Hesabu 5:1-31

  • Kuwatenga watu wasio safi (1-4)

  • Kuungama na kulipia kosa (5-10)

  • Maji yatumiwa kuthibitisha ikiwa mtu alifanya uzinzi (11-31)

5  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Waamuru Waisraeli wamtoe nje ya kambi kila mtu mwenye ukoma+ na kila mtu anayetokwa na umajimaji+ na kila mtu aliyejichafua kwa kumgusa mtu aliyekufa.*+  Mnapaswa kumtoa nje awe ni mwanamume au mwanamke. Mnapaswa kuwatoa nje ya kambi watu hao ili wasichafue+ kambi za wale ninaokaa* kati yao.”+  Basi Waisraeli wakafanya hivyo, wakawatoa nje ya kambi. Waisraeli wakafanya kama Yehova alivyomwambia Musa.  Yehova akaendelea kumwambia Musa:  “Waambie Waisraeli, ‘Mwanamume au mwanamke akitenda dhambi yoyote ya kibinadamu na kukosa kuwa mwaminifu kwa Yehova, mtu huyo ana* hatia.+  Ni lazima aungame+ dhambi aliyotenda na alipe malipo kamili kwa ajili ya hatia yake na kuongeza sehemu ya tano ya malipo hayo;+ atampa yule aliyemkosea.  Lakini ikiwa mtu aliyekosewa hana mtu wa karibu wa ukoo atakayepokea malipo hayo, yanapaswa kurudishwa kwa Yehova nayo yatakuwa ya kuhani, isipokuwa kondoo dume wa dhabihu ya kufunika dhambi atakayetolewa kufunika dhambi yake.+  “‘Kila mchango mtakatifu+ kutoka kwa Waisraeli unaoletwa kwa kuhani utakuwa wake.+ 10  Vitu vitakatifu vya kila mtu vitaendelea kuwa vyake mwenyewe. Kitu chochote ambacho mtu anampa kuhani kitakuwa cha kuhani.’” 11  Yehova akaendelea kumwambia Musa: 12  “Waambie Waisraeli, ‘Hivi ndivyo mtakavyofanya mke wa mtu yeyote akipotoka na kukosa uaminifu kwa mume wake 13  na mwanamume mwingine afanye naye ngono,+ lakini mume wake hajui jambo hilo na halijagunduliwa, kwa hiyo mwanamke huyo amejichafua lakini hakuna shahidi wa kumshtaki, naye hajakamatwa: 14  Iwe mume wake ana wivu na anatilia shaka uaminifu wa mke wake aliyejichafua, au iwe ana wivu na anatilia shaka uaminifu wa mke wake ingawa hajajichafua, 15  ni lazima mwanamume huyo ampeleke mke wake kwa kuhani pamoja na toleo kwa ajili yake, yaani, sehemu ya kumi ya kipimo cha efa* ya unga wa shayiri. Hapaswi kumimina mafuta juu ya toleo hilo wala kutia ubani juu yake, kwa sababu ni toleo la nafaka la wivu, toleo la nafaka ambalo ni kumbukumbu la hatia. 16  “‘Kuhani atamleta mwanamke huyo na kumsimamisha mbele za Yehova.+ 17  Kisha kuhani atatia maji matakatifu katika chombo cha udongo na kuchukua kiasi kidogo cha mavumbi kutoka kwenye sakafu ya hema la ibada na kuyatia katika maji hayo. 18  Baada ya kuhani kumsimamisha mwanamke huyo mbele za Yehova, atafungua nywele za mwanamke huyo na kuweka katika mikono ya mwanamke huyo lile toleo la nafaka la kumbukumbu, yaani, toleo la nafaka la wivu,+ huku kuhani akiwa ameshika mkononi yale maji machungu yanayoleta laana.+ 19  “‘Kisha kuhani atamwapisha mwanamke huyo akisema: “Ikiwa hujafanya ngono na mwanamume mwingine ukiwa chini ya mamlaka ya mume wako+ wala hujapotoka au kujichafua, basi maji haya machungu yanayoleta laana yasikudhuru. 20  Lakini ikiwa umepotoka ukiwa chini ya mamlaka ya mume wako na kujichafua kwa kufanya ngono na mwanamume mwingine+ ambaye si mume wako—” 21  Basi kuhani atamwapisha mwanamke huyo kiapo chenye laana, na kumwambia: “Yehova na akufanye uwe mfano wa laana na kiapo miongoni mwa watu wako, Yehova na akufanye uwe tasa* na tumbo lako livimbe. 22  Maji haya yanayoleta laana yataingia katika matumbo yako na kufanya tumbo lako livimbe nawe utakuwa tasa.”* Kisha mwanamke huyo atasema: “Amina! Amina!”* 23  “‘Halafu kuhani ataandika laana hizo katika kitabu na kuziosha kwenye maji machungu ili zifutike. 24  Kisha atamnywesha mwanamke huyo maji hayo machungu yanayoleta laana, na maji hayo yanayoleta laana yataingia mwilini mwake na kusababisha maumivu makali. 25  Kuhani atachukua toleo la nafaka la wivu+ kutoka mikononi mwa mwanamke huyo na kulitikisa kwenda mbele na nyuma mbele za Yehova, kisha atalileta karibu na madhabahu. 26  Halafu kuhani atachukua mkono mmoja wa toleo la nafaka ili kuwa dhabihu ya kumbukumbu na kuliteketeza juu ya madhabahu ili lifuke moshi,+ kisha atamnywesha mwanamke huyo maji hayo. 27  Baada ya mwanamke huyo kunyweshwa maji hayo, ikiwa amejichafua na kukosa uaminifu kwa mume wake, maji yanayoleta laana yataingia mwilini mwake na kusababisha maumivu makali, na tumbo lake litavimba naye atakuwa tasa,* na mwanamke huyo atakuwa mfano wa laana miongoni mwa watu wake. 28  Hata hivyo, ikiwa mwanamke huyo hajajichafua, naye ni safi, basi hatapata madhara, ataweza kupata mimba na kuzaa watoto. 29  “‘Hiyo ndiyo sheria kuhusu wivu+ inayopaswa kufuatwa mwanamke akipotoka na kujichafua akiwa chini ya mamlaka ya mume wake, 30  au ikiwa mwanamume ana wivu na anatilia shaka uaminifu wa mke wake; mwanamume huyo atamsimamisha mke wake mbele za Yehova, naye kuhani atamtendea mwanamke huyo kulingana na sheria hii yote. 31  Mwanamume huyo hatakuwa na hatia, lakini mke wake ataadhibiwa kwa sababu ya kosa lake.’”

Maelezo ya Chini

Au “kugusa nafsi iliyokufa.” Angalia Kamusi.
Au “ninaopiga hema.”
Au “nafsi hiyo ina.”
Sehemu ya kumi ya efa ilikuwa sawa na lita 2.2 au kilogramu 1.3 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Tnn., “afanye paja lako lidhoofike.” Inaonekana msemo huu unarejelea viungo vya uzazi.
Tnn., “na paja lako litadhoofika.” Inaonekana msemo huu unarejelea viungo vya uzazi.
Au “Na iwe hivyo! Na iwe hivyo!”
Tnn., “na paja lake litadhoofika.” Inaonekana msemo huu unarejelea viungo vya uzazi.