Malaki 1:1-14

  • Yehova anawapenda watu wake (1-5)

  • Makuhani watoa dhabihu zisizofaa (6-14)

    • Jina la Mungu litakuwa kuu miongoni mwa mataifa (11)

1  Tangazo: Neno la Yehova kwa Waisraeli kupitia Malaki:*  “Nimewaonyesha ninyi watu upendo,”+ asema Yehova. Lakini mnauliza: “Umetuonyeshaje upendo?” “Je, Esau hakuwa ndugu ya Yakobo?”+ asema Yehova. “Lakini nilimpenda Yakobo,  nami nikamchukia Esau;+ nikafanya milima yake kuwa ukiwa+ na urithi wake nikawaachia mbwamwitu wa nyikani.”+  “Ingawa Waedomu wanasema, ‘Tumevunjwavunjwa, lakini tutarudi na kujenga tena magofu,’ Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Watajenga, lakini nitabomoa, nao wataitwa “eneo la uovu” na “watu ambao Yehova amewahukumu milele.”+  Macho yenu wenyewe yataona hilo, nanyi mtasema: “Yehova na atukuzwe katika eneo la Israeli.”’”  “‘Mwana humheshimu baba yake,+ na mtumishi bwana wake. Basi ikiwa mimi ni baba,+ iko wapi heshima ninayostahili?+ Na ikiwa mimi ni bwana,* iko wapi hofu* ninayostahili?’ Mimi Yehova wa majeshi ninawauliza ninyi makuhani mnaolidharau jina langu.+ “‘Lakini mnauliza: “Tumelidharau jina lako kwa njia gani?”’  “‘Kwa kutoa chakula kilichochafuliwa* juu ya madhabahu yangu.’ “‘Nanyi mnauliza: “Tumekuchafua jinsi gani?”’ “‘Kwa kusema: “Meza ya Yehova+ ni kitu cha kudharauliwa.”  Na mnapomtoa mnyama kipofu kuwa dhabihu, mnasema: “Si vibaya.” Na mnapomtoa mnyama kilema au mgonjwa mnasema: “Si vibaya.”’”+ “Tafadhali, jaribuni kumtolea gavana wenu vitu hivyo. Je, atapendezwa nanyi au kuwapokea ninyi kwa kibali?” asema Yehova wa majeshi.  “Na sasa, tafadhali, msihini* Mungu ili atuonyeshe kibali. Mkitoa dhabihu za aina hiyo kwa mikono yenu, je, atampokea yeyote kati yenu kwa kibali?” auliza Yehova wa majeshi. 10  “Na ni nani miongoni mwenu aliye tayari kufunga milango?*+ Kwa maana hata hamtawasha moto kwenye madhabahu yangu bila malipo.+ Sipendezwi nanyi,” asema Yehova wa majeshi, “nami sipendezwi na zawadi yoyote kutoka mikononi mwenu.”+ 11  “Kwa maana tangu jua linapochomoza mpaka linapotua,* jina langu litakuwa kuu miongoni mwa mataifa.+ Kila mahali dhabihu zitafukizwa moshi, na matoleo yatatolewa kwa jina langu, yakiwa zawadi safi; kwa sababu jina langu litakuwa kuu miongoni mwa mataifa,”+ asema Yehova wa majeshi. 12  “Lakini ninyi mnalitia unajisi*+ kwa kusema, ‘Meza ya Yehova imechafuliwa, matunda yake, chakula chake, ni kitu cha kudharauliwa.’+ 13  Pia mnasema, ‘Tazama! Inachosha kwelikweli!’ na kwa pua zenu mnaishushia pumzi kwa dharau,” asema Yehova wa majeshi. “Nanyi mnaleta wanyama walioibwa, vilema, na wagonjwa. Naam, mnaleta vitu hivyo kuwa zawadi! Je, niikubali kutoka mikononi mwenu?”+ auliza Yehova. 14  “Amelaaniwa mtu mjanja aliye na mnyama asiye na kasoro katika kundi lake, lakini anaapa na kumtolea Yehova dhabihu ya mnyama mwenye kasoro.* Kwa maana mimi ni Mfalme mkuu,”+ asema Yehova wa majeshi, “na jina langu litakuwa lenye kuogopesha miongoni mwa mataifa.”+

Maelezo ya Chini

Maana yake “Mjumbe Wangu.”
Au “bwana mkubwa.”
Au “heshima.”
Tnn., “mkate uliotiwa unajisi.”
Tnn., “utulizeni uso wa.”
Inaonekana ni wajibu wa kufunga milango ya hekalu.
Au “kutoka mashariki mpaka magharibi.”
Au labda, “mnanitia unajisi.”
Au “dosari.”