Kitabu cha Pili cha Wafalme 15:1-38

  • Azaria, mfalme wa Yuda (1-7)

  • Wafalme wa mwisho wa Israeli: Zekaria (8-12), Shalumu (13-16), Menahemu (17-22), Pekahia (23-26), Peka (27-31)

  • Yothamu, mfalme wa Yuda (32-38)

15  Katika mwaka wa 27 wa utawala wa Mfalme Yeroboamu* wa Israeli, Azaria*+ mwana wa Mfalme Amazia+ wa Yuda akawa mfalme.+  Alikuwa na umri wa miaka 16 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 52 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yekolia wa Yerusalemu.  Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, kama alivyotenda Amazia baba yake.+  Hata hivyo, mahali pa juu hapakuondolewa,+ na watu bado walikuwa wakitoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu.+  Yehova alimletea mfalme pigo, naye aliendelea kuwa na ukoma+ mpaka siku aliyokufa; alikaa katika nyumba iliyotengwa,+ huku Yothamu mwana wa mfalme+ akiisimamia nyumba ya mfalme,* akiwahukumu watu nchini.+  Na mambo mengine katika historia ya Azaria,+ mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda?  Kisha Azaria akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake+ katika Jiji la Daudi; na Yothamu mwanawe akawa mfalme baada yake.  Katika mwaka wa 38 wa utawala wa Mfalme Azaria+ wa Yuda, Zekaria+ mwana wa Yeroboamu akawa mfalme wa Israeli huko Samaria, naye alitawala kwa miezi sita.  Alitenda maovu machoni pa Yehova, kama walivyotenda mababu zake. Hakuacha dhambi za Yeroboamu mwana wa Nebati alizosababisha Waisraeli kutenda.+ 10  Kisha Shalumu mwana wa Yabeshi akapanga njama dhidi yake na kumuua+ huko Ibleamu.+ Baada ya kumuua, Shalumu akawa mfalme. 11  Na mambo mengine katika historia ya Zekaria yameandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli. 12  Hilo lilitimiza neno hili la Yehova alilokuwa amemwambia Yehu: “Vizazi vinne vya wana wako+ vitaketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli.”+ Na ikawa hivyo. 13  Shalumu mwana wa Yabeshi akawa mfalme katika mwaka wa 39 wa utawala wa Mfalme Uzia+ wa Yuda, naye alitawala kwa mwezi mmoja kamili huko Samaria. 14  Kisha Menahemu mwana wa Gadi akapanda kutoka Tirsa+ na kuja Samaria, akamuua Shalumu+ mwana wa Yabeshi huko Samaria. Baada ya kumuua, akawa mfalme. 15  Mambo mengine katika historia ya Shalumu na njama aliyopanga, yameandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli. 16  Wakati huo ndipo Menahemu alipokuja kutoka Tirsa na kuliangamiza jiji la Tifsa na wote waliokuwa katika jiji hilo na katika eneo lake, kwa sababu hawakumfungulia malango ya jiji hilo. Aliliangamiza na kuwapasua tumbo wanawake wenye mimba wa jiji hilo. 17  Katika mwaka wa 39 wa utawala wa Mfalme Azaria wa Yuda, Menahemu mwana wa Gadi akawa mfalme wa Israeli, naye alitawala kwa miaka kumi huko Samaria. 18  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova. Na sikuzote za utawala wake hakuacha dhambi zote za Yeroboamu mwana wa Nebati alizosababisha Waisraeli kutenda.+ 19  Mfalme Pulu+ wa Ashuru aliingia nchini, na Menahemu akampa Pulu talanta 1,000 za fedha* ili amsaidie kuimarisha mamlaka yake katika ufalme huo.+ 20  Kwa hiyo Menahemu alikusanya fedha hizo kwa kuwatoza ushuru wanaume mashuhuri na matajiri wa Israeli.+ Akampa mfalme wa Ashuru shekeli 50 za fedha* kwa kila mwanamume. Kisha mfalme wa Ashuru akarudi, hakukaa nchini. 21  Na mambo mengine katika historia ya Menahemu,+ mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli? 22  Kisha Menahemu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake; na Pekahia mwana wake akawa mfalme baada yake. 23  Katika mwaka wa 50 wa utawala wa Mfalme Azaria wa Yuda, Pekahia mwana wa Menahemu akawa mfalme wa Israeli huko Samaria, naye alitawala kwa miaka miwili. 24  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova. Hakuacha dhambi za Yeroboamu mwana wa Nebati alizosababisha Waisraeli kutenda.+ 25  Kisha Peka+ mwana wa Remalia kamanda wake msaidizi akapanga njama dhidi yake na kumuua huko Samaria katika mnara wenye ngome wa nyumba ya mfalme* pamoja na Argobu na Arie. Alikuwa pamoja na wanaume 50 wa Gileadi; na baada ya kumuua, akawa mfalme. 26  Na mambo mengine katika historia ya Pekahia, mambo yote aliyofanya, yameandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli. 27  Katika mwaka wa 52 wa utawala wa Mfalme Azaria wa Yuda, Peka+ mwana wa Remalia akawa mfalme wa Israeli huko Samaria, naye alitawala kwa miaka 20. 28  Aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, naye hakuacha dhambi za Yeroboamu mwana wa Nebati alizosababisha Waisraeli kutenda.+ 29  Katika siku za utawala wa Mfalme Peka wa Israeli, Mfalme Tiglath-pileseri+ wa Ashuru alivamia na kuteka Iyoni, Abel-beth-maaka,+ Yanoa, Kedeshi, Hasori, Gileadi,+ na Galilaya,+ nchi yote ya Naftali,+ akawapeleka wakaaji wa maeneo hayo uhamishoni kule Ashuru.+ 30  Kisha Hoshea+ mwana wa Ela akapanga njama dhidi ya Peka mwana wa Remalia, akampiga na kumuua; naye akawa mfalme baada yake katika mwaka wa 20 wa utawala wa Yothamu+ mwana wa Uzia. 31  Na mambo mengine katika historia ya Peka, mambo yote aliyofanya, yameandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Israeli. 32  Katika mwaka wa pili wa utawala wa Peka mwana wa Remalia mfalme wa Israeli, Yothamu+ mwana wa Mfalme Uzia+ wa Yuda akawa mfalme. 33  Alikuwa na umri wa miaka 25 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 16 huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Yerusha binti ya Sadoki.+ 34  Aliendelea kutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova, kama alivyofanya Uzia baba yake.+ 35  Hata hivyo, mahali pa juu hapakuondolewa, na watu bado walikuwa wakitoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu.+ Yeye ndiye aliyejenga lango la juu la nyumba ya Yehova.+ 36  Na mambo mengine katika historia ya Yothamu, mambo aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 37  Siku hizo Yehova alianza kumtuma Resini mfalme wa Siria na Peka+ mwana wa Remalia kushambulia Yuda.+ 38  Kisha Yothamu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi babu yake. Na Ahazi mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Yaani, Yeroboamu wa Pili.
Maana yake “Yehova Amesaidia.” Anaitwa Uzia katika 2Fa 15:13; 2Nya 26:1-23; Isa 6:1; na Zek 14:5.
Au “jumba la mfalme.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “jumba la mfalme.”