Mwanzo 43:1-34

  • Ndugu za Yosefu warudi Misri mara ya pili wakiwa na Benjamini (1-14)

  • Yosefu akutana tena na ndugu zake (15-23)

  • Yosefu ala na kunywa na ndugu zake (24-34)

43  Sasa njaa ilikuwa kali sana nchini.+  Basi walipomaliza kula nafaka waliyoleta kutoka Misri,+ baba yao akawaambia: “Rudini huko mkatununulie chakula kidogo.”  Yuda akamwambia: “Yule mtu alituonya waziwazi akisema, ‘Msiuone tena uso wangu msipokuja na ndugu yenu.’+  Ukituruhusu twende na ndugu yetu, tutashuka huko na kukununulia chakula.  Lakini usipoturuhusu twende naye, hatutashuka kwenda huko, kwa sababu mtu huyo alituambia, ‘Msiuone uso wangu tena msipokuja na ndugu yenu.’”+  Israeli+ akawauliza: “Kwa nini mmeniletea shida hii kwa kumwambia mtu huyo kwamba mna ndugu mwingine?”  Wakamjibu: “Mtu huyo alituuliza hivi moja kwa moja kutuhusu sisi na watu wetu wa ukoo: ‘Je, baba yenu angali hai? Je, mna ndugu mwingine?’ nasi tukamwambia ukweli.+ Tungejuaje atasema, ‘Mleteni ndugu yenu huku chini’?”+  Kisha Yuda akamsihi Israeli baba yake: “Niruhusu niende na mvulana huyu,+ acha twende zetu ili tuishi tusije tukafa+—wewe na sisi na watoto wetu.+  Nitakuwa dhamana kwa ajili ya ulinzi wake.*+ Nitawajibika kwako. Nisipomrudisha na kukukabidhi, nitakuwa nimekutendea dhambi ya kudumu. 10  Lakini ikiwa hatungalikawia, kufikia sasa tungalikuwa tumefika huko na kurudi mara mbili.” 11  Kwa hiyo Israeli baba yao akawaambia: “Ikiwa ni lazima iwe hivyo, basi fanyeni hivi: Bebeni katika mifuko yenu vitu bora zaidi vya nchi yetu mkampelekee mtu huyo zawadi:+ zeri+ kidogo, asali kidogo, labdanamu, magome yenye utomvu,+ kungu, na lozi. 12  Bebeni kiasi maradufu cha pesa; na pia rudisheni pesa zilizowekwa kwenye midomo ya mifuko yenu.+ Huenda walikosea. 13  Mchukueni ndugu yenu mwende, rudini kwa mtu huyo. 14  Mungu Mweza-Yote na amchochee mtu huyo awahurumie, ili awaruhusu mrudi na yule ndugu yenu mwingine na Benjamini. Lakini ikiwa ni lazima nifiwe, basi nitafiwa!”+ 15  Kwa hiyo wanaume hao wakachukua zawadi hiyo, kiasi maradufu cha pesa, na pia wakamchukua Benjamini. Wakaondoka na kushuka Misri, wakafika na kusimama tena mbele ya Yosefu.+ 16  Yosefu alipomwona Benjamini akiwa pamoja nao, mara moja akamwambia msimamizi wa nyumba yake: “Wapeleke watu hawa nyumbani, uchinje wanyama na kutayarisha chakula, kwa sababu watakula nami chakula cha mchana.” 17  Mara moja mtu huyo akafanya kama Yosefu alivyomwambia,+ akawapeleka nyumbani kwa Yosefu. 18  Lakini waliogopa walipopelekwa nyumbani kwa Yosefu, wakaanza kusema: “Tumeletwa hapa kwa sababu ya zile pesa zilizorudishwa katika mifuko yetu wakati uliopita. Sasa watatushambulia na kutufanya watumwa na kuchukua punda wetu!”+ 19  Kwa hiyo wakamfikia msimamizi wa nyumba ya Yosefu, wakaongea naye kwenye mlango wa nyumba hiyo. 20  Wakamwambia: “Samahani, bwana wetu! Tulikuja huku chini mara ya kwanza kununua chakula.+ 21  Lakini tulipofika mahali tulipokuwa tukilala na kuanza kufungua mifuko yetu, tazama, kila mmoja wetu alikuta pesa zake kwenye mdomo wa mfuko wake, kiasi kilekile tulicholeta.+ Basi tungependa kuzirudisha sisi wenyewe. 22  Nasi tumeleta pesa zaidi za kununua chakula. Hatujui ni nani aliyeweka pesa zetu katika mifuko yetu.”+ 23  Msimamizi huyo akawaambia: “Ni sawa. Msiogope. Mungu wenu na Mungu wa baba yenu aliweka hazina katika mifuko yenu. Tayari nimepokea pesa zenu.” Baada ya hayo akamtoa Simeoni na kumleta kwao.+ 24  Kisha msimamizi huyo akawapeleka ndani ya nyumba ya Yosefu, akawapa maji ya kunawa miguu na kuwapa punda wao chakula. 25  Nao wakatayarisha zawadi+ ya kumpa Yosefu atakapokuja mchana, kwa sababu walisikia kwamba wangekula chakula humo.+ 26  Yosefu alipoingia nyumbani, wakampelekea zawadi yao na kuinama kifudifudi mbele yake.+ 27  Kisha akawauliza kuhusu hali yao na kusema: “Baba yenu aliyezeeka mliyeniambia habari zake anaendeleaje? Je, angali hai?”+ 28  Wakamjibu: “Baba yetu ambaye ni mtumishi wako ni mzima. Angali hai.” Kisha wakainama chini na kuanguka kifudifudi.+ 29  Alipoinua macho yake na kumwona Benjamini ndugu yake, mwana wa mama yake,+ akasema: “Je, huyu ndiye ndugu yenu mdogo mliyeniambia habari zake?”+ Kisha akamwambia: “Mungu na akupe kibali chake, mwanangu.” 30  Halafu Yosefu akatoka nje haraka kwa sababu alilemewa na hisia alipomwona ndugu yake, akatafuta mahali pa kulilia. Kwa hiyo akaingia katika chumba cha faragha na kulia huku akitokwa na machozi.+ 31  Kisha akanawa uso na kutoka chumbani, sasa akiwa amedhibiti hisia zake, akasema: “Leteni chakula.” 32  Basi wakampa Yosefu chakula chake na ndugu zake chakula chao, nao Wamisri waliokuwa pamoja naye wakala peke yao kwa sababu Wamisri hawangeweza kula pamoja na Waebrania, kwa sababu hilo ni jambo linalochukiza kwa Wamisri.+ 33  Ndugu zake waliketi mbele yake, mzaliwa wa kwanza kulingana na haki yake ya mzaliwa wa kwanza+ na yule mdogo kulingana na umri wake, nao walikuwa wakitazamana kwa mshangao. 34  Yosefu alikuwa akiagiza chakula kichukuliwe kutoka kwenye meza yake na kupelekwa kwenye meza yao, lakini aliongeza chakula cha Benjamini mara tano zaidi ya chakula ambacho wengine wote walipewa.+ Basi wakaendelea kula na kunywa pamoja naye mpaka waliposhiba.

Maelezo ya Chini

Au “rehani kwa ajili yake.”