Kitabu cha Pili cha Wafalme 8:1-29

  • Mwanamke Mshunamu arudishiwa shamba lake (1-6)

  • Elisha, Ben-hadadi, na Hazaeli (7-15)

  • Yehoramu, mfalme wa Yuda (16-24)

  • Ahazia, mfalme wa Yuda (25-29)

8  Elisha alimwambia hivi yule mwanamke ambaye alikuwa amemfufua mwanawe:+ “Ondoka uende, wewe pamoja na familia yako, uishi kama mgeni mahali popote unapoweza kuishi, kwa maana Yehova ametangaza kwamba kutakuwa na njaa kali+ nchini kwa miaka saba.”  Basi yule mwanamke akaondoka na kufanya kama mtu wa Mungu wa kweli alivyomwambia. Akaenda pamoja na familia yake kuishi katika nchi ya Wafilisti+ kwa miaka saba.  Baada ya miaka saba, mwanamke huyo akarudi kutoka katika nchi ya Wafilisti, akaenda kumsihi mfalme ili arudishiwe nyumba yake na shamba lake.  Sasa mfalme alikuwa akizungumza na Gehazi mtumishi wa yule mtu wa Mungu wa kweli, akamwambia: “Tafadhali, nisimulie mambo yote makuu ambayo Elisha amefanya.”+  Alipokuwa akimsimulia mfalme jinsi Elisha alivyomfufua mtoto aliyekufa,+ yule mwanamke ambaye mwana wake alikuwa amefufuliwa akaja kwa mfalme akimsihi arudishiwe nyumba yake na shamba lake.+ Mara moja Gehazi akasema: “Bwana wangu mfalme, huyu ndiye yule mwanamke, na huyu ndiye mwana wake ambaye Elisha alimfufua.”  Ndipo mfalme akamuuliza mwanamke huyo, naye akamsimulia kisa chote. Kisha mfalme akamkabidhi mwanamke huyo kwa ofisa wa makao ya mfalme, akamwambia hivi ofisa huyo: “Rudisha mali yote ya mwanamke huyu na mazao yote ya shamba lake tangu siku alipotoka nchini hadi sasa.”  Elisha alienda Damasko+ wakati Ben-hadadi+ mfalme wa Siria alipokuwa mgonjwa. Ben-hadadi akaambiwa hivi: “Yule mtu wa Mungu wa kweli+ amekuja.”  Ndipo mfalme akamwambia Hazaeli:+ “Chukua zawadi, ukakutane na mtu wa Mungu wa kweli.+ Muulize Yehova kupitia kwake, ‘Je, nitapona ugonjwa huu?’”  Hazaeli akachukua zawadi na kwenda kukutana naye, alichukua vitu vizuri vya kila aina kutoka Damasko, mizigo iliyoweza kubebwa na ngamia 40. Akaja na kusimama mbele yake na kumwambia: “Mwana wako, Ben-hadadi, mfalme wa Siria amenituma kwako nikuulize, ‘Je, nitapona ugonjwa huu?’” 10  Elisha akamjibu: “Nenda ukamwambie, ‘Hakika utapona,’ lakini Yehova amenionyesha kwamba hakika atakufa.”+ 11  Elisha akamkazia macho sana Hazaeli mpaka akaona aibu. Kisha yule mtu wa Mungu wa kweli akaanza kulia. 12  Hazaeli akamuuliza: “Bwana wangu, kwa nini unalia?” Akamjibu: “Kwa sababu ninajua madhara utakayowatendea Waisraeli.+ Utateketeza ngome zao, utawaua kwa upanga wanaume wao mashujaa, utawapondaponda watoto wao, na kuwapasua tumbo wanawake wao wenye mimba.”+ 13  Hazaeli akasema: “Mimi mtumishi wako, ambaye ni mbwa tu, ninawezaje kufanya jambo kama hilo?” Lakini Elisha akasema: “Yehova amenionyesha kwamba wewe utakuwa mfalme wa Siria.”+ 14  Kisha Hazaeli akamwacha Elisha na kurudi kwa bwana wake, Ben-hadadi akamuuliza: “Elisha alikwambia nini?” Akamjibu: “Aliniambia kwamba hakika utapona.”+ 15  Lakini siku iliyofuata, Hazaeli akachukua tandiko, akalitumbukiza ndani ya maji, na kumfunika nalo usoni mpaka akafa.+ Kisha Hazaeli akawa mfalme baada yake.+ 16  Katika mwaka wa tano wa utawala wa Yehoramu+ mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, Yehoshafati alipokuwa mfalme wa Yuda, Yehoramu+ mwana wa Mfalme Yehoshafati wa Yuda akawa mfalme. 17  Alikuwa na umri wa miaka 32 alipoanza kutawala, naye alitawala huko Yerusalemu kwa miaka minane. 18  Alitembea katika njia ya wafalme wa Israeli,+ kama walivyofanya watu wa nyumba ya Ahabu,+ kwa maana alikuwa amemwoa binti ya Ahabu;+ naye aliendelea kutenda maovu machoni pa Yehova.+ 19  Lakini Yehova hakutaka kuangamiza Yuda kwa sababu ya Daudi mtumishi wake,+ kwa maana alikuwa amemwahidi atampa yeye na wanawe taa sikuzote.+ 20  Katika siku za Yehoramu, Waedomu waliasi dhidi ya Yuda,+ nao wakajichagulia mfalme wao wenyewe.+ 21  Basi Yehoramu akavuka kwenda Sairi na magari yake yote ya vita, akaondoka usiku na kuwashinda Waedomu waliokuwa wamemzingira yeye na makamanda wa magari ya vita; na wanajeshi wakakimbilia katika mahema yao. 22  Lakini tangu siku hiyo Waedomu wameendelea kuiasi nchi ya Yuda. Watu wa Libna+ waliasi pia wakati huo. 23  Na mambo mengine katika historia ya Yehoramu, mambo yote aliyofanya, je, hayajaandikwa katika kitabu cha historia ya nyakati za wafalme wa Yuda? 24  Kisha Yehoramu akafa na kuzikwa pamoja na mababu zake katika Jiji la Daudi.+ Na Ahazia+ mwana wake akawa mfalme baada yake. 25  Katika mwaka wa 12 wa utawala wa Yehoramu mwana wa Ahabu mfalme wa Israeli, Ahazia mwana wa Mfalme Yehoramu wa Yuda akawa mfalme.+ 26  Ahazia alikuwa na umri wa miaka 22 alipoanza kutawala, naye alitawala kwa mwaka mmoja huko Yerusalemu. Mama yake aliitwa Athalia,+ mjukuu wa* Mfalme Omri+ wa Israeli. 27  Alitembea katika njia ya nyumba ya Ahabu+ na kuendelea kutenda maovu machoni pa Yehova, kama nyumba ya Ahabu, kwa maana alikuwa ameoa kutoka katika nyumba ya Ahabu.+ 28  Basi Ahazia alienda pamoja na Yehoramu mwana wa Ahabu kupigana vita na Mfalme Hazaeli wa Siria kule Ramothi-gileadi,+ lakini Wasiria wakamjeruhi Yehoramu.+ 29  Kwa hiyo Mfalme Yehoramu akarudi Yezreeli+ ili apone majeraha aliyopata kutoka kwa Wasiria huko Rama alipopigana na Mfalme Hazaeli wa Siria.+ Ahazia mwana wa Yehoramu mfalme wa Yuda akashuka kwenda Yezreeli kumwona Yehoramu mwana wa Ahabu, kwa sababu alikuwa amejeruhiwa.*

Maelezo ya Chini

Tnn., “binti ya.”
Au “mgonjwa.”