Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAISHA YA MKRISTO

Jinsi ya Kusaidia Baada ya Janga

Jinsi ya Kusaidia Baada ya Janga

Misiba ya asili inazidi kutokea kwa ukawaida siku hizi. Janga linapotokea, jitihada za kutoa msaada zinapaswa kupangwa na kuratibiwa vizuri. Kwa sababu hiyo, Baraza Linaloongoza limepanga kwamba Idara ya Kutoa Msaada ianzishwe katika ofisi zote za tawi.

Ndugu katika idara hiyo wanapopata habari kwamba janga limetokea, mara moja wanawasiliana na wazee wa eneo hilo ili kufahamu mahitaji ya wahubiri. Ikiwa uharibifu ni mkubwa hivi kwamba wahubiri wa eneo hilo hawawezi kuushughulikia wenyewe, ofisi ya tawi itawapa mgawo ndugu wanaostahili kuongoza jitihada za kutoa msaada. Ndugu hao wanaweza kuomba wapate wajitoleaji au bidhaa hususa, au wanaweza kununua na kugawa vitu vinavyohitajika katika eneo lao.

Kuna faida nyingi za kushughulikia mambo kwa njia hiyo. Kufanya hivyo kunasaidia jitihada kuelekezwa mahali zinapohitajika hasa na hivyo kuepuka mvurugo na upotevu wa pesa na vifaa, ambao unaweza kutokea akina ndugu wanapotenda bila mwelekezo.

Akina ndugu waliowekwa rasmi na ofisi ya tawi wanaweza kuamua kiasi cha pesa na wajitoleaji wanaohitajika kutoa msaada. Pia wanaweza kufahamiana na maofisa wa eneo lao, ambao mara nyingi wanaweza kutusaidia kuharakisha jitihada za kutoa msaada. Kwa hiyo, mtu binafsi hapaswi kuanzisha mradi wa kukusanya pesa, kutuma misaada, wala kusafiri kwenda kwenye eneo lililoathiriwa isipokuwa awe ameombwa kufanya hivyo.

Hata hivyo, bado tungependa kusaidia janga linapotokea. (Ebr 13:16) Tunawapenda ndugu zetu! Tunaweza kufanya nini? Jambo muhimu zaidi tunaloweza kufanya ni kusali kwa ajili ya walioathiriwa na janga hilo na kwa ajili ya wanaotoa msaada. Pia tunaweza kutoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote. Chini ya mwelekezo wa Baraza Linaloongoza, ofisi za tawi zinafaa zaidi kuamua mahali ambapo pesa hizo zitatumiwa kwa njia nzuri zaidi. Na ikiwa tunataka kushiriki moja kwa moja, tunaweza kuonyesha utayari wetu kwa kujaza fomu ya Ombi la Kujitolea Katika Kazi ya Usanifu na Ujenzi (DC-50).

TAZAMENI VIDEO YENYE KICHWA MAFURIKO NCHINI BRAZILI, KISHA MJIBU MASWALI YAFUATAYO:

Ni nini kinachokuvutia kuhusu jitihada za kutoa msaada za Mashahidi wa Yehova baada ya mafuriko nchini Brazili mwaka wa 2020?