Hesabu 18:1-32

  • Majukumu ya makuhani na Walawi (1-7)

  • Posho za makuhani (8-19)

    • Agano la chumvi (19)

  • Walawi watapokea na kutoa sehemu moja ya kumi (20-32)

18  Kisha Yehova akamwambia Haruni, “Wewe na wana wako na ukoo wako* mtawajibika ikiwa kosa lolote litafanywa dhidi ya mahali patakatifu,+ na wewe na wana wako mtawajibika ikiwa kosa lolote litafanywa dhidi ya ukuhani wenu.+  Pia walete ndugu zako wa kabila la Lawi, kabila la mababu zako, ili wajiunge nawe na kukuhudumia wewe+ pamoja na wanao mbele ya hema la Ushahidi.+  Wanapaswa kutimiza majukumu utakayowapa na utumishi wa hema lote.+ Hata hivyo, hawapaswi kukaribia vyombo vya mahali patakatifu na madhabahu, ili wewe pamoja nao msife.+  Watajiunga nawe na kutimiza majukumu yao kuhusiana na hema la mkutano na utumishi wote katika hema hilo, na mtu yeyote asiye na idhini* hapaswi kuwakaribia ninyi.+  Ni lazima mtimize majukumu yenu ya mahali patakatifu+ na madhabahu,+ ili ghadhabu+ yangu isije tena juu ya Waisraeli.  Mimi mwenyewe nimewachukua ndugu zenu, Walawi, kutoka miongoni mwa Waisraeli na kuwakabidhi ninyi kama zawadi.+ Wamekabidhiwa kwa Yehova ili watumikie katika hema la mkutano.+  Wewe na wanao mna wajibu wa kufanya kazi za ukuhani zinazohusu madhabahu na vitu vilivyo nyuma ya pazia,+ nanyi mtatimiza utumishi huo.+ Nimewapa utumishi wa ukuhani kama zawadi, na mtu yeyote asiye na idhini* atakayekaribia mahali patakatifu anapaswa kuuawa.”+  Yehova akaendelea kumwambia Haruni: “Mimi mwenyewe nilikuweka usimamie michango ninayoletewa.+ Nimekupa wewe na wanao sehemu ya vitu vyote vitakatifu vinavyotolewa kama mchango na Waisraeli ili viwe posho yenu ya kudumu.+  Hivi ndivyo vitakavyokuwa vitu vyenu kutoka katika matoleo yote matakatifu kabisa yanayochomwa kwa moto: matoleo yao yote, kutia ndani matoleo yao ya nafaka+ na dhabihu zao za dhambi+ na dhabihu zao za hatia+ wanazoniletea. Ni vitu vitakatifu kabisa kwako na wanao. 10  Mtavila vitu hivyo mahali patakatifu zaidi.+ Kila mwanamume anaweza kuvila. Vitakuwa vitu vitakatifu kwenu.+ 11  Vitu hivi pia vitakuwa vyenu: zawadi ambazo Waisraeli wanatoa kuwa mchango+ pamoja na matoleo yao yote ya kutikiswa.+ Nimekupa wewe na wanao na mabinti wako vitu hivyo ili viwe posho yenu ya kudumu.+ Kila mtu aliye safi katika nyumba yako anaweza kula.+ 12  “Mafuta yote bora na divai yote mpya na nafaka, mazao yao ya kwanza,+ ambayo wanampa Yehova, ninakupa wewe.+ 13  Mazao yote ya kwanza yaliyokomaa ya ardhi yao, ambayo watamletea Yehova, yatakuwa yako.+ Kila mtu aliye safi katika nyumba yako anaweza kula. 14  “Kila kitu kilichotolewa kwa ajili yangu* katika Israeli kinapaswa kuwa chako.+ 15  “Kila mzaliwa wa kwanza wa viumbe wote walio hai,+ ambaye watanitolea mimi Yehova, awe ni mwanadamu au mnyama, anapaswa kuwa wako. Hata hivyo, ni lazima uwakomboe wazaliwa wa kwanza wa wanadamu,+ na unapaswa pia kuwakomboa wazaliwa wa kwanza wa wanyama wasio safi.+ 16  Unapaswa kumkomboa mzaliwa wa kwanza kwa bei ya ukombozi akiwa na umri wa kuanzia mwezi mmoja na zaidi, kwa thamani iliyokadiriwa ya shekeli tano za fedha,*+ kulingana na shekeli ya kawaida ya mahali patakatifu.* Ni gera 20.* 17  Lakini hupaswi kumkomboa+ ng’ombe dume ambaye ni mzaliwa wa kwanza au mwanakondoo dume ambaye ni mzaliwa wa kwanza au mbuzi ambaye ni mzaliwa wa kwanza. Hao ni watakatifu. Unapaswa kunyunyiza damu yao kwenye madhabahu,+ na mafuta yao unapaswa kuyateketeza ili yafuke moshi yakiwa dhabihu inayochomwa kwa moto yenye harufu inayompendeza* Yehova.+ 18  Nyama yao itakuwa yako. Itakuwa yako sawa na kidari cha toleo la kutikiswa na mguu wa kulia.+ 19  Michango yote mitakatifu ambayo Waisraeli watamchangia Yehova,+ nimekupa wewe na wanao na mabinti wako, ili iwe posho yenu ya kudumu.+ Ni agano la chumvi linalodumu* mbele za Yehova kwa ajili yako na wazao wako.” 20  Yehova akaendelea kumwambia Haruni: “Hutakuwa na urithi katika nchi yao, wala hutakuwa na sehemu ya* ardhi miongoni mwao.+ Mimi ni fungu lako na urithi wako miongoni mwa Waisraeli.+ 21  “Ona kwamba nimewapa wana wa Lawi kila sehemu ya kumi+ katika Israeli iwe urithi wao kwa sababu ya utumishi wao, utumishi wa hema la mkutano. 22  Waisraeli wasikaribie tena hema la mkutano ili wasitende dhambi na kufa. 23  Ni Walawi tu watakaotumikia katika hema la mkutano, na ndio watakaowajibika kwa ajili ya makosa yao.+ Ni sheria ya kudumu katika vizazi vyenu vyote kwamba hawapaswi kuchukua urithi miongoni mwa Waisraeli.+ 24  Kwa maana nimewapa Walawi sehemu ya kumi ambayo Waisraeli wananitolea mchango, mimi Yehova, ili iwe urithi wao. Ndiyo sababu nimewaambia, ‘Hawapaswi kuchukua urithi miongoni mwa Waisraeli.’”+ 25  Kisha Yehova akamwambia Musa, 26  “Unapaswa kuwaambia hivi Walawi: ‘Mtapokea kutoka kwa Waisraeli sehemu ya kumi ambayo nimewapa ninyi kutoka kwao ili iwe urithi wenu,+ nanyi mnapaswa kumtolea Yehova mchango wa sehemu ya kumi kutoka katika sehemu hiyo ya kumi.+ 27  Sehemu hiyo itahesabiwa kuwa mchango wenu, itaonwa kama nafaka kutoka katika uwanja wa kupuria+ au divai yote inayotoka katika shinikizo la divai au mafuta yote yanayotoka katika shinikizo la mafuta. 28  Kwa njia hiyo mtamtolea Yehova mchango kutoka katika sehemu zote za kumi mnazopokea kutoka kwa Waisraeli, na kutoka kwa sehemu hizo mnapaswa kumtolea Yehova mchango na kumpa kuhani Haruni. 29  Mtamtolea Yehova michango yote kutoka katika zawadi bora zaidi mnazopokea,+ ambazo ni takatifu.’ 30  “Nawe unapaswa kuwaambia, ‘Mnapotoa vitu bora zaidi kutoka katika zawadi hizo kuwa mchango, mchango huo wa Walawi utaonwa kama nafaka kutoka katika uwanja wa kupuria na kama divai inayotoka katika shinikizo la divai au mafuta yanayotoka katika shinikizo la mafuta. 31  Ninyi na familia zenu mnaweza kula vitu hivyo mahali popote kwa sababu ni malipo kwa ajili ya utumishi wenu katika hema la mkutano.+ 32  Hamtakuwa na hatia ya dhambi maadamu mnanitolea vitu bora kutoka katika zawadi hizo, nanyi hampaswi kuchafua vitu vitakatifu vya Waisraeli, msije mkafa.’”+

Maelezo ya Chini

Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Tnn., “mgeni yeyote,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.
Tnn., “mgeni yeyote,” yaani, mtu ambaye si wa familia ya Haruni.
Yaani, kila kitu kilichofanywa kuwa kitakatifu kwa Mungu kwa kuwa hakiwezi kukombolewa au kuchukuliwa tena.
Au “shekeli takatifu.”
Gera moja ilikuwa na uzito wa gramu 0.57. Angalia Nyongeza B14.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Au “inayomtuliza.”
Yaani, agano linalodumu na lisilobadilika.
Au “fungu la.”