Mwanzo 24:1-67

  • Isaka atafutiwa mke (1-58)

  • Rebeka aenda kukutana na Isaka (59-67)

24  Sasa Abrahamu alikuwa amezeeka, umri wake ulikuwa umesonga, na Yehova alikuwa amembariki Abrahamu katika kila jambo.+  Abrahamu akamwambia mtumishi wake, aliyekuwa na umri mkubwa zaidi nyumbani mwake, ambaye alisimamia mali zake zote:+ “Tafadhali, weka mkono wako chini ya paja langu,  nami nitakuapisha kwa jina la Yehova, Mungu wa mbingu na Mungu wa dunia, kwamba hutamchukulia mwanangu mke kutoka kwa mabinti wa Wakanaani, ninaoishi miongoni mwao.+  Badala yake unapaswa kwenda katika nchi yangu na kwa watu wangu wa ukoo,+ ukamchukulie mke mwanangu Isaka.”  Lakini mtumishi huyo akamuuliza: “Namna gani mwanamke huyo akikataa kuja pamoja nami katika nchi hii? Je, nimrudishe mwana wako katika nchi uliyotoka?”+  Ndipo Abrahamu akamwambia: “Hakikisha kwamba humpeleki mwanangu huko.+  Yehova Mungu wa mbinguni, aliyenitoa katika nyumba ya baba yangu na kutoka katika nchi ya watu wangu wa ukoo+ na ambaye alizungumza nami na kuniapia:+ ‘Nitaupa uzao wako*+ nchi hii,’+ atamtuma malaika wake mbele yako,+ nawe hakika utamchukulia mwanangu mke kutoka huko.+  Lakini ikiwa mwanamke huyo atakataa kuja pamoja nawe, utakuwa huru kutokana na kiapo hiki. Lakini usimpeleke mwanangu huko.”  Ndipo mtumishi huyo akaweka mkono wake chini ya paja la Abrahamu bwana wake na kumwapia kuhusu jambo hilo.+ 10  Basi mtumishi huyo akachukua ngamia kumi kati ya ngamia wa bwana wake na kuondoka, akiwa na vitu vizuri vya kila aina kutoka kwa bwana wake. Kisha akaenda zake Mesopotamia, katika jiji la Nahori. 11  Akawapumzisha ngamia* kwenye kisima cha maji kilichokuwa nje ya jiji. Ilikuwa inaelekea jioni, wakati ambapo wanawake huenda kisimani kuteka maji. 12  Kisha akasema: “Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu, tafadhali, nifanikishe leo, na umtendee kwa upendo wako mshikamanifu bwana wangu Abrahamu. 13  Nimesimama hapa kwenye chemchemi ya maji, na mabinti wa watu wa jiji wanakuja kuteka maji. 14  Na itukie kwamba msichana nitakayemwambia, ‘Tafadhali, ushushe mtungi wako ili ninywe maji,’ naye aseme, ‘Kunywa, nami nitawanywesha ngamia wako pia,’ na awe ndiye uliyemchagulia mtumishi wako, Isaka; na kwa jambo hilo acha nijue kwamba umemtendea bwana wangu kwa upendo wako mshikamanifu.” 15  Hata kabla hajamaliza kuongea, Rebeka, binti ya Bethueli+ mwana wa Milka+ mke wa Nahori,+ ndugu ya Abrahamu, akaja akiwa amebeba mtungi wa maji begani. 16  Basi msichana huyo alikuwa mrembo sana, bikira; hakuna mwanamume yeyote aliyekuwa amefanya ngono naye. Akateremka chini kwenye chemchemi, akaujaza maji mtungi wake, kisha akapanda kurudi. 17  Mara moja yule mtumishi akakimbia ili akutane naye, akamwambia: “Tafadhali, nipe maji kidogo ninywe kutoka kwenye mtungi wako.” 18  Msichana huyo akasema: “Kunywa, bwana wangu.” Ndipo akaushusha haraka mtungi wake na kuushikilia ili anywe maji. 19  Alipomaliza kumpa maji ya kunywa, akasema: “Nitateka pia maji kwa ajili ya ngamia wako mpaka watosheke.” 20  Kwa hiyo akamimina haraka maji ya mtungi wake ndani ya chombo cha kuwanyweshea wanyama, naye akakimbia tena na tena kisimani kuteka maji, akaendelea kuteka maji kwa ajili ya ngamia wake wote. 21  Wakati huo wote mwanamume huyo alikuwa kimya akimtazama kwa mshangao, akijiuliza kama Yehova alikuwa amefanikisha safari yake au la. 22  Ngamia walipotosheka kunywa maji, mwanamume huyo akatoa na kumpa pete ya puani ya dhahabu yenye uzito wa nusu shekeli* na bangili mbili za dhahabu zenye uzito wa shekeli kumi,* 23  kisha akamuuliza: “Tafadhali niambie, wewe ni binti ya nani? Kuna nafasi katika nyumba ya baba yako ambamo tunaweza kulala usiku huu?” 24  Akamjibu: “Mimi ni binti ya Bethueli+ mwana wa Milka, ambaye alimzalia Nahori.”+ 25  Akaendelea kusema: “Tuna nyasi na chakula kingi cha mifugo na pia mahali mnapoweza kulala usiku.” 26  Ndipo mwanamume huyo akainama chini na kusujudu mbele za Yehova 27  na kusema: “Yehova na asifiwe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, kwa maana hajaacha kumtendea bwana wangu kwa upendo wake mshikamanifu na kwa uaminifu wake. Yehova ameniongoza mpaka kwenye nyumba ya ndugu za bwana wangu.” 28  Kisha msichana huyo akakimbia kuwaambia watu wa nyumbani mwa mama yake kuhusu mambo hayo. 29  Sasa Rebeka alikuwa na ndugu aliyeitwa Labani.+ Basi Labani akakimbia kwenda kukutana na huyo mwanamume aliyekuwa nje kwenye chemchemi. 30  Labani alipoona ile pete na zile bangili mikononi mwa dada yake na kuyasikia maneno ya Rebeka dada yake, ambaye alikuwa akisema, “Hivi ndivyo mwanamume huyo alivyoniambia,” Labani alikwenda kukutana na mwanamume huyo, ambaye bado alikuwa amesimama karibu na ngamia wake kando ya chemchemi. 31  Mara moja akamwambia: “Njoo, wewe uliyebarikiwa na Yehova. Kwa nini bado umesimama hapa nje? Nimekutayarishia nyumba na mahali kwa ajili ya ngamia wako.” 32  Ndipo mwanamume huyo akaingia ndani ya nyumba, naye* akawafungua ngamia na kuwapa nyasi na chakula cha mifugo na kuleta maji ya kuosha miguu yake na miguu ya wanaume waliokuwa pamoja naye. 33  Hata hivyo, chakula kilipowekwa mbele yake, alisema: “Sitakula mpaka niwaambie kilichonileta.” Kwa hiyo Labani akamwambia: “Tuambie!” 34  Kisha akasema: “Mimi ni mtumishi wa Abrahamu.+ 35  Na Yehova amembariki sana bwana wangu, na amemtajirisha sana kwa kumpa kondoo na ng’ombe, fedha na dhahabu, watumishi wa kiume na wa kike, na ngamia na punda.+ 36  Isitoshe, Sara, mke wa bwana wangu, akiwa amezeeka,+ alimzalia bwana wangu mwana, na bwana wangu atampa kila kitu alicho nacho.+ 37  Kwa hiyo bwana wangu aliniapisha hivi: ‘Usimchukulie mwanangu mke kutoka kwa mabinti wa Wakanaani ambao ninaishi katika nchi yao.+ 38  Hapana, bali utaenda katika nyumba ya baba yangu na katika ukoo wangu,+ nawe utamchukulia mwanangu mke kutoka huko.’+ 39  Lakini nikamuuliza bwana wangu: ‘Namna gani mwanamke huyo akikataa kuja pamoja nami?’+ 40  Akaniambia: ‘Yehova, ambaye nimetembea mbele zake,+ atamtuma malaika wake+ pamoja nawe, naye hakika ataifanikisha safari yako, nawe utamchukulia mwanangu mke kutoka katika ukoo wangu na kutoka katika nyumba ya baba yangu.+ 41  Utakuwa huru kutokana na kiapo chako ikiwa utaenda katika ukoo wangu nao wakatae kukupa msichana huyo. Hilo litakuweka huru kutokana na kiapo chako.’+ 42  “Nilipofika kwenye chemchemi leo, nilisema: ‘Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ikiwa utaifanikisha safari yangu, 43  nimesimama kwenye kisima. Itatukia kwamba msichana+ akija kuteka maji nitasema, “Tafadhali, niruhusu ninywe maji kidogo kutoka katika mtungi wako,” 44  naye ataniambia, “Kunywa maji, na pia nitateka maji kwa ajili ya ngamia wako.” Mwanamke huyo na awe ndiye ambaye Yehova amemchagulia mwana wa bwana wangu.’+ 45  “Kabla sijamaliza kusema maneno hayo moyoni mwangu, Rebeka akatokea akiwa amebeba mtungi begani, akateremka mpaka kwenye chemchemi na kuanza kuteka maji. Ndipo nikamwambia: ‘Tafadhali, nipe maji ninywe.’+ 46  Kwa hiyo akaushusha haraka mtungi wake kutoka begani mwake, akasema: ‘Kunywa maji,+ nami nitawanywesha pia ngamia wako.’ Basi nikanywa maji, naye akawanywesha pia ngamia wangu. 47  Baada ya hayo nikamuuliza, ‘Wewe ni binti ya nani?’ akajibu, ‘Binti ya Bethueli mwana wa Nahori, ambaye Milka alimzalia.’ Kwa hiyo nikamvisha pete puani na bangili mikononi mwake.+ 48  Nami nikainama chini na kusujudu mbele za Yehova na kumsifu Yehova Mungu wa bwana wangu Abrahamu,+ aliyekuwa ameniongoza kwenye njia inayofaa ili nimchukue binti ya ndugu ya bwana wangu kwa ajili ya mwana wake. 49  Na sasa niambieni ikiwa mnataka kumtendea bwana wangu kwa upendo mshikamanifu na uaminifu; lakini ikiwa sivyo, niambieni, ili nijue jambo la kufanya.”*+ 50  Ndipo Labani na Bethueli wakajibu: “Jambo hili limetoka kwa Yehova. Hatuwezi kukuambia ndio au la.* 51  Rebeka ndiye huyu hapa. Mchukue uende, na awe mke wa mwana wa bwana wako, kama Yehova alivyosema.” 52  Mtumishi wa Abrahamu aliposikia maneno yao, mara moja akainama chini kifudifudi mbele za Yehova. 53  Na mtumishi huyo akaanza kutoa vito vya fedha na dhahabu na mavazi na kumpa Rebeka, naye akampa ndugu yake na mama yake vitu vyenye thamani. 54  Kisha mtumishi huyo na wanaume waliokuwa pamoja naye wakala na kunywa, nao wakalala huko usiku huo. Alipoamka asubuhi alisema: “Niruhusuni niende kwa bwana wangu.” 55  Lakini ndugu na mama ya Rebeka wakamwambia: “Acha msichana huyu akae nasi kwa angalau siku kumi. Kisha anaweza kwenda.” 56  Lakini akawaambia: “Msinicheleweshe, kwa maana Yehova ameifanikisha safari yangu. Niruhusuni niondoke, ili niende kwa bwana wangu.” 57  Kwa hiyo wakasema: “Acha tumwite msichana huyo tumuulize.” 58  Wakamwita Rebeka na kumuuliza: “Je, utakwenda na mtu huyu?” Akajibu: “Niko tayari kwenda.” 59  Basi wakamruhusu Rebeka+ dada yao na mlezi wake*+ waende pamoja na mtumishi wa Abrahamu na watu wake. 60  Nao wakambariki Rebeka na kumwambia: “Dada yetu, na uwe maelfu mara elfu kumi,* na uzao wako umiliki* lango la* wale wanaowachukia.”+ 61  Kisha Rebeka na vijakazi wake wakainuka, wakapanda ngamia, na kumfuata mtumishi huyo. Kwa hiyo mtumishi huyo akamchukua Rebeka na kuondoka. 62  Sasa Isaka alikuwa ametoka upande wa Beer-lahai-roi,+ kwa maana alikuwa akiishi katika nchi ya Negebu.+ 63  Na Isaka alikuwa nje akitembea shambani akitafakari+ jioni giza linapokaribia kuingia. Alipoinua macho yake, tazama, aliona ngamia wakija! 64  Rebeka alipoinua macho, alimwona Isaka, akashuka haraka kutoka kwenye ngamia. 65  Kisha akamuuliza mtumishi wa Abrahamu: “Mwanamume yule anayetembea shambani akija kutupokea ni nani?” Mtumishi huyo akajibu: “Ni bwana wangu.” Kwa hiyo Rebeka akachukua shela yake na kujifunika. 66  Na mtumishi huyo akamwambia Isaka mambo yote aliyokuwa amefanya. 67  Kisha Isaka akampeleka Rebeka ndani ya hema la Sara mama yake.+ Hivyo akamchukua Rebeka, akawa mke wake; Isaka akampenda,+ akafarijika baada ya kifo cha mama yake.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “mbegu yako.”
Tnn., “Akawapigisha magoti ngamia.”
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Shekeli moja ilikuwa na uzito wa gramu 11.4. Angalia Nyongeza B14.
Huenda ni Labani.
Tnn., “ili niende mkono wa kulia au wa kushoto.”
Au “Hatuwezi kukuambia jambo jema au baya.”
Yaani, mlezi wake ambaye sasa alikuwa kijakazi wake.
Au “na uwe mama ya maelfu ya makumi ya maelfu.”
Tnn., “mbegu yako imiliki.”
Au “majiji ya.”