Kitabu cha Pili cha Wafalme 12:1-21

  • Yehoashi, mfalme wa Yuda (1-3)

  • Yehoashi arekebisha hekalu (4-16)

  • Wasiria wavamia (17, 18)

  • Yehoashi auawa (19-21)

12  Katika mwaka wa 7 wa utawala wa Yehu,+ Yehoashi+ akawa mfalme, naye akatawala kwa miaka 40 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Sibia kutoka Beer-sheba.+  Yehoashi akaendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova sikuzote ambazo kuhani Yehoyada alimfundisha.  Hata hivyo, mahali pa juu+ hapakuondolewa, na bado watu walikuwa wakitoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu.  Yehoashi akawaambia makuhani: “Chukueni pesa zote zinazoletwa katika nyumba ya Yehova kwa ajili ya matoleo matakatifu,+ pesa ambazo kila mtu amekadiriwa kutoa,+ pesa zilizotolewa kama thamani iliyokadiriwa ya mtu,* na pesa zote ambazo moyo wa kila mtu umemchochea kuleta katika nyumba ya Yehova.+  Makuhani wenyewe watachukua pesa hizo kutoka kwa wale wanaozitoa* na kuzitumia kurekebisha nyumba hiyo, sehemu yoyote iliyoharibika.”*+  Kufikia mwaka wa 23 wa utawala wa Mfalme Yehoashi, makuhani walikuwa bado hawajairekebisha nyumba hiyo.+  Kwa hiyo Mfalme Yehoashi akamwita kuhani+ Yehoyada na makuhani wengine na kuwauliza: “Kwa nini hamwirekebishi nyumba? Kwa hiyo msichukue pesa zaidi kutoka kwa watu ikiwa hazitumiwi kurekebisha nyumba.”+  Basi makuhani wakakubali kwamba hawatachukua pesa zaidi kutoka kwa watu na kwamba hawatakuwa na wajibu wa kurekebisha nyumba hiyo.  Kisha kuhani Yehoyada akachukua sanduku,+ akatoboa tundu kwenye kifuniko chake, akaliweka kando ya madhabahu upande wa kulia unapoingia ndani ya nyumba ya Yehova. Makuhani waliolinda mlangoni waliweka pesa zote zilizoletwa katika nyumba ya Yehova katika sanduku hilo.+ 10  Kila mara walipoona kwamba sanduku hilo lina pesa nyingi, mwandishi wa mfalme na kuhani mkuu walikuja na kuzikusanya* na kuzihesabu pesa hizo zilizoletwa katika nyumba ya Yehova.+ 11  Waliwapa wale waliowekwa kusimamia kazi katika nyumba ya Yehova pesa zilizokuwa zimehesabiwa. Nao wakawalipa maseremala na wajenzi waliokuwa wakifanya kazi katika nyumba ya Yehova,+ 12  na pia waashi na watu waliokata mawe. Pia walinunua mbao na mawe yaliyochongwa kwa ajili ya kurekebisha sehemu zilizoharibika za nyumba ya Yehova na kutumia pesa hizo kulipia gharama nyingine zote za kurekebisha nyumba hiyo. 13  Hata hivyo, hawakutumia pesa zozote zilizoletwa katika nyumba ya Yehova kutengeneza mabeseni ya fedha, mikasi ya kukatia tambi za taa, mabakuli, tarumbeta,+ au kitu chochote cha dhahabu au fedha kwa ajili ya nyumba ya Yehova.+ 14  Waliwapa pesa hizo wale tu waliofanya kazi hiyo, nao walizitumia kurekebisha nyumba ya Yehova. 15  Hawakudai hesabu ya matumizi ya pesa hizo kutoka kwa wanaume waliowapa pesa za kuwalipa wafanyakazi, kwa sababu wanaume hao walikuwa waaminifu.+ 16  Hata hivyo, pesa za dhabihu za hatia+ na pesa za dhabihu za dhambi hazikuletwa katika nyumba ya Yehova; zilikuwa za makuhani.+ 17  Wakati huo ndipo Hazaeli+ mfalme wa Siria alipanda kwenda kupigana na jiji la Gathi,+ naye akaliteka, kisha akaamua kulishambulia* jiji la Yerusalemu.+ 18  Ndipo Mfalme Yehoashi wa Yuda akachukua matoleo yote matakatifu ambayo mababu zake Yehoshafati, Yehoramu, na Ahazia, wafalme wa Yuda, walikuwa wameyatakasa na pia matoleo yake mwenyewe matakatifu na dhahabu yote iliyokuwa katika hazina za nyumba ya Yehova na katika nyumba ya mfalme,* akampelekea Hazaeli mfalme wa Siria.+ Kwa hiyo Hazaeli akaondoka Yerusalemu. 19  Na mambo mengine katika historia ya Yehoashi, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha nyakati za wafalme wa Yuda? 20  Hata hivyo, watumishi wake walipanga njama dhidi ya Yehoashi+ na kumuua katika nyumba ya Kilima,*+ katika njia inayoshuka kwenda Sila. 21  Yozakari mwana wa Shimeathi na Yehozabadi mwana wa Shomeri, watumishi wake, ndio waliompiga na kumuua.+ Wakamzika pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi, na Amazia mwanawe akawa mfalme baada yake.+

Maelezo ya Chini

Au “nafsi.”
Au “wale wanaowajua.”
Au “yenye nyufa.”
Au “kuziweka ndani ya mifuko.” Tnn., “kuzifunga.”
Tnn., “Hazaeli akauelekeza uso wake dhidi ya.”
Au “jumba la mfalme.”
Au “Beth-milo.”