Zekaria 7:1-14
7 Na katika mwaka wa nne wa utawala wa Mfalme Dario, neno la Yehova lilimjia Zekaria+ siku ya nne ya mwezi wa tisa, yaani, mwezi wa Kislevu.*
2 Watu wa Betheli walimtuma Shareza na Regem-meleki na wanaume wake ili wamwombe Yehova kibali,*
3 wawaulize hivi makuhani wa nyumba ya* Yehova wa majeshi na pia manabii: “Je, nilie katika mwezi wa tano+ na kujinyima chakula, kama vile ambavyo nimekuwa nikifanya kwa miaka mingi sana?”
4 Neno la Yehova wa majeshi likanijia tena, likisema:
5 “Waambie watu wote nchini na makuhani, ‘Mlipofunga na kulia kwa sauti katika mwezi wa tano na mwezi wa saba+ kwa miaka 70,+ je, kweli mlifunga kwa ajili yangu?
6 Na mlipokuwa mkila na kunywa, je, hamkuwa mkila na kunywa kwa ajili yenu wenyewe?
7 Je, hampaswi kutii maneno ambayo Yehova alitangaza kupitia manabii wa kale,+ wakati jiji la Yerusalemu na majiji yaliyolizunguka yalipokuwa na wakaaji na yalipokuwa na amani, na watu walipokaa Negebu na Shefela?’”
8 Neno la Yehova likamjia tena Zekaria, likisema:
9 “Yehova wa majeshi anasema hivi: ‘Hukumuni kwa haki ya kweli,+ na mtendeane kwa upendo mshikamanifu+ na rehema.
10 Msimpunje mjane wala yatima,*+ mgeni+ wala maskini;+ na katika mioyo yenu msipangiane njama za kutendeana uovu.’+
11 Lakini waliendelea kukataa kusikiliza,+ wakageuza migongo yao kwa ukaidi,+ na kuziba masikio yao ili wasisikie.+
12 Waliifanya mioyo yao iwe kama almasi*+ nao walikataa kutii sheria* na maneno ambayo Yehova wa majeshi aliwapa kwa roho yake kupitia manabii wa kale.+ Kwa hiyo Yehova wa majeshi akakasirika sana.”+
13 “‘Kama vile ambavyo hawakunisikiliza nilipowaita,+ mimi pia sikuwasikiliza waliponiita,’+ asema Yehova wa majeshi.
14 ‘Nami niliwatawanya kwa kimbunga kotekote katika mataifa yote ambayo hawakuyajua,+ na nchi ikaachwa ukiwa nyuma yao, hivi kwamba hakuna yeyote aliyeingia wala kutoka;+ kwa maana waliibadili nchi yenye kutamanika ikawa kitu cha kutisha.’”
Maelezo ya Chini
^ Angalia Nyongeza B15.
^ Tnn., “wautulize uso wa Yehova.”
^ Au “hekalu la.”
^ Tnn., “mtoto asiye na baba.”
^ Au labda, “jiwe gumu,” kama vile jiwe la msasa.
^ Au “mafundisho.”