Hesabu 35:1-34

  • Majiji ya Walawi (1-8)

  • Majiji ya makimbilio (9-34)

35  Yehova akaendelea kuzungumza na Musa katika jangwa tambarare la Moabu karibu na Yordani+ huko Yeriko, akamwambia:  “Waagize Waisraeli wawape Walawi majiji ya kuishi kutoka katika urithi watakaomiliki,+ nao wanapaswa kuwapa Walawi malisho yanayozunguka majiji hayo.+  Wataishi katika majiji hayo, na malisho hayo yatakuwa ya mifugo yao, na ya mali zao, na wanyama wao wengine wote.  Malisho ya majiji mtakayowapa Walawi yatakuwa na upana wa mikono 1,000* kila upande kutoka kwenye ukuta wa jiji.  Mtapima nje ya jiji mikono 2,000 upande wa mashariki, mikono 2,000 upande wa kusini, mikono 2,000 upande wa magharibi, na mikono 2,000 upande wa kaskazini; jiji litakuwa katikati. Hayo ndiyo yatakayokuwa malisho ya majiji yao.  “Majiji mtakayowapa Walawi yatakuwa majiji 6 ya makimbilio+ ili mtu anayemuua mwenzake akimbilie humo,+ pia mtawapa majiji mengine 42.  Mtawapa Walawi jumla ya majiji 48 pamoja na malisho yake.+  Majiji mtakayowapa yatatoka katika urithi wa Waisraeli.+ Mtachukua majiji mengi kutoka kwa makabila makubwa na majiji machache kutoka kwa makabila madogo.+ Kila kabila litawapa Walawi baadhi ya majiji yake kulingana na urithi ambao litapokea.”  Yehova akaendelea kumwambia Musa, 10  “Waambie hivi Waisraeli: ‘Mnavuka Mto Yordani kuingia katika nchi ya Kanaani.+ 11  Mnapaswa kuchagua majiji yatakayowafaa ninyi ili yawe majiji ya makimbilio ili mtu anayemuua mwenzake bila kukusudia akimbilie humo.+ 12  Majiji hayo yatakuwa mahali penu pa kukimbilia kutoka kwa mtu anayelipiza kisasi cha damu,+ ili muuaji asiuawe kabla ya kesi yake kusikilizwa mbele ya kusanyiko.+ 13  Majiji sita ya makimbilio mtakayotoa yatatumiwa kwa kusudi hilo. 14  Mtatoa majiji matatu upande huu wa Yordani+ na majiji matatu katika nchi ya Kanaani+ ili yawe majiji ya makimbilio. 15  Majiji hayo sita yatakuwa majiji ya makimbilio kwa ajili ya Waisraeli, kwa ajili ya wageni,+ na kwa ajili ya wahamiaji wanaoishi miongoni mwenu, ili mtu yeyote anayemuua mwenzake bila kukusudia akimbilie humo.+ 16  “‘Lakini ikiwa mtu amempiga mwenzake kwa kifaa cha chuma na kumuua, yeye ni muuaji. Lazima muuaji huyo auawe.+ 17  Ikiwa alimpiga kwa jiwe ambalo linaweza kuua, na mtu huyo akafa, aliyempiga ni muuaji. Lazima muuaji huyo auawe. 18  Ikiwa alimpiga kwa kifaa cha mbao kinachoweza kuua, na mtu huyo akafa, aliyempiga ni muuaji. Lazima muuaji huyo auawe. 19  “‘Mwenye kulipiza kisasi cha damu ndiye atakayemuua muuaji. Atakapokutana naye, atamuua yeye mwenyewe. 20  Ikiwa mtu anayemchukia mwenzake anamsukuma au kumtupia kitu fulani kwa nia mbaya* na kumuua,+ 21  au kwa sababu ya chuki anampiga kwa mkono na kumuua, ni lazima mtu huyo aliyempiga auawe. Yeye ni muuaji. Mtu anayelipiza kisasi cha damu atamuua muuaji huyo atakapokutana naye. 22  “‘Lakini ikiwa alimsukuma au kumtupia kitu chochote na kumuua bila kukusudia au bila chuki na bila nia mbaya,*+ 23  au ikiwa alimwangushia jiwe bila kumwona na mtu huyo akafa, lakini hakuwa adui yake au hakukusudia kumdhuru, 24  basi watu wanapaswa kuhukumu kati ya muuaji na mtu anayelipiza kisasi cha damu, kwa kufuata sheria hizo.+ 25  Kisha watu watamwokoa muuaji kutoka mikononi mwa mtu anayelipiza kisasi cha damu na kumrudisha katika jiji lake la makimbilio alimokuwa amekimbilia, naye atakaa humo mpaka kuhani mkuu aliyetiwa mafuta matakatifu+ atakapokufa. 26  “‘Lakini muuaji akitoka nje ya mpaka wa jiji la makimbilio alimokimbilia, 27  kisha mtu anayelipiza kisasi cha damu ampate nje ya mpaka wa jiji la makimbilio na kumuua, mtu huyo anayelipiza kisasi cha damu hatakuwa na hatia ya damu. 28  Kwa maana ni lazima muuaji akae katika jiji lake la makimbilio mpaka kuhani mkuu atakapokufa. Lakini baada ya kuhani mkuu kufa, muuaji anaweza kurudi katika ardhi anayomiliki.+ 29  Mtatumia sheria hizo kuhukumu katika vizazi vyenu vyote mahali popote mnapoishi. 30  “‘Yeyote anayemuua mtu* anapaswa kuuawa kama muuaji+ ikiwa kuna ushahidi kutoka kwa mashahidi;+ lakini hakuna mtu atakayeuawa* kwa ushahidi wa mtu mmoja tu. 31  Hampaswi kuchukua fidia yoyote kwa ajili ya uhai wa* muuaji anayestahili kufa, kwa maana ni lazima auawe.+ 32  Nanyi hampaswi kuchukua fidia kwa ajili ya mtu aliyekimbilia katika jiji lake la makimbilio na hivyo kumruhusu arudi kuishi katika ardhi yake kabla ya kuhani mkuu kufa. 33  “‘Msiichafue nchi mnayoishi ndani yake, kwa sababu damu inachafua nchi,+ na hakuna msamaha kwa ajili ya damu iliyomwagwa nchini isipokuwa kwa kumwaga damu ya yule aliyeimwaga.+ 34  Msiitie unajisi nchi mnayoishi ndani yake, ambamo ninakaa; kwa maana mimi, Yehova, ninakaa miongoni mwa Waisraeli.’”+

Maelezo ya Chini

Mkono mmoja ulilingana na sentimita 44.5 (inchi 17.5). Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “huku akimvizia.”
Tnn., “bila kumvizia.”
Au “nafsi itakayouawa.”
Au “anayeua nafsi.”
Au “nafsi ya.”