Yeremia 44:1-30

  • Msiba watabiriwa dhidi ya Wayahudi walio Misri (1-14)

  • Watu wakataa onyo la Mungu (15-30)

    • “Malkia wa Mbinguni” aabudiwa (17-19)

44  Neno lililomjia Yeremia kwa ajili ya Wayahudi wote waliokuwa wakiishi katika nchi ya Misri,+ wale waliokuwa wakiishi Migdoli,+ Tahpanhesi,+ Nofu,*+ na katika nchi ya Pathrosi,+ likisema:  “Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Mmeona msiba wote nilioleta dhidi ya Yerusalemu+ na dhidi ya majiji yote ya Yuda, na leo yamebaki magofu, bila mkaaji.+  Ni kwa sababu ya mambo maovu waliyofanya ili kunikasirisha kwa kwenda kutoa dhabihu+ na kuiabudu miungu mingine ambayo hawakuijua, wala ninyi wala mababu zenu.+  Niliendelea kuwatuma kwenu watumishi wangu wote manabii, niliwatuma tena na tena* nikisema: “Tafadhali msifanye jambo hili lenye kuchukiza ninalochukia.”+  Lakini hawakusikiliza wala kutega sikio lao na kuacha uovu wao na kuacha kuitolea dhabihu miungu mingine.+  Basi ghadhabu yangu na hasira yangu ilimwagwa na kuwaka katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu, na majiji hayo yakawa magofu na ukiwa, kama ilivyo leo.’+  “Na sasa Yehova, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Kwa nini mnajiletea msiba mkubwa, ili kila mwanamume na mwanamke, mtoto mdogo na mtoto anayenyonya, waangamie kutoka Yuda, asibaki yeyote?  Kwa nini mnikasirishe kwa kazi za mikono yenu kwa kuitolea dhabihu miungu mingine katika nchi ya Misri, ambako mmeenda kukaa? Mtaangamia na kuwa kitu cha kulaaniwa na shutuma miongoni mwa mataifa yote ya dunia.+  Je, mmeyasahau matendo maovu ya mababu zenu na matendo maovu ya wafalme wa Yuda+ na matendo maovu ya wake zao,+ na pia matendo yenu maovu na matendo maovu ya wake zenu,+ yaliyofanywa katika nchi ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu? 10  Mpaka leo hii hawajajinyenyekeza,* hawajaogopa,+ wala hawajafuata sheria yangu na amri zangu nilizoweka mbele yenu na mbele ya mababu zenu.’+ 11  “Kwa hiyo Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Tazameni, nimeazimia kuwaletea msiba, kuiangamiza nchi yote ya Yuda. 12  Nami nitawachukua watu wa Yuda waliobaki walioazimia kwenda nchini Misri kukaa huko, na wote wataangamia nchini Misri.+ Watauawa kwa upanga na kuangamia kwa njaa kali; kuanzia mdogo zaidi mpaka mkubwa zaidi, watakufa kwa upanga na kwa njaa kali. Nao watakuwa laana, kitu cha kutisha, matusi, na shutuma.+ 13  Nitawaadhibu wale wanaoishi nchini Misri kama nilivyoliadhibu Yerusalemu, kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari.+ 14  Na watu wa Yuda waliobaki ambao wameenda kukaa nchini Misri hawataponyoka wala kuokoka na kurudi kwenye nchi ya Yuda. Watatamani kurudi na kukaa huko, lakini hawatarudi, isipokuwa wachache watakaoponyoka.’” 15  Wanaume wote waliojua kwamba wake zao walikuwa wakiitolea miungu mingine dhabihu na wake wote waliokuwa wamesimama hapo, wakiwa kundi kubwa, na watu wote waliokuwa wakiishi nchini Misri,+ kule Pathrosi,+ wakamjibu hivi Yeremia: 16  “Hatutasikiliza neno ulilotuambia katika jina la Yehova. 17  Badala yake, hakika tutafanya kila neno ambalo vinywa vyetu vimesema, tutamtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji,+ kama vile sisi, mababu zetu, wafalme wetu, na wakuu wetu walivyofanya katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu tulipokuwa tumeshiba mkate na tulipokuwa na hali njema, wakati ambapo hatukuona msiba wowote. 18  Tangu tulipoacha kumtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji, tumekosa kila kitu nasi tumeangamia kwa upanga na kwa njaa kali.” 19  Wanawake wakasema: “Na tulipokuwa tukimtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji, je, tulitengeneza keki za dhabihu zinazofanana naye na kummiminia matoleo ya kinywaji bila idhini ya waume zetu?” 20  Kisha Yeremia akawaambia hivi watu wote, wanaume na wake zao na watu wote waliokuwa wakizungumza naye: 21  “Dhabihu ambazo ninyi, mababu zenu, wafalme wenu, wakuu wenu, na watu wa nchi walitoa katika majiji ya Yuda na kwenye barabara za Yerusalemu+—Yehova alizikumbuka nazo zikaingia moyoni mwake! 22  Mwishowe Yehova hangeweza tena kuvumilia matendo yenu maovu na mambo yenye kuchukiza mliyokuwa mmefanya, nayo nchi yenu ikawa ukiwa, kitu cha kutisha na laana, bila mkaaji, kama ilivyo leo.+ 23  Ni kwa sababu mmetoa dhabihu hizi na kwa sababu mmemtendea dhambi Yehova, kwa kutotii sauti ya Yehova na kutofuata sheria yake, amri zake, na vikumbusho vyake, ndiyo sababu msiba huu umewapata, kama ilivyo leo.”+ 24  Yeremia akaendelea kuwaambia hivi watu wote na wanawake wote: “Sikieni neno la Yehova, ninyi nyote watu wa Yuda mlio nchini Misri. 25  Yehova wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Mambo ambayo ninyi na wake zenu mmesema kwa vinywa vyenu, mmeyatimiza kwa mikono yenu, kwa maana mlisema: “Hakika tutatimiza nadhiri zetu za kumtolea dhabihu Malkia wa Mbinguni* na kummiminia matoleo ya kinywaji.”+ Hakika ninyi wanawake mtatekeleza nadhiri zenu na kuzitimiza nadhiri zenu.’ 26  “Kwa hiyo sikieni neno la Yehova, ninyi nyote watu wa Yuda mnaoishi nchini Misri: ‘“Ninaapa kwa jina langu mwenyewe lililo kuu,” asema Yehova, “kwamba jina langu halitatajwa tena katika kiapo na mtu yeyote wa Yuda+ katika nchi yote ya Misri anayesema, ‘Kwa hakika kama anavyoishi Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova!’+ 27  Sasa ninawatazama ili kuwaletea msiba bali si mema;+ watu wote wa Yuda walio nchini Misri wataangamia kwa upanga na kwa njaa kali, mpaka watakapokwisha kabisa.+ 28  Ni wachache tu watakaoponyoka upanga nchini Misri na kurudi katika nchi ya Yuda.+ Kisha watu wote wa Yuda waliobaki ambao walienda kukaa nchini Misri watajua ni neno la nani lililotimia, langu au lao!”’” 29  “‘Na hii ndiyo ishara kwenu,’ asema Yehova, ‘kwamba nitawaadhibu mahali hapa, ili mjue kwamba maneno niliyosema kuhusu kuwaletea msiba hakika yatatimia. 30  Yehova anasema hivi: “Ninamtia Farao Hofra, mfalme wa Misri, mikononi mwa maadui wake na wale wanaotaka kumuua,* kama nilivyomtia Mfalme Sedekia wa Yuda mikononi mwa Mfalme Nebukadneza* wa Babiloni, aliyekuwa adui yake na ambaye alitaka kumuua.”’”+

Maelezo ya Chini

Au “Memfisi.”
Tnn., “nikiamka mapema na kuwatuma.”
Au “hawajahisi wamepondeka.”
Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.
Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.
Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.
Jina la mungu wa kike aliyeabudiwa na Waisraeli waasi imani; huenda ni mungu wa kike wa uzazi.
Au “wanaoitafuta nafsi yake.”
Tnn., “Nebukadreza,” njia nyingine ya kuandika jina hili.