Kitabu cha Pili cha Wafalme 6:1-33

  • Elisha afanya shoka lielee (1-7)

  • Elisha apambana na Wasiria (8-23)

    • Macho ya mtumishi wa Elisha yafunguliwa (16, 17)

    • Wasiria wapofushwa akili (18, 19)

  • Njaa kali katika jiji lililozingirwa la Samaria (24-33)

6  Wana wa manabii+ wakamwambia Elisha: “Tazama! Mahali tunapokaa pamoja nawe ni padogo sana kwetu.  Tafadhali, acha twende Yordani. Kila mmoja wetu achukue gogo kutoka sehemu hiyo na kujenga huko mahali tunapoweza kukaa.” Akawaambia: “Nendeni.”  Mmoja wao akamwambia: “Tafadhali, unaweza kwenda pamoja nasi watumishi wako?” Basi akasema: “Nitakwenda.”  Kwa hiyo akaenda pamoja nao, wakafika Yordani na kuanza kukata miti.  Mmoja wao alipokuwa akikata mti, shoka likaanguka majini, akasema kwa sauti: “Ole wangu, bwana wangu, liliazimwa!”  Mtu wa Mungu wa kweli akauliza: “Limeanguka wapi?” Basi akamwonyesha mahali hapo. Ndipo Elisha akakata kipande cha mti na kukitupa hapo, akalifanya shoka lielee.  Akasema: “Lichukue.” Akaunyoosha mkono wake na kulichukua.  Sasa mfalme wa Siria alienda kupigana vita na Waisraeli.+ Akashauriana na watumishi wake na kuwaambia: “Nitapiga kambi pamoja nanyi mahali fulani na fulani.”  Kisha mtu wa Mungu wa kweli+ akamtumia mfalme wa Israeli ujumbe huu: “Jihadhari usipitie mahali hapa, kwa sababu hapa ndipo Wasiria wanaposhukia.” 10  Basi mfalme wa Israeli akatuma ujumbe mahali ambapo mtu wa Mungu wa kweli alikuwa amemwonya kupahusu. Mtu wa Mungu wa kweli akaendelea kumwonya, naye mfalme akaepuka mahali hapo mara kadhaa.*+ 11  Jambo hilo likamkasirisha sana mfalme* wa Siria, kwa hiyo akawaita watumishi wake na kuwauliza: “Niambieni! Ni nani miongoni mwetu aliye upande wa mfalme wa Israeli?” 12  Kisha mmoja wa watumishi wake akajibu: “Hakuna yeyote miongoni mwetu, bwana wangu mfalme! Nabii Elisha aliye Israeli ndiye humwambia mfalme wa Israeli mambo unayosema katika chumba chako mwenyewe cha kulala.”+ 13  Mfalme akasema: “Nendeni mkatafute mahali alipo, ili niwatume watu wamkamate.” Baadaye mfalme akaambiwa, “Yuko Dothani.”+ 14  Mara moja akapeleka huko farasi na magari ya vita, na pia jeshi kubwa; likaja usiku na kulizunguka jiji hilo. 15  Mtumishi* wa mtu wa Mungu wa kweli alipoamka asubuhi na mapema na kutoka nje, aliona jeshi lenye farasi na magari ya vita yakiwa yamezunguka jiji. Mara moja mtumishi huyo akamwambia: “Ole wetu, bwana wangu! Tutafanya nini?” 16  Lakini Elisha akamwambia: “Usiogope!+ Kwa maana wale walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao.”+ 17  Ndipo Elisha akaanza kusali na kusema: “Ee Yehova, tafadhali, mfungue macho yake, ili aone.”+ Mara moja Yehova akamfungua macho mtumishi huyo naye akaona, na tazama! eneo lenye milima lilikuwa limejaa farasi na magari ya vita ya moto+ kumzunguka Elisha pande zote.+ 18  Wasiria waliposhuka kuelekea mahali alipokuwa, Elisha akasali kwa Yehova na kusema: “Tafadhali, lipige kwa upofu taifa hili.”+ Basi akawapiga kwa upofu kama Elisha alivyoomba. 19  Sasa Elisha akawaambia: “Njia yenyewe si hii, na jiji lenyewe si hili. Nifuateni, nami nitawapeleka kwa mtu mnayemtafuta.” Hata hivyo, aliwapeleka Samaria.+ 20  Walipofika Samaria, Elisha akasema: “Ee Yehova, wafungue macho ili waone.” Kwa hiyo, Yehova akawafungua macho, nao wakaona kwamba walikuwa katikati ya Samaria. 21  Mfalme wa Israeli alipowaona, alimuuliza Elisha, “Je, niwaue, baba yangu, niwaue?” 22  Lakini Elisha akajibu: “Usiwaue. Je, unawaua wale ambao umewachukua mateka kwa upanga wako na kwa upinde wako? Wape mikate na maji ili wale na kunywa+ na kurudi kwa bwana wao.” 23  Basi akawaandalia karamu kubwa, nao wakala na kunywa, kisha akawaruhusu warudi kwa bwana wao. Makundi ya wavamizi ya Wasiria+ hayakurudi tena katika nchi ya Israeli. 24  Baadaye Ben-hadadi mfalme wa Siria akalikusanya pamoja jeshi lake lote* na kupanda kwenda kulizingira jiji la Samaria.+ 25  Kwa hiyo kukawa na njaa kali+ sana huko Samaria, nao wakalizingira jiji hilo mpaka kichwa cha punda+ kikawa na thamani ya vipande 80 vya fedha, na robo ya kipimo cha kabi* cha mavi ya njiwa ikawa na thamani ya vipande vitano vya fedha. 26  Mfalme wa Israeli alipokuwa akipita juu ya ukuta, mwanamke fulani akamwambia hivi kwa sauti: “Tusaidie, Ee bwana wangu mfalme!” 27  Mfalme akasema: “Yehova asipokusaidia, nitakupa msaada kutoka wapi? Kutoka kwenye uwanja wa kupuria? Au kutoka katika shinikizo la divai au mafuta?” 28  Mfalme akamuuliza: “Una shida gani?” Akamjibu: “Mwanamke huyu aliniambia, ‘Mtoe mwana wako tumle leo, na mwanangu tutamla kesho.’+ 29  Basi tukamchemsha mwanangu na kumla.+ Siku iliyofuata nikamwambia, ‘Mlete mwana wako tumle.’ Lakini akamficha mwanawe.” 30  Mara tu mfalme aliposikia maneno ya mwanamke huyo, akayararua mavazi yake.+ Alipokuwa akipita juu ya ukuta, watu wakaona kwamba alikuwa amevaa nguo za magunia ndani ya nguo zake. 31  Mfalme akasema: “Mungu na aniadhibu, tena vikali, ikiwa Elisha mwana wa Shafati hatakatwa kichwa leo!”+ 32  Elisha alikuwa ameketi nyumbani kwake pamoja na wazee. Mfalme akamtuma mtu amtangulie, lakini kabla ya mjumbe huyo kufika, Elisha akawaambia wazee hao: “Je, mmeona jinsi ambavyo mwana huyu wa muuaji+ amemtuma mtu aje kunikata kichwa? Mjumbe huyo atakapofika, fungeni mlango, nanyi muusukume ili asiingie. Je, bwana wake hayuko nyuma yake akimfuata?” 33  Alipokuwa akizungumza nao, mjumbe huyo akaja kwake, mfalme akasema: “Msiba huu unatoka kwa Yehova. Kwa nini niendelee kumngojea Yehova?”

Maelezo ya Chini

Au “zaidi ya mara moja au mbili.”
Tnn., “lilikasirisha sana moyo wa mfalme.”
Au “Mhudumu.”
Tnn., “akaikusanya pamoja kambi yake yote.”
Kabi moja ilikuwa sawa na lita 1.22. Angalia Nyongeza B14.