Zekaria 12:1-14
12 Tangazo:
“Neno la Yehova kuhusu Israeli,” asema Yehova,Yule aliyezitandaza mbingu,+Aliyeweka msingi wa dunia,+Na kuumba roho* iliyo ndani ya mwanadamu.
2 “Tazama, ninafanya jiji la Yerusalemu liwe kikombe kinachosababisha* mataifa yote jirani yapepesuke; na jiji la Yuda litazingirwa, na pia Yerusalemu.+
3 Siku hiyo nitafanya Yerusalemu liwe jiwe zito* kwa mataifa yote. Kwa hakika wote watakaolinyanyua watajeruhiwa vibaya;+ na mataifa yote duniani yatakusanyika kupigana na jiji hilo.+
4 Siku hiyo,” asema Yehova, “nitamtia hofu kila farasi na kumtia wazimu yule anayempanda. Nitaikazia macho nyumba ya Yuda, lakini nitampofusha kila farasi wa mataifa.
5 Na mashehe* wa Yuda watasema moyoni mwao, ‘Wakaaji wa Yerusalemu ni nguvu kwetu kwa sababu ya Yehova wa majeshi Mungu wao.’+
6 Siku hiyo nitawafanya mashehe wa Yuda wawe kama chungu cha moto kati ya kuni na kama mwenge unaowaka kati ya safu ya miganda iliyokatwa ya nafaka,+ nao watayateketeza mataifa yote jirani yaliyo upande wa kulia na wa kushoto;+ na jiji la Yerusalemu litakuwa tena na wakaaji mahali pake,* huko Yerusalemu.+
7 “Na Yehova atayaokoa kwanza mahema ya Yuda, ili umaridadi wa* nyumba ya Daudi na umaridadi wa* wakaaji wa Yerusalemu usizidi sana ule wa Yuda.
8 Siku hiyo Yehova atakuwa ulinzi kuwazunguka wakaaji wa Yerusalemu;+ siku hiyo yule anayejikwaa* kati yao atakuwa kama Daudi, na nyumba ya Daudi itakuwa kama Mungu, kama malaika wa Yehova anayetangulia mbele yao.+
9 Na siku hiyo, kwa hakika nitayaangamiza mataifa yote yatakayokuja kushambulia Yerusalemu.+
10 “Nitamimina roho ya kibali na dua juu ya nyumba ya Daudi na juu ya wakaaji wa Yerusalemu, nao watamtazama yule waliyemchoma,+ watamwombolezea kwa sauti kama ambavyo wangemwombolezea mwana wa pekee; watamhuzunikia sana kama ambavyo wangemhuzunikia mwana mzaliwa wa kwanza.
11 Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makubwa Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika Nchi Tambarare ya Megido.+
12 Na nchi itaomboleza kwa sauti, kila ukoo peke yake; ukoo wa nyumba ya Daudi peke yake, na wanawake wao peke yao; ukoo wa nyumba ya Nathani+ peke yake, na wanawake wao peke yao;
13 ukoo wa nyumba ya Lawi+ peke yake, na wanawake wao peke yao; ukoo wa Washimei+ peke yake, na wanawake wao peke yao;
14 na koo zote zinazobaki, kila ukoo peke yake, na wanawake wao peke yao.
Maelezo ya Chini
^ Au “pumzi.”
^ Au “bakuli linalosababisha.”
^ Au “lenye kulemea.”
^ Shehe alikuwa mkuu wa kabila.
^ Au “mahali pake panapostahili.”
^ Au “fahari ya.”
^ Au “fahari ya.”
^ Au “aliye dhaifu zaidi.”