Yoshua 4:1-24

  • Mawe ya ukumbusho (1-24)

4  Baada tu ya taifa lote kuvuka Yordani, Yehova akamwambia Yoshua:  “Wachukue wanaume 12 kutoka kati ya watu, yaani, mtu mmoja kutoka katika kila kabila,+  na uwaamuru hivi: ‘Chukueni mawe 12 kutoka katikati ya Yordani, mahali ambapo miguu ya makuhani ilisimama tuli,+ myabebe na kuyaweka mahali mtakapolala usiku huu.’”+  Basi Yoshua akawaita wale wanaume 12 aliowachagua kutoka kati ya Waisraeli, yaani, mtu mmoja kutoka katika kila kabila;  Yoshua akawaambia: “Nendeni katikati ya Yordani mbele ya sanduku la Yehova Mungu wenu, na kila mmoja wenu abebe jiwe begani, kulingana na idadi ya makabila ya Waisraeli,  ili yawe ishara kwenu. Ikiwa watoto* wenu watawauliza wakati ujao, ‘Mawe haya ni ya nini?’+  waambieni: ‘Sanduku la agano la Yehova lilipovushwa Yordani, maji ya Yordani yalizuiwa yasitiririke.+ Basi mawe haya yatakuwa kumbukumbu la kudumu kwa Waisraeli.’”+  Kwa hiyo Waisraeli wakafanya kama Yoshua alivyowaamuru. Wakachukua mawe 12 kutoka katikati ya Yordani, kama Yehova alivyomwagiza Yoshua, kulingana na idadi ya makabila ya Waisraeli. Wakayapeleka mahali walipolala usiku na kuyaweka hapo.  Pia Yoshua akaweka mawe 12 katikati ya Yordani mahali iliposimama miguu ya makuhani waliobeba sanduku la agano,+ na mawe hayo yako huko mpaka leo. 10  Makuhani waliobeba lile Sanduku waliendelea kusimama katikati ya Yordani mpaka watu walipofanya mambo yote ambayo Yehova alimwamuru Yoshua, sawasawa na mambo yote ambayo Musa alikuwa amemwamuru Yoshua. Wakati huohuo, watu waliharakisha kuvuka. 11  Baada tu ya watu wote kuvuka, makuhani waliobeba Sanduku la Yehova wakavuka huku watu wakiwatazama.+ 12  Na watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase wakavuka wakiwa wamejipanga kivita+ na kuwatangulia Waisraeli wengine, kama Musa alivyokuwa amewaagiza.+ 13  Wanajeshi wapatao 40,000 wakiwa na silaha tayari kwa vita wakavuka mbele za Yehova na kuingia katika jangwa tambarare la Yeriko. 14  Siku hiyo Yehova alimkweza Yoshua machoni pa Waisraeli wote,+ wakamheshimu sana* sikuzote za maisha yake, kama walivyomheshimu sana Musa.+ 15  Ndipo Yehova akamwambia Yoshua: 16  “Waamuru makuhani wanaobeba sanduku+ la Ushahidi watoke ndani ya Yordani.” 17  Basi Yoshua akawaamuru hivi makuhani: “Tokeni ndani ya Yordani.” 18  Makuhani waliobeba sanduku la agano+ la Yehova walipotoka katikati ya Yordani na nyayo zao kukanyaga nchi kavu, maji ya Yordani yakaanza kutiririka tena na kingo zake zikafurika+ kama mwanzoni. 19  Watu walivuka Yordani siku ya kumi ya mwezi wa kwanza na kupiga kambi Gilgali+ kwenye mpaka wa mashariki wa Yeriko. 20  Kisha Yoshua akapanga kule Gilgali yale mawe 12 ambayo walichukua kutoka Mto Yordani.+ 21  Akawaambia hivi Waisraeli: “Watoto wenu watakapowauliza wakati ujao, ‘Mawe haya ni ya nini?’+ 22  Waambieni, ‘Waisraeli walivuka katikati ya Mto Yordani kwenye nchi kavu+ 23  Yehova Mungu wenu alipoyakausha maji ya Yordani mbele yao mpaka walipovuka, kama Yehova Mungu wenu alivyoikausha Bahari Nyekundu* mbele yetu mpaka tulipovuka.+ 24  Alifanya hivyo ili watu wote duniani wajue jinsi mkono wa Yehova ulivyo na nguvu+ na ili ninyi mmwogope Yehova Mungu wenu sikuzote.’”

Maelezo ya Chini

Tnn., “wana.”
Tnn., “wakamwogopa.”
Au “Bahari ya Shamu.”