Waamuzi 6:1-40

  • Wamidiani wawakandamiza Waisraeli (1-10)

  • Malaika amhakikishia Mwamuzi Gideoni atapata msaada (11-24)

  • Gideoni abomoa madhabahu ya Baali (25-32)

  • Roho ya Mungu yamtia nguvu Gideoni (33-35)

  • Jaribio la manyoya (36-40)

6  Lakini Waisraeli wakatenda tena mambo maovu machoni pa Yehova,+ basi Yehova akawatia mikononi mwa Wamidiani kwa miaka saba.+  Na Wamidiani wakawakandamiza Waisraeli.+ Kwa sababu ya Wamidiani, Waisraeli wakachimba mashimo ya kujificha* katika milima, mapango, na mahali pagumu kufikiwa.+  Waisraeli walipopanda mbegu, Wamidiani, Waamaleki,+ na watu wa Mashariki+ waliwashambulia.  Nao walikuwa wakipiga kambi ili kuwashambulia na kuharibu mazao yote nchini hadi Gaza, na hawakuwaachia Waisraeli chakula chochote, wala kondoo, ng’ombe dume, au punda.+  Walikuja na mifugo yao na mahema mengi sana kama nzige,+ na wao pamoja na ngamia wao hawangeweza kuhesabiwa,+ walikuja ili kuiharibu nchi.  Basi Wamidiani wakawafanya Waisraeli kuwa maskini sana; na Waisraeli wakamlilia Yehova awasaidie.+  Waisraeli walipomlilia Yehova awasaidie kwa sababu ya Wamidiani,+  Yehova aliwaletea Waisraeli nabii aliyewaambia hivi: “Yehova Mungu wa Israeli anasema, ‘Niliwatoa Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa.+  Nikawaokoa kutoka mikononi mwa Wamisri na mikononi mwa wote waliowakandamiza, nikawafukuza mbele yenu na kuwapa ninyi nchi yao.+ 10  Kisha nikawaambia, “Mimi ni Yehova Mungu wenu.+ Msiogope miungu ya Waamori ambao mnakaa katika nchi yao.”+ Lakini hamkunitii.’”*+ 11  Baadaye malaika wa Yehova akaja+ na kuketi chini ya mti mkubwa wa Yoashi Mwabiezeri uliokuwa Ofra.+ Gideoni mwanawe+ alikuwa akipura ngano katika shinikizo la divai ili Wamidiani wasiione. 12  Ndipo malaika wa Yehova akamtokea, akamwambia hivi: “Yehova yuko pamoja nawe,+ ewe shujaa hodari.” 13  Gideoni akamwambia, “Niwie radhi, bwana wangu, lakini ikiwa Yehova yuko pamoja nasi, kwa nini mambo haya yote yametupata?+ Yako wapi matendo yake ya ajabu ambayo baba zetu walitusimulia,+ wakisema, ‘Yehova ndiye aliyetutoa Misri?’+ Sasa Yehova ametuacha,+ naye ametutia mikononi mwa Wamidiani.” 14  Ndipo Yehova akamgeukia na kumwambia, “Nenda kwa nguvu ulizo nazo, nawe utawaokoa Waisraeli kutoka mikononi mwa Wamidiani.+ Je, si mimi ninayekutuma?” 15  Gideoni akamjibu, “Niwie radhi, Yehova. Ninawezaje kuwaokoa Waisraeli? Ukoo wangu ndio mdogo* zaidi katika kabila la Manase, nami ni mdogo kabisa katika nyumba ya baba yangu.” 16  Lakini Yehova akamwambia, “Kwa sababu nitakuwa pamoja nawe,+ utawashinda Wamidiani kana kwamba ni mtu mmoja.” 17  Ndipo Gideoni akamwambia, “Ikiwa nimepata kibali machoni pako, nionyeshe ishara kwamba ni wewe unayeongea nami. 18  Tafadhali usiondoke hapa mpaka nitakaporudi na kukuletea zawadi yangu na kuiweka mbele yako.”+ Basi akasema, “Sitaondoka mpaka utakaporudi.” 19  Kwa hiyo Gideoni akaingia nyumbani na kutayarisha mwanambuzi na kuoka mikate isiyo na chachu kwa kutumia efa* ya unga.+ Akaweka nyama katika kikapu na kutia mchuzi katika chungu cha kupikia; kisha akampelekea chini ya ule mti mkubwa. 20  Sasa yule malaika wa Mungu wa kweli akamwambia, “Chukua nyama na mikate hiyo isiyo na chachu, uviweke juu ya lile jiwe kubwa, na umimine mchuzi juu yake.” Akafanya hivyo. 21  Ndipo malaika wa Yehova akanyoosha fimbo iliyokuwa mkononi mwake na kwa ncha yake akaigusa ile nyama na ile mikate isiyo na chachu, na moto ukatoka kwenye lile jiwe na kuiteketeza ile nyama na ile mikate isiyo na chachu.+ Kisha malaika wa Yehova akatoweka. 22  Ndipo Gideoni akatambua kwamba huyo alikuwa malaika wa Yehova.+ Mara moja Gideoni akasema, “Ole wangu, Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova, kwa sababu nimemwona malaika wa Yehova uso kwa uso!”+ 23  Lakini Yehova akamwambia, “Uwe na amani. Usiogope;+ hutakufa.” 24  Basi Gideoni akamjengea Yehova madhabahu hapo, ambayo mpaka leo hii inaitwa Yehova-shalomu.*+ Bado iko huko Ofra ya Waabiezeri. 25  Usiku huo Yehova akamwambia, “Mchukue ng’ombe dume mchanga wa baba yako, ng’ombe dume mchanga wa pili mwenye miaka saba, nawe ubomoe madhabahu ya Baali ambayo ni ya baba yako, na ukate mti mtakatifu* ulio kando yake.+ 26  Baada ya kumjengea Yehova Mungu wako madhabahu juu ya ngome hii kwa mawe yaliyopangwa vizuri, mchukue yule ng’ombe dume mchanga wa pili unitolee dhabihu ya kuteketezwa juu ya kuni za ule mti mtakatifu* ambao ulikata.” 27  Basi Gideoni akawachukua wanaume kumi kati ya watumishi wake na kufanya kama Yehova alivyomwambia. Lakini kwa kuwa aliwaogopa sana watu wa nyumba ya baba yake na wakaaji wa jiji, hakufanya mambo hayo mchana, aliyafanya usiku. 28  Wakaaji wa jiji walipoamka asubuhi na mapema, waliona kwamba madhabahu ya Baali ilikuwa imebomolewa na ule mti mtakatifu* uliokuwa kando yake ulikuwa umekatwa, na yule ng’ombe dume mchanga wa pili alikuwa ameteketezwa juu ya madhabahu iliyokuwa imejengwa. 29  Wakaulizana, “Ni nani aliyefanya jambo hili?” Baada ya kufanya uchunguzi, wakasema, “Gideoni mwana wa Yoashi ndiye aliyefanya jambo hili.” 30  Kwa hiyo wakaaji wa jiji wakamwambia hivi Yoashi: “Mtoe nje mwana wako, anapaswa kufa kwa sababu amebomoa madhabahu ya Baali na kukata mti mtakatifu* uliokuwa kando yake.” 31  Ndipo Yoashi+ akawaambia watu wote waliomkabili, “Je, ni lazima mumtetee Baali? Je, ni lazima mumwokoe? Yeyote anayemtetea anapaswa kuuawa asubuhi hii.+ Ikiwa yeye ni mungu, acheni ajitetee mwenyewe,+ kwa sababu mtu fulani amebomoa madhabahu yake.” 32  Siku hiyo akamwita Gideoni jina Yerubaali,* akisema, “Acheni Baali ajitetee mwenyewe, kwa sababu mtu fulani amebomoa madhabahu yake.” 33  Wamidiani wote+ na Waamaleki+ na watu wa Mashariki wakaungana;+ wakavuka* na kupiga kambi katika Bonde la* Yezreeli. 34  Kisha roho ya Yehova ikamjia* Gideoni+ naye akapiga pembe,*+ na Waabiezeri+ wakakusanyika na kumfuata. 35  Akatuma wajumbe katika nchi yote ya kabila la Manase, wakakusanyika pia na kumfuata. Akatuma pia wajumbe kotekote katika nchi ya Asheri, Zabuloni, na Naftali, nao wakaja kukutana naye. 36  Kisha Gideoni akamwambia hivi Mungu wa kweli: “Ikiwa utawaokoa Waisraeli kwa mkono wangu, kama ulivyoahidi,+ 37  ninaweka manyoya ya kondoo kwenye uwanja wa kupuria. Ikiwa kutakuwa na umande juu ya manyoya hayo peke yake lakini ardhi yote inayozunguka manyoya hayo iwe kavu, ndipo nitakapojua kwamba utawaokoa Waisraeli kwa mkono wangu, kama ulivyoahidi.” 38  Na ikawa hivyo. Alipoamka mapema siku iliyofuata na kukamua manyoya hayo, maji ya umande yalijaa kwenye bakuli kubwa. 39  Hata hivyo, Gideoni akamwambia hivi Mungu wa kweli: “Tafadhali usinikasirikie, nakuomba jambo moja zaidi. Tafadhali niruhusu nifanye jaribio lingine moja tu kwa manyoya haya. Tafadhali, acha manyoya peke yake yawe makavu, na ardhi yote iwe na umande.” 40  Basi Mungu akafanya hivyo usiku huo; manyoya peke yake yakawa makavu, na ardhi yote ikawa na umande.

Maelezo ya Chini

Au labda, “maghala yaliyo chini ya ardhi.”
Tnn., “hamkuisikiliza sauti yangu.”
Tnn., “Elfu yangu ndiyo ndogo.”
Efa ya unga ilikuwa karibu kilogramu 13. Angalia Nyongeza B14.
Maana yake “Yehova Ni Amani.”
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Angalia Kamusi.
Maana yake “Acheni Baali Ajitetee Kisheria (Apambane).”
Au “wakavuka mto.”
Au “Nchi Tambarare ya Chini ya.”
Au “ikamfunika.”
Au “tarumbeta.”