Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAISHA YA MKRISTO

Jinsi ya Kutumia Kitabu Biblia Inatufundisha Nini?

Jinsi ya Kutumia Kitabu Biblia Inatufundisha Nini?

Kitabu Biblia Inatufundisha kinafanana na kitabu Biblia Inafundisha. Vifaa hivyo vya kufundishia vinazungumzia kweli zilezile, kwa mpangilio uleule. Hata hivyo, kitabu Biblia Inatufundisha kinazungumzia mambo kwa njia rahisi zaidi na kinatumia maneno rahisi zaidi. Kimetayarishwa kwa ajili ya watu ambao wanashindwa kukielewa kitabu Biblia Inafundisha. Badala ya kuwa na nyongeza, kitabu Biblia Inatufundisha kina maelezo ya ziada yanayotoa ufafanuzi wa baadhi ya maneno na maelezo yanayozungumziwa katika sura mbalimbali. Sura hazina maswali ya utangulizi wala sanduku la pitio. Badala yake kuna muhtasari wa kweli za Biblia zinazofafanuliwa katika kila sura. Kitabu Biblia Inatufundisha kinaweza kutolewa wakati wowote hata ikiwa si toleo la mwezi, kama tunavyofanya na kitabu Biblia Inafundisha. Tunawezaje kutumia sehemu hizo za pekee za kitabu Biblia Inatufundisha tunapoongoza funzo la Biblia?

MUHTASARI: Kwa watu wengi, njia yetu ya kawaida ya kuongoza funzo la Biblia kwa kusoma fungu na kisha kuuliza swali inafaa tunapotumia kitabu Biblia Inafundisha. Lakini namna gani ikiwa mwanafunzi haelewi vizuri lugha au hawezi kusoma vizuri? Katika visa kama hivyo unaweza kuamua kutumia kitabu Biblia Inatufundisha. Kisha, muhtasari wa sura unaweza kutumiwa kama msingi wa funzo na mwanafunzi anaweza kutiwa-moyo ajisomee mafungu katika sura hiyo kwa wakati wake mwenyewe. Kila kweli ya Biblia inaweza kufundishwa katika kipindi cha dakika 15 hivi. Kwa kuwa muhtasari hauna habari zote zinazopatikana katika mafungu, mwalimu anahitaji kujitayarisha vizuri, na kufikiria kwa makini mahitaji ya mwanafunzi. Ikiwa ataongoza funzo kwa kutumia njia ya kawaida ya kusoma mafungu, basi muhtasari unaweza kutumiwa kama pitio.

MAELEZO YA ZIADA: Maelezo ya ziada yameorodheshwa kwa kutegemea mahali ambapo maneno hayo yalizungumziwa kwa mara ya kwanza katika kitabu. Mwalimu anaweza kuamua ikiwa atazungumzia maelezo ya ziada katika kitabu Biblia Inatufundisha wakati wa funzo.