Zekaria 6:1-15

  • Maono ya 8: Magari manne (1-8)

  • Chipukizi atakuwa mfalme na kuhani (9-15)

6  Kisha nikatazama juu tena na kuona magari manne ya vita yakitoka katikati ya milima miwili, na milima hiyo ilikuwa ya shaba.  Gari la kwanza lilikokotwa na farasi wekundu, na gari la pili, farasi weusi.+  Gari la tatu lilikokotwa na farasi weupe, na gari la nne, farasi wenye madoadoa na mabaka.+  Nikamuuliza malaika aliyekuwa akizungumza nami: “Magari haya yanamaanisha nini bwana wangu?”  Malaika huyo akanijibu: “Hizi ni zile roho nne+ za mbinguni zinazotoka baada ya kusimama mbele ya Bwana wa dunia yote.+  Gari linalokokotwa na farasi weusi linaenda katika nchi ya kaskazini;+ farasi weupe wanaenda kuvuka bahari; na wale wenye madoadoa wanaenda katika nchi ya kusini.  Na farasi wenye mabaka walitamani sana kwenda kutembea kotekote duniani.” Kisha akasema: “Nendeni, tembeeni kotekote duniani.” Nao wakaanza kutembea kotekote duniani.  Kisha akaniita kwa sauti na kuniambia: “Tazama, farasi wanaoenda katika nchi ya kaskazini wameifanya roho ya Yehova itulie katika nchi ya kaskazini.”  Neno la Yehova likanijia tena, likisema: 10  “Chukua vitu ambavyo Heldai, Tobaya, na Yedaya walileta kutoka kwa watu walio uhamishoni; na siku hiyo, ni lazima uende katika nyumba ya Yosia mwana wa Sefania ukiwa pamoja na watu hawa waliotoka Babiloni. 11  Unapaswa kuchukua fedha na dhahabu, utengeneze taji* na kumvika kichwani Yoshua+ mwana wa Yehosadaki, kuhani mkuu. 12  Nawe umwambie,“‘Yehova wa majeshi anasema hivi: “Ndiye huyu mwanamume anayeitwa Chipukizi.+ Atachipuka kutoka mahali pake mwenyewe, naye atalijenga hekalu la Yehova.+ 13  Yeye ndiye atakayelijenga hekalu la Yehova, na ndiye atakayepokea utukufu. Ataketi kwenye kiti chake cha ufalme na kutawala, naye atakuwa pia kuhani kwenye kiti chake cha ufalme,+ na kutakuwa na mapatano ya amani kati ya hivyo viwili.* 14  Na taji hilo* litakuwa kumbukumbu* kwa Helemu, Tobaya, Yedaya,+ na Heni mwana wa Sefania, katika hekalu la Yehova. 15  Na wale walio mbali sana watakuja na kushiriki katika ujenzi wa hekalu la Yehova.” Nanyi mtalazimika kujua kwamba Yehova wa majeshi amenituma kwenu. Na itakuwa hivyo—ikiwa hamtakosa kuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu.’”

Maelezo ya Chini

Au “taji lenye utukufu.”
Yaani, kati ya cheo chake akiwa mtawala na cheo chake akiwa kuhani.
Au “taji lenye utukufu.”
Au “ukumbusho.”