Kitabu cha Pili cha Wafalme 14:1-29

  • Amazia, mfalme wa Yuda (1-6)

  • Apigana vita na Waedomu na Waisraeli (7-14)

  • Kifo cha Yehoashi wa Israeli (15, 16)

  • Kifo cha Amazia (17-22)

  • Yeroboamu wa Pili, mfalme wa Israeli (23-29)

14  Katika mwaka wa pili wa utawala wa Yehoashi+ mwana wa Yehoahazi mfalme wa Israeli, Amazia mwana wa Mfalme Yehoashi wa Yuda akawa mfalme.  Alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 29 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yehoadini wa Yerusalemu.+  Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, lakini si kama Daudi+ babu yake. Alifanya mambo yote kama Yehoashi baba yake.+  Hata hivyo, mahali pa juu hapakuondolewa,+ na watu bado walikuwa wakitoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu katika mahali pa juu.+  Mara tu ufalme ulipoimarika kabisa mikononi mwake, aliwaua watumishi wake waliomuua mfalme, baba yake.+  Lakini hakuwaua wana wa wauaji hao, kulingana na amri hii ya Yehova iliyoandikwa katika kitabu cha Sheria ya Musa: “Akina baba hawapaswi kuuawa kwa sababu ya wana wao, na wana hawapaswi kuuawa kwa sababu ya baba zao; lakini kila mtu anapaswa kuuawa kwa sababu ya dhambi yake mwenyewe.”+  Akawaua Waedomu+ katika Bonde la Chumvi,+ wanaume 10,000, akaliteka jiji la Sela katika vita hivyo,+ na tangu wakati huo jiji hilo likaitwa Yoktheeli.  Kisha Amazia akawatuma wajumbe kwa Yehoashi mwana wa Yehoahazi mwana wa Yehu mfalme wa Israeli, akisema: “Njoo, tupambane vitani.”*+  Mfalme Yehoashi wa Israeli akatuma ujumbe huu kwa Mfalme Amazia wa Yuda: “Gugu lenye miiba kule Lebanoni lilituma ujumbe huu kwa mwerezi huko Lebanoni, ‘Mpe mwanangu binti yako awe mke wake.’ Hata hivyo, mnyama wa mwituni wa Lebanoni akapita karibu na kulikanyaga-kanyaga gugu hilo lenye miiba. 10  Ni kweli kwamba uliwaangamiza Waedomu,+ kwa hiyo moyo wako umekuwa na kiburi. Furahia utukufu wako, lakini kaa katika nyumba yako mwenyewe.* Kwa nini utafute msiba kisha uanguke, na kuwaangusha pia watu wa Yuda?” 11  Lakini Amazia hakusikiliza.+ Basi Mfalme Yehoashi wa Israeli akapanda kwenda huko, naye akapambana vitani na Mfalme Amazia wa Yuda huko Beth-shemeshi,+ jiji la Yuda.+ 12  Watu wa Yuda wakashindwa na Waisraeli, kwa hiyo kila mmoja akakimbilia nyumbani kwake.* 13  Mfalme Yehoashi wa Israeli akamkamata Mfalme Amazia wa Yuda, mwana wa Yehoashi mwana wa Ahazia, huko Beth-shemeshi. Kisha wakaja Yerusalemu, naye akabomoa ukuta wa Yerusalemu kuanzia Lango la Efraimu+ mpaka Lango la Pembeni,+ urefu wa mikono 400.* 14  Akachukua dhahabu yote na fedha na vitu vyote vilivyokuwa katika nyumba ya Yehova na katika hazina za nyumba ya mfalme,* na pia akachukua mateka. Kisha akarudi Samaria. 15  Na mambo mengine katika historia ya Yehoashi, mambo aliyofanya na ukuu wake na jinsi alivyopigana na Mfalme Amazia wa Yuda, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 16  Kisha Yehoashi akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake huko Samaria+ pamoja na wafalme wa Israeli; na Yeroboamu mwana wake*+ akawa mfalme baada yake. 17  Amazia+ mwana wa Yehoashi mfalme wa Yuda aliendelea kuishi kwa miaka 15 baada ya kifo cha Yehoashi+ mwana wa Yehoahazi mfalme wa Israeli.+ 18  Na mambo mengine katika historia ya Amazia, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 19  Baadaye njama ikapangwa dhidi yake+ huko Yerusalemu, naye akakimbilia Lakishi, lakini wakawatuma watu wamfuatie huko Lakishi, nao wakamuua huko. 20  Kwa hiyo wakambeba juu ya farasi, naye akazikwa Yerusalemu pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ 21  Kisha watu wote wa Yuda wakamchukua Azaria,*+ aliyekuwa na umri wa miaka 16,+ wakamweka kuwa mfalme baada ya Amazia baba yake.+ 22  Alijenga upya jiji la Elathi+ na kulirudisha kwa Yuda baada ya mfalme* kuzikwa pamoja na mababu zake.+ 23  Katika mwaka wa 15 wa utawala wa Amazia mwana wa Yehoashi mfalme wa Yuda, Yeroboamu+ mwana wa Mfalme Yehoashi wa Israeli akawa mfalme huko Samaria, naye alitawala kwa miaka 41. 24  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova. Hakuacha dhambi zote za Yeroboamu mwana wa Nebati ambazo alisababisha Waisraeli kutenda.+ 25  Alirudisha mpaka wa Israeli kuanzia Lebo-hamathi*+ hadi kwenye Bahari ya Araba,*+ kulingana na neno ambalo Yehova Mungu wa Israeli alisema kupitia Yona+ mtumishi wake, mwana wa Amitai, nabii kutoka Gath-heferi.+ 26  Kwa maana Yehova alikuwa ameyaona mateso makali sana ya Waisraeli.+ Hakukuwa na yeyote aliyebaki wa kuwasaidia Waisraeli, hata watu wasio na uwezo au walio dhaifu hawakuwepo. 27  Lakini Yehova alikuwa ameahidi kwamba hatafutilia mbali jina la Israeli kutoka chini ya mbingu.+ Kwa hiyo akawaokoa kwa mkono wa Yeroboamu mwana wa Yehoashi.+ 28  Na mambo mengine katika historia ya Yeroboamu, mambo yote aliyofanya na ukuu wake, jinsi alivyopigana na jinsi alivyorudisha jiji la Damasko+ na Hamathi+ ili yamilikiwe tena na Yuda nchini Israeli, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 29  Kisha Yeroboamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake, pamoja na wafalme wa Israeli; na Zekaria+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Au “tukutane uso kwa uso.”
Au “jumba lako la mfalme.”
Tnn., “katika hema lake.”
Karibu mita 178 (futi 584). Angalia Nyongeza B14.
Au “jumba la mfalme.”
Yaani, Yeroboamu wa Pili.
Maana yake “Yehova Amesaidia.” Anaitwa Uzia katika 2Fa 15:13; 2Nya 26:1-23; Isa 6:1; na Zek 14:5.
Yaani, Amazia baba yake.
Au “njia ya kuingia Hamathi.”
Yaani, Bahari ya Chumvi.