Yeremia 34:1-22

  • Ujumbe wa hukumu kwa Sedekia (1-7)

  • Agano la kuwaachilia huru watumwa lavunjwa (8-22)

34  Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova, Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni na jeshi lake lote na falme zote za dunia chini ya mamlaka yake na mataifa yote yalipokuwa yakishambulia Yerusalemu na majiji yake yote:+  “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Nenda uzungumze na Mfalme Sedekia+ wa Yuda nawe umwambie hivi: “Yehova anasema, ‘Ninalitia jiji hili mikononi mwa mfalme wa Babiloni, naye ataliteketeza kwa moto.+  Nawe hutaponyoka kutoka mikononi mwake, kwa maana kwa hakika utakamatwa na kutiwa mikononi mwake.+ Nawe utamwona Mfalme wa Babiloni jicho kwa jicho, naye atazungumza nawe uso kwa uso, nawe utapelekwa Babiloni.’+  Hata hivyo, sikia neno la Yehova, ewe Mfalme Sedekia wa Yuda, ‘Yehova anasema hivi kukuhusu wewe: “Hutakufa kwa upanga.  Utakufa kwa amani,+ nao watakufanyia sherehe ya kufukiza manukato kama walivyowafanyia baba zako, wafalme wa zamani waliokutangulia, nao watakuombolezea wakisema, ‘Ole, ewe bwana!’ kwa maana ‘nimelisema neno hilo,’ asema Yehova.”’”’”  Kisha nabii Yeremia akamwambia maneno haya yote Mfalme Sedekia wa Yuda huko Yerusalemu,  majeshi ya mfalme wa Babiloni yalipokuwa yakishambulia Yerusalemu na majiji yote ya Yuda yaliyobaki,+ yakishambulia Lakishi+ na Azeka;+ kwa maana hayo ndiyo majiji pekee ya Yuda yenye ngome yaliyobaki.  Neno lililomjia Yeremia kutoka kwa Yehova baada ya Mfalme Sedekia kufanya agano pamoja na watu wote waliokuwa Yerusalemu ili kuwatangazia uhuru,+  kwamba kila mtu awaachilie huru watumwa wake Waebrania, wa kiume na wa kike, ili mtu yeyote asimfanye Myahudi mwenzake kuwa mtumwa. 10  Basi wakuu wote na watu wote wakatii. Walikuwa wamefanya agano kwamba kila mtu awaachilie huru watumwa wake wa kiume na wa kike na asiwafanye tena kuwa watumwa. Wakatii na kuwaruhusu waende zao. 11  Hata hivyo, baadaye waliwarudisha watumwa wao wa kiume na wa kike ambao walikuwa wamewaachilia huru, nao wakawalazimisha tena kuwa watumwa. 12  Basi neno la Yehova likamjia Yeremia kutoka kwa Yehova likisema: 13  “Yehova Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Nilifanya agano pamoja na mababu zenu+ siku niliyowatoa nchini Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa,+ nikisema: 14  “Mwishoni mwa miaka saba, kila mmoja wenu anapaswa kumwachilia huru ndugu yake Mwebrania aliyeuzwa kwake na ambaye amemtumikia miaka sita; lazima umwachilie huru.”+ Lakini mababu zenu hawakunisikiliza wala kunitegea masikio yao. 15  Na hivi karibuni* ninyi wenyewe mligeuka na kufanya yaliyo sawa machoni pangu kwa kuwatangazia uhuru wenzenu, nanyi mkafanya agano mbele zangu katika nyumba inayoitwa kwa jina langu. 16  Lakini mligeuka tena na kulichafua jina langu+ kwa kuwarudisha watumwa wenu wa kiume na wa kike ambao mlikuwa mmewaachilia huru kama walivyotaka, nanyi mkawalazimisha tena kuwa watumwa.’ 17  “Kwa hiyo Yehova anasema hivi: ‘Hamjanitii kwa sababu kila mtu hajamtangazia uhuru ndugu yake na mwenzake.+ Basi sasa ninawatangazia uhuru,’ asema Yehova, ‘kwa upanga, ugonjwa hatari, na njaa kali,+ nami nitawafanya muwe kitu cha kutisha kwa falme zote za dunia.+ 18  Na hivi ndivyo itakavyokuwa kwa watu waliolivunja agano langu kwa kutofuata maneno ya agano walilofanya mbele zangu walipomkata ndama vipande viwili na kupita kati ya vile vipande viwili,+ 19  yaani, wakuu wa Yuda, wakuu wa Yerusalemu, maofisa wa makao ya mfalme, makuhani, na watu wote wa nchi waliopita kati ya vile vipande viwili vya ndama: 20  Nitawatia mikononi mwa maadui wao na mikononi mwa wale wanaotaka kuwaua,* na maiti zao zitakuwa chakula cha ndege wa angani na cha wanyama wa dunia.+ 21  Nami nitamtia Mfalme Sedekia wa Yuda na wakuu wake mikononi mwa maadui wao na mikononi mwa wale wanaotaka kuwaua* na mikononi mwa majeshi ya mfalme wa Babiloni,+ ambao wanaondoka na kuacha kuwashambulia.’+ 22  “‘Nitatoa agizo,’ asema Yehova, ‘nami nitawarudisha katika jiji hili, nao watalishambulia na kuliteka na kuliteketeza kwa moto;+ nami nitayafanya majiji ya Yuda yawe ukiwa, bila mkaaji.’”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.
Tnn., “leo.”
Au “wanaotafuta nafsi zao.”
Au “wanaotafuta nafsi zao.”