Kitabu cha Pili cha Wafalme 16:1-20

  • Ahazi, mfalme wa Yuda (1-6)

  • Ahazi awahonga Waashuru (7-9)

  • Ahazi aiga madhabahu ya wapagani (10-18)

  • Kifo cha Ahazi (19, 20)

16  Katika mwaka wa 17 wa utawala wa Peka mwana wa Remalia, Ahazi+ mwana wa Mfalme Yothamu wa Yuda akawa mfalme.  Ahazi alikuwa na umri wa miaka 20 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa miaka 16 huko Yerusalemu. Hakutenda yaliyokuwa sawa machoni pa Yehova Mungu wake, kama alivyotenda Daudi babu yake.+  Badala yake, alitembea katika njia ya wafalme wa Israeli,+ na hata alimteketeza* motoni mwana wake mwenyewe,+ akifuata mazoea yenye kuchukiza ya mataifa+ ambayo Yehova alikuwa ameyafukuza kutoka mbele ya Waisraeli.  Aliendelea pia kutoa dhabihu na kufukiza moshi wa dhabihu mahali pa juu,+ kwenye vilima, na chini ya kila mti wenye majani mengi.+  Wakati huo ndipo Mfalme Resini wa Siria na Peka mwana wa Remalia mfalme wa Israeli walipopanda ili kuja kupigana vita dhidi ya Yerusalemu.+ Wakamzingira Ahazi lakini hawakuweza kuliteka jiji.  Wakati huo Mfalme Resini wa Siria akarudisha Elathi+ kwa Edomu, kisha akawafukuza Wayahudi* kutoka Elathi. Na Waedomu wakaingia Elathi, nao wamekuwa wakiishi humo tangu wakati huo.  Kwa hiyo Ahazi akatuma wajumbe kwa Mfalme Tiglath-pileseri+ wa Ashuru, akisema: “Mimi ni mtumishi wako na mwanao. Njoo uniokoe kutoka mikononi mwa mfalme wa Siria na kutoka mikononi mwa mfalme wa Israeli, wanaonishambulia.”  Kisha Ahazi akachukua fedha na dhahabu iliyokuwa katika nyumba ya Yehova na katika hazina za nyumba ya mfalme,* akampelekea mfalme wa Ashuru kama rushwa.+  Mfalme wa Ashuru akakubali ombi lake, naye akapanda kwenda Damasko na kuliteka jiji hilo na kuwapeleka watu wake uhamishoni huko Kiri,+ akamuua Resini.+ 10  Ndipo Mfalme Ahazi akaenda kukutana na Mfalme Tiglath-pileseri wa Ashuru kule Damasko. Alipoona madhabahu iliyokuwa Damasko, Mfalme Ahazi akamtumia kuhani Uriya ramani ya madhabahu hiyo, akamwonyesha mfano wake na jinsi ilivyojengwa.+ 11  Kuhani Uriya+ akajenga madhabahu+ kulingana na maagizo yote ambayo Mfalme Ahazi alikuwa ametuma kutoka Damasko. Kuhani Uriya akamaliza kuijenga kabla ya Mfalme Ahazi kurudi kutoka Damasko. 12  Mfalme aliporudi kutoka Damasko na kuiona madhabahu hiyo, aliikaribia na kutoa dhabihu juu yake.+ 13  Akaendelea kufukizia moshi wa dhabihu zake za kuteketezwa na matoleo yake ya nafaka juu ya madhabahu hiyo; pia aliimiminia madhabahu hiyo matoleo yake ya kinywaji na kuinyunyizia damu ya dhabihu zake za ushirika. 14  Kisha akaiondoa madhabahu ya shaba+ iliyokuwa mbele za Yehova, kutoka mahali ilipokuwa mbele ya nyumba, katikati ya madhabahu yake na nyumba ya Yehova, akaiweka upande wa kaskazini wa madhabahu yake. 15  Mfalme Ahazi akamwamuru hivi kuhani Uriya:+ “Fukiza moshi wa dhabihu ya asubuhi kwenye madhabahu hiyo kubwa,+ pia toleo la nafaka la jioni,+ dhabihu ya kuteketezwa ya mfalme, na toleo lake la nafaka, na pia dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na matoleo ya kinywaji ya watu wote. Unapaswa pia kuinyunyizia madhabahu hiyo damu yote ya dhabihu za kuteketezwa na damu yote ya dhabihu nyingine. Nitaamua nitakalofanya na madhabahu ya shaba.” 16  Kuhani Uriya akafanya mambo yote ambayo Mfalme Ahazi aliamuru.+ 17  Zaidi ya hayo, Mfalme Ahazi akazikata vipandevipande kuta za pembeni za yale magari+ na kuondoa mabeseni yaliyokuwa juu yake,+ akaiondoa ile Bahari kutoka juu ya wale ng’ombe dume wa shaba+ na kuiweka kwenye sakafu ya mawe.+ 18  Pia, alihamisha kutoka katika nyumba ya Yehova sehemu iliyofunikwa ambayo ilikuwa imejengwa katika nyumba hiyo kwa ajili ya Sabato na pia njia ya nje aliyotumia mfalme kuingia katika nyumba hiyo; alifanya hivyo kwa sababu ya mfalme wa Ashuru. 19  Na mambo mengine katika historia ya Ahazi, mambo aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda?+ 20  Kisha Ahazi akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi; na Hezekia*+ mwanawe akawa mfalme baada yake.

Maelezo ya Chini

Tnn., “alimpitisha.”
Au “watu wa Yuda.”
Au “jumba la mfalme.”
Maana yake “Yehova Huimarisha.”