Kitabu cha Pili cha Wafalme 20:1-21

  • Hezekia awa mgonjwa kisha apona (1-11)

  • Wajumbe kutoka Babiloni (12-19)

  • Kifo cha Hezekia (20, 21)

20  Siku hizo Hezekia akawa mgonjwa karibu afe.+ Nabii Isaya mwana wa Amozi akaja na kumwambia, “Yehova anasema hivi: ‘Wape maagizo watu wa nyumba yako, kwa maana utakufa; hutapona.’”+  Ndipo akaugeuza uso wake kuelekea ukutani, akaanza kusali hivi kwa Yehova:  “Nakusihi, Ee Yehova, tafadhali, kumbuka jinsi ambavyo nimetembea mbele zako kwa uaminifu na kwa moyo kamili, nami nimetenda mambo mema machoni pako.”+ Kisha Hezekia akaanza kulia sana na kububujikwa na machozi.  Isaya hakuwa amefika katika ua wa katikati, neno la Yehova lilipomjia likisema:+  “Rudi ukamwambie Hezekia, kiongozi wa watu wangu, ‘Yehova Mungu wa Daudi babu yako anasema hivi: “Nimesikia sala yako. Nimeona machozi yako.+ Tazama, ninakuponya.+ Siku ya tatu utapanda kwenda katika nyumba ya Yehova.+  Nitakuongezea miaka 15 ya kuishi,* nami nitakuokoa wewe na jiji hili kutoka mikononi mwa mfalme wa Ashuru,+ nami nitalilinda jiji hili kwa ajili yangu mwenyewe na kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu.”’”+  Ndipo Isaya akasema: “Leteni keki ya tini kavu zilizoshinikizwa.” Basi wakaileta na kuipaka kwenye jipu hilo, kisha akapona hatua kwa hatua.+  Hezekia alikuwa amemuuliza hivi Isaya: “Ni ishara gani+ itakayonionyesha kwamba Yehova ataniponya na kwamba nitapanda kwenda katika nyumba ya Yehova siku ya tatu?”  Isaya akajibu: “Hii ndiyo ishara kutoka kwa Yehova itakayokuonyesha kwamba Yehova atatimiza neno alilosema: Je, unataka kivuli kilicho kwenye ngazi* kiende mbele hatua kumi au kirudi nyuma hatua kumi?”+ 10  Hezekia akasema: “Ni rahisi kivuli kwenda mbele hatua kumi lakini si rahisi kirudi nyuma hatua kumi.” 11  Kwa hiyo nabii Isaya akamwomba Yehova, Naye akafanya kivuli kilichokuwa kwenye ngazi ya Ahazi kirudi nyuma hatua kumi na tayari kilikuwa kimeshuka ngazi.+ 12  Wakati huo mfalme wa Babiloni, Berodak-baladani mwana wa Baladani, akamtumia Hezekia barua na zawadi, kwa maana alisikia kwamba Hezekia alikuwa mgonjwa.+ 13  Hezekia akawakaribisha* na kuwaonyesha nyumba yake yote yenye hazina+—fedha, dhahabu, mafuta ya zeri na mafuta mengine yenye thamani, ghala lake la silaha, na kila kitu kilichokuwa katika hazina zake. Hakuna kitu chochote ambacho Hezekia hakuwaonyesha katika nyumba yake mwenyewe* na katika milki yake yote. 14  Kisha nabii Isaya akaenda kwa Mfalme Hezekia na kumuuliza: “Watu hawa walisema nini, nao walitoka wapi?” Hezekia akajibu: “Walitoka katika nchi ya mbali, kutoka Babiloni.”+ 15  Kisha akauliza: “Waliona nini katika nyumba yako?”* Hezekia akajibu: “Waliona kila kitu katika nyumba yangu.* Hakuna chochote ambacho sikuwaonyesha katika hazina zangu.” 16  Sasa Isaya akamwambia Hezekia: “Sikia neno la Yehova,+ 17  ‘Tazama! Siku zinakuja, na vitu vyote vilivyo katika nyumba yako* na vitu vyote ambavyo mababu zako wamehifadhi mpaka leo hii vitapelekwa Babiloni.+ Hakuna chochote kitakachobaki,” asema Yehova. 18  ‘Na baadhi ya wana wako mwenyewe utakaowazaa watachukuliwa+ na kuwa maofisa wa makao ya mfalme katika jumba la mfalme wa Babiloni.’”+ 19  Ndipo Hezekia akamwambia Isaya: “Neno la Yehova ambalo umesema ni jema.”+ Kisha akasema: “Ni jema ikiwa kutakuwa na amani na utulivu* wakati wa maisha yangu.”*+ 20  Na mambo mengine katika historia ya Hezekia, ukuu wake wote na jinsi alivyotengeneza kile kidimbwi+ na ule mfereji na kuleta maji jijini,+ je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 21  Kisha Hezekia akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake;+ na Manase mwanawe+ akawa mfalme baada yake.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “katika siku zako.”
Huenda ngazi hizo zilitumiwa kuonyesha wakati, kama saa ya kivuli inavyoonyesha wakati kwa kufuata mwendo wa jua.
Au “jumba lake la kifalme.”
Au “akawasikiliza.”
Au “jumba lako la mfalme?”
Au “jumba langu la mfalme.”
Au “jumba lako la mfalme.”
Tnn., “katika siku zangu.”
Au “ukweli.”