia,*+ na Yehova amefanya yale aliyosema kupitia mtumishi wake Eliya.”+ 11  Basi Yehu akawaua watu wote waliobaki wa nyumba ya Ahabu kule Yezreeli, na pia watu wake wote mashuhuri, marafiki zake, na makuhani wake,+ hakumwacha mtu yeyote wa nyumba yake akiwa hai.+ 12  Kisha akaondoka na kuelekea Samaria. Njiani kulikuwa na nyumba ya kuwakatia kondoo manyoya. 13  Huko Yehu akakutana na ndugu za Mfalme Ahazia+ wa Yuda, naye akawauliza, “Ninyi ni nani?” Wakasema: “Sisi ni ndugu za Ahazia, nasi tunashuka kwenda kuwajulia hali wana wa mfalme na wana wa mama malkia.” 14  Mara moja akasema: “Wakamateni wakiwa hai!” Basi wakawakamata wanaume 42 wakiwa hai na kuwachinja kando ya tangi la maji la nyumba ya kuwakatia kondoo manyoya. Hakumwacha yeyote kati yao akiwa hai.+ 15  Alipokuwa akiondoka mahali hapo, alikutana na Yehonadabu+ mwana wa Rekabu+ akija kumpokea. Yehu akamsalimia* na kumuuliza: “Je, moyo wako ni kamili* kunielekea, kama moyo wangu ulivyo kamili kukuelekea?” Yehonadabu akajibu: “Ndiyo.” “Ikiwa ndivyo, nipe mkono wako.” Kwa hiyo akampa mkono wake, na Yehu akamvuta na kumpandisha kwenye gari lake. 16  Kisha akasema: “Twende pamoja, uone kwamba sivumilii ushindani wowote kumwelekea* Yehova.”+ Basi wakaenda pamoja naye katika gari lake la vita. 17  Kisha Yehu akafika Samaria na kuwaua watu wote waliobaki wa nyumba ya Ahabu huko Samaria mpaka alipowaangamiza wote,+ kulingana na neno la Yehova alilomwambia Eliya.+ 18  Tena Yehu akawakusanya watu wote na kuwaambia: “Ahabu alimwabudu Baali kwa kiwango kidogo tu,+ lakini Yehu atamwabudu kwa kiwango kikubwa zaidi. 19  Basi wakusanyeni manabii wote wa Baali,+ waabudu wake wote, na makuhani wake wote+ waje kwangu. Hakikisheni kwamba hakuna hata mmoja atakayekosa kufika, kwa sababu nina dhabihu kubwa kwa ajili ya Baali. Yeyote atakayekosa kufika hataishi.” Lakini Yehu alikuwa akitenda kwa ujanja ili awaangamize waabudu wa Baali. 20  Yehu akaendelea kusema: “Tangazeni* kusanyiko takatifu kwa ajili ya Baali.” Basi wakalitangaza. 21  Kisha Yehu akatuma ujumbe kotekote katika Israeli, na waabudu wote wa Baali wakaja. Hakuna hata mmoja wao ambaye hakuja. Wakaingia katika nyumba ya* Baali,+ na nyumba ya Baali ikajaa kutoka mwisho mmoja hadi mwisho mwingine. 22  Akamwambia msimamizi wa chumba cha mavazi: “Leta mavazi kwa ajili ya waabudu wote wa Baali.” Basi akawaletea mavazi. 23  Halafu Yehu na Yehonadabu+ mwana wa Rekabu wakaingia katika nyumba ya Baali. Yehu akawaambia waabudu wa Baali: “Tafuteni kwa uangalifu mhakikishe kwamba hakuna mwabudu yeyote wa Yehova humu ndani isipokuwa waabudu wa Baali.” 24  Mwishowe wakaingia ndani ili kutoa dhabihu mbalimbali na dhabihu za kuteketezwa. Yehu alikuwa ameweka wanaume wake 80 nje na kuwaambia, “Yeyote kati ya wanaume ninaowatia mikononi mwenu akiponyoka, mtalipia uhai wake kwa uhai wenu.”* 25  Mara tu alipomaliza kutoa dhabihu ya kuteketezwa, Yehu akawaambia hivi walinzi* na makamanda wasaidizi: “Ingieni ndani na kuwaua! Msimwache yeyote aponyoke!”+ Basi walinzi na makamanda wasaidizi wakawaua kwa upanga na kuwatupa nje, wakaingia mpaka kwenye chumba kitakatifu cha ndani cha* nyumba hiyo ya Baali. 26  Kisha wakatoa nje nguzo takatifu+ za nyumba ya Baali na kuiteketeza kila nguzo.+ 27  Wakabomoa nguzo takatifu+ ya Baali na kuibomoa nyumba ya Baali,+ na kuigeuza kuwa vyoo, na hivyo ndivyo ilivyo mpaka leo. 28  Kwa hiyo Yehu akakomesha kabisa ibada ya Baali katika Israeli. 29  Hata hivyo, Yehu hakugeuka na kuacha dhambi ambazo Yeroboamu mwana wa Nebati alisababisha Waisraeli kutenda kuhusiana na wale ndama wa dhahabu waliokuwa Betheli na Dani.+ 30  Basi Yehova akamwambia Yehu: “Kwa kuwa umetenda vema na umefanya yaliyo sawa machoni pangu kwa kutenda mambo yote yaliyokuwa moyoni mwangu niliyokusudia kuitendea nyumba ya Ahabu,+ vizazi vinne vya wana wako vitaketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli.”+ 31  Lakini Yehu hakuwa mwangalifu kutembea katika Sheria ya Yehova Mungu wa Israeli kwa moyo wake wote.+ Hakugeuka na kuacha dhambi ambazo Yeroboamu alisababisha Waisraeli kutenda.+ 32  Siku hizo Yehova alianza kupunguza* eneo la Israeli, eneo moja baada ya lingine. Hazaeli akaendelea kuwashambulia kotekote katika eneo la Israeli,+ 33  kuanzia Yordani kuelekea mashariki, nchi yote ya Gileadi—ya watu wa kabila la Gadi, Rubeni, na Manase+—kutoka Aroeri, jiji lililo kando ya Bonde la Arnoni,* mpaka Gileadi na Bashani.+ 34  Na mambo mengine katika historia ya Yehu, mambo yote aliyofanya na ukuu wake, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 35  Kisha Yehu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake huko Samaria; na Yehoahazi mwana wake+ akawa mfalme baada yake. 36  Yehu alitawala Israeli kwa miaka 28 akiwa Samaria.

Maelezo ya Chini

Tnn., “walezi wa Ahabu.”
Au “mnyoofu.”
Tnn., “nyumba.”
Au “Ninyi ni waadilifu.”
Tnn., “litakaloanguka ardhini.”
Au “akambariki.”
Tnn., “mnyoofu.”
Au “uone bidii yangu kwa ajili ya.”
Tnn., “Takaseni.”
Au “hekalu la.”
Au “mtalipia nafsi yake kwa nafsi yenu.”
Tnn., “wakimbiaji.”
Tnn., “kwenye jiji la,” labda ni jengo lililokuwa kama ngome.
Tnn., “kukata.”
Au “Korongo la Arnoni.”