Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kielelezo cha wazazi huwasaidia watoto kujua jinsi ya kuonyesha upendo

NJIA MOJA YA KUNG’OA MZIZI WA TATIZO

Elimu Kuhusu Maadili

Elimu Kuhusu Maadili

Walipokuwa kwenye ziara ya shule, wavulana fulani walimtendea mvulana mwenzao vibaya kingono. Vijana hao wote walikuwa wanafunzi wa shule fulani ya kibinafsi iliyo maarufu nchini Kanada. Baada ya tukio hilo, Leonard Stern, mwandishi wa gazeti la Ottawa Citizen aliandika hivi: “Kuwa werevu, kupata elimu bora, na kuheshimika katika jamii hakuwazuii vijana kufanya maamuzi mabaya kuhusu maadili.”

Stern alisema hivi pia: “Kwa kawaida tunatarajia lengo kuu la wazazi liwe kuwalea watoto ili wawe na maadili mazuri. Lakini inaonekana kwamba machoni pa wazazi wengi, jambo muhimu zaidi ni watoto wao kufaulu shuleni ili wapate kazi nzuri na kuwa na pesa nyingi.”

Ni kweli kwamba elimu ni muhimu. Lakini elimu ambayo watu hupata shuleni, hata iwe nzuri kadiri gani, haiwasaidii kushinda tamaa mbaya au mielekeo isiyofaa. Hivyo basi, tunaweza kupata wapi elimu itakayotupatia mwongozo unaofaa kuhusu maadili?

ELIMU BORA ZAIDI

Biblia ni kama kioo. Tunapoichunguza, tunaweza kutambua vizuri udhaifu na mipaka yetu. (Yakobo 1:23-25) Lakini zaidi ya hilo, Biblia hutusaidia kufanya mabadiliko yanayohitajika na kusitawisha sifa zinazotokeza amani ya kweli na umoja. Sifa hizo zinatia ndani wema, fadhili, subira, kujizuia, na upendo. Upendo ni sifa ya pekee hivi kwamba inatajwa kuwa “kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:14) Kwa nini? Biblia inasema hivi:

  • “Upendo ni wenye subira na fadhili. Upendo hauna wivu. Haujigambi, haujivuni [kwa kiburi], haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii ukosefu wa uadilifu [au ubaya], bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, . . .  huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”—1 Wakorintho 13:4-8.

  • “Upendo haumfanyii uovu jirani.”—Waroma 13:10.

  • “Zaidi ya mambo yote, pendaneni sana, kwa sababu upendo hufunika dhambi nyingi.”—1 Petro 4:8.

Unapokuwa na watu wanaokupenda, wewe huhisije? Unahisi hali ya usalama na utulivu, sivyo? Bila shaka, kwa sababu unajua kwamba watu hao wana nia nzuri na hawawezi kukuumiza kimakusudi.

Upendo pia huwachochea watu kujidhabihu, na hata kubadili tabia zao, ili wawanufaishe wengine. Kwa mfano, baada ya binti yake kujifungua, George alitamani sana kuwa pamoja na mjukuu wake mara kwa mara. Lakini kulikuwa na tatizo. George alikuwa na zoea la kuvuta sigara, na mume wa binti yake hakutaka avute sigara anapokuwa na mtoto. George alifanya nini? Licha ya kwamba alikuwa mvuta-sigara kwa miaka 50, aliacha zoea hilo ili apate nafasi ya kuwa na mjukuu wake. Kwa kweli, upendo una nguvu!

Biblia hutusaidia kusitawisha sifa nyingi nzuri kama vile wema, fadhili, na hasa upendo.

Hatuzaliwi tukiwa na sifa ya upendo. Wazazi wana nafasi kubwa ya kuwaonyesha watoto wao jinsi ya kuwa wenye upendo. Wao huwapatia chakula na kuwalinda, na pia wanawasaidia wanapoumia au wanapokuwa wagonjwa. Wazazi wazuri huzungumza na watoto wao na kuwaelimisha pia. Vilevile, wao huwatia nidhamu na kuwafundisha kuwa na maadili. Na bila shaka, wazazi wazuri huishi kulingana na kile wanachofundisha, na hivyo kuwawekea watoto wao kielelezo kinachofaa.

Hata hivyo, inasikitisha kwamba baadhi ya wazazi wameshindwa kutimiza wajibu wao. Je, hilo linamaanisha kwamba haiwezekani kabisa kwa watoto wao kusitawisha sifa nzuri? La hasha! Kuna watu wengi, kutia ndani wale waliolelewa katika familia zenye migogoro na matatizo, ambao wamefanikiwa kubadili maisha yao na kuwa watu wanaotegemeka na wanaowajali wengine. Na kama tutakavyoona katika makala inayofuata, hata watu ambao huenda wakaonekana kuwa wameshindikana, wanaweza kubadilika!