Hesabu 8:1-26

  • Haruni awasha taa saba (1-4)

  • Walawi watakaswa na kuanza utumishi wao (5-22)

  • Mipaka ya umri kwa ajili ya utumishi wa Walawi (23-26)

8  Yehova akamwambia Musa:  “Mwambie hivi Haruni: ‘Unapowasha taa, taa hizo saba zinapaswa kuangaza upande wa mbele wa kinara cha taa.’”+  Basi Haruni akafanya hivi: Akawasha taa hizo ili ziangaze upande wa mbele wa kinara cha taa,+ kama Yehova alivyomwamuru Musa.  Hivi ndivyo kinara cha taa kilivyotengenezwa: Kilitengenezwa kwa nyundo+ kwa kutumia dhahabu; kuanzia shina lake mpaka maua yake, kilitengenezwa kwa nyundo. Kinara hicho cha taa kilitengenezwa kulingana na maono+ ambayo Yehova alikuwa amemwonyesha Musa.  Yehova akazungumza tena na Musa, akamwambia:  “Wachukue Walawi kutoka miongoni mwa Waisraeli, uwatakase.+  Hivi ndivyo unavyopaswa kuwatakasa: Wanyunyizie maji ya kutakasa dhambi, na ni lazima wajinyoe mwili mzima kwa wembe, wafue mavazi yao, na kujitakasa.+  Kisha watachukua ng’ombe dume mchanga+ na toleo lake la nafaka+ la unga laini uliochanganywa na mafuta, nawe utachukua ng’ombe dume mwingine mchanga kwa ajili ya dhabihu ya dhambi.+  Utawapeleka Walawi mbele ya hema la mkutano na kuwakusanya Waisraeli wote.+ 10  Utakapowapeleka Walawi mbele za Yehova, Waisraeli wataweka mikono yao juu ya Walawi.+ 11  Ni lazima Haruni awatoe* Walawi mbele za Yehova kama toleo la kutikiswa+ kutoka kwa Waisraeli, nao watatekeleza utumishi wa Yehova.+ 12  “Kisha Walawi wataweka mikono yao juu ya vichwa vya wale ng’ombe dume.+ Kisha watamtolea Yehova ng’ombe dume mmoja kwa ajili ya dhabihu ya dhambi na mwingine kwa ajili ya dhabihu ya kuteketezwa ili kufunika dhambi+ zao. 13  Nawe utawasimamisha Walawi mbele ya Haruni na wanawe na kuwatoa* kwa Yehova kama toleo la kutikiswa. 14  Ni lazima uwatenge Walawi kutoka miongoni mwa Waisraeli, nao Walawi watakuwa wangu.+ 15  Kisha Walawi wataingia ndani ya hema la mkutano ili kutumikia. Hivyo ndivyo unavyopaswa kuwatakasa na kuwatoa* kama toleo la kutikiswa. 16  Kwa maana wao ni watu waliokabidhiwa, niliokabidhiwa kutoka miongoni mwa Waisraeli. Nitawachukua hao kwa ajili yangu badala ya wazaliwa wote wa kwanza* wa Waisraeli.+ 17  Kwa maana kila mzaliwa wa kwanza miongoni mwa Waisraeli ni wangu, awe mwanadamu au mnyama.+ Niliwatakasa ili wawe wangu siku niliyomuua kila mzaliwa wa kwanza nchini Misri.+ 18  Nitawachukua Walawi badala ya wazaliwa wote wa kwanza wa Waisraeli. 19  Nitampa Haruni na wanawe Walawi hao wakiwa watu waliokabidhiwa kutoka miongoni mwa Waisraeli, ili watumikie katika hema la mkutano+ kwa niaba ya Waisraeli na kutoa dhabihu ya kufunika dhambi za Waisraeli, na ili Waisraeli wasipatwe na pigo lolote+ kwa sababu wao hukaribia mahali patakatifu.” 20  Musa na Haruni na Waisraeli wote wakawatendea Walawi mambo hayo. Waisraeli waliwatendea Walawi kulingana na mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Musa awatendee. 21  Basi Walawi wakajitakasa na kufua mavazi yao,+ kisha Haruni akawatoa* kama toleo la kutikiswa mbele za Yehova.+ Halafu Haruni akatoa dhabihu ya kufunika dhambi zao ili kuwatakasa.+ 22  Baada ya hayo, Walawi waliingia ili kutumikia katika hema la mkutano chini ya usimamizi wa Haruni na wanawe. Waliwatendea kama Yehova alivyomwamuru Musa kuhusu Walawi. 23  Sasa Yehova akamwambia Musa: 24  “Jambo hili linawahusu Walawi: Mwanamume mwenye umri wa miaka 25 na zaidi atajiunga na wale wanaotumikia katika hema la mkutano. 25  Lakini baada ya umri wa miaka 50 atastaafu, hataendelea na utumishi huo. 26  Anaweza kuwasaidia ndugu zake wanaotumikia katika hema la mkutano, lakini hapaswi kupewa kazi humo. Hivyo ndivyo utakavyofanya kuhusu Walawi na majukumu yao.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “awatikise,” yaani, awafanye waende mbele na nyuma.
Tnn., “kuwatikisa,” yaani, kuwafanya waende mbele na nyuma.
Tnn., “kuwatikisa,” yaani, kuwafanya waende mbele na nyuma.
Au “kila kifungua mimba.”
Tnn., “akawatikisa,” yaani, akawafanya waende mbele na nyuma.