Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ili kutatua tatizo, ni muhimu kushughulikia chanzo chake na si kutuliza dalili

CHANGAMOTO

Kushughulikia Mzizi wa Matatizo Yetu

Kushughulikia Mzizi wa Matatizo Yetu

Je, unaamini kwamba wanadamu wana uwezo wa kutatua matatizo yanayofanya tukose amani na usalama na yanayohatarisha maisha yetu ya wakati ujao? Ili kutatua tatizo, tunahitaji kushughulikia chanzo au mzizi wake na si dalili.

Ili kuelewa jambo hilo, mfikirie Tom, * ambaye aliugua na kisha akafa. Ni nini kilisababisha kifo chake? Daktari wa hospitali iliyompokea muda mfupi kabla hajafa, aliandika kwamba Tom “alipoanza kuugua, hakuna aliyefikiria kutafuta chanzo cha tatizo alilokuwa nalo.” Inaonekana kwamba madaktari waliomtibu Tom mwanzoni, walimpatia dawa za kutuliza tu ugonjwa aliokuwa nao.

Je, inawezekana kwamba wanadamu wanafanya vivyo hivyo kuhusiana na matatizo yaliyopo duniani leo? Kwa mfano, ili kukabiliana na uhalifu, serikali hutunga sheria, huweka kamera, na kuimarisha jeshi la polisi. Hata hivyo, ingawa mbinu hizo hufaulu kwa kadiri fulani, bado hazitatui chanzo hasa cha tatizo. Ukweli ni kwamba, matendo ya watu hutegemea tamaa zao, mtazamo wao, na mambo wanayoamini.

Daniel, anayeishi Amerika Kusini katika nchi ambayo uchumi wake umeporomoka, alisema: “Tuliishi maisha ya kawaida tu mwanzoni. Hatukuwazia kuvamiwa na wezi wenye silaha. Lakini sasa hakuna usalama tena, iwe ni mjini au kijiji. Kuporomoka kwa uchumi kumefunua kwamba watu ni wenye pupa na hawaheshimu uhai wala mali za wengine, sifa ambazo zilikuwa zimejificha.”

Mwanamume anayeitwa Elias alikimbia mapigano huko Mashariki ya Kati na baadaye akajifunza Biblia. Alisema: “Vijana wengi kwenye eneo letu walishinikizwa na familia zao na wanasiasa na viongozi wa dini, wajiunge vitani ili waonekane mashujaa. Wale wa upande wa upinzani, nao waliambiwa maneno hayohayo! Hilo lilinifumbua macho na nikaona jinsi inavyokatisha tamaa kuutumaini uongozi wa wanadamu.”

Kitabu cha kale kilichojaa hekima kinasema hivi:

  • “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu wakati wa ujana.”—Mwanzo 8:21.

  • “Moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari. Ni nani anayeweza kuujua?”—Yeremia 17:9.

  • “Moyoni hutoka mawazo mabaya, mauaji, . . . uasherati, wizi, ushahidi wa uwongo.”—Mathayo 15:19.

Wanadamu wameshindwa kupata tiba ya mielekeo mibaya inayowaongoza watu kuwadhuru wengine. Na kama makala iliyotangulia ilivyoonyesha, inaonekana kwamba hali inazidi kuwa mbaya siku baada ya siku. (2 Timotheo 3:1-5) Cha kushangaza, mambo yako hivyo licha ya kwamba leo wanadamu wana ujuzi mwingi sana na njia nyingi zaidi za kuwasiliana! Hivyo, kwa nini tunashindwa kuleta amani na usalama ulimwenguni? Je, tunajitahidi kufanya jambo lililo nje ya uwezo wetu? Je, tunajaribu kufanya jambo lisilowezekana?

JE, TUNAJARIBU KUFANYA KISICHOWEZEKANA?

Hata ikiwa kwa njia fulani tungefanikiwa kutibu mielekeo mibaya ya wanadamu, bado hatungeweza kuleta amani na usalama duniani. Kwa nini? Uwezo wetu una mipaka.

Ukweli wa mambo ni huu: “Mwanadamu . . . hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Yeremia 10:23) Hivyo ndivyo ilivyo, hatukuumbwa tujiongoze wenyewe. Kwa kweli, mwanadamu hakuumbwa amtawale mwenzake kama tu ambavyo hatukuumbwa tuishi kwenye maji au nje ya anga la dunia!

Mwanadamu hakuumbwa amtawale mwenzake kama tu ambavyo hatukuumbwa tuishi kwenye maji

Kwa mfano, fikiria hili: Kwa ujumla, je, watu wanapenda kuambiwa na wanadamu wenzao jinsi ya kuishi au tabia wanazopaswa kuwa nazo? Au watu huonaje wengine wanapowaambia cha kufanya inapohusu mambo kama vile kutoa mimba au jinsi ya kuwaadhibu watoto wao? Hayo ni baadhi ya mambo ambayo yanawatenganisha wanadamu. Hivyo, Biblia iko sahihi, ingawa huenda ikawa vigumu kuukubali ukweli huo. Hatuna uwezo wala haki ya kuwatawala wanadamu wenzetu. Hivyo basi, tutapata wapi msaada?

Muumba wetu tu ndiye aliye na uwezo wa kutusaidia. Yeye ndiye aliyetuumba, sivyo? Na kinyume na maoni ya baadhi ya watu, Mungu hajatusahau. Hekima iliyo katika Biblia inafunua wazi jinsi anavyotujali. Kitabu hicho cha pekee hutusaidia kuelewa vizuri mipaka ya uwezo wetu. Pia, kinatusaidia kuelewa kwa nini maisha ya wanadamu yamekuwa na matatizo chungu nzima. Na hivyo tunaweza kuelewa kwa nini “wanadamu . . . hawajajifunza lolote na wala hawatumii kanuni zinazotokana na mambo yaliyotokea zamani,” kama mwanafalsafa fulani Mjerumani alivyoandika.

HEKIMA INAYOPATIKANA KWENYE BIBLIA HUTULINDA!

Yesu alisema kwamba “hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kupitia watoto wake wote,” au matokeo yake. (Luka 7:35) Mfano mmoja ni ushauri ulio katika andiko la Isaya 2:22: “Kwa faida yenu wenyewe, acheni kumtumaini mwanadamu.” Ushauri huo mzuri unaweza kutusaidia tuepuke kutumaini ahadi ambazo hazitawahi kutimia. Kenneth, anayeishi Amerika Kaskazini katika nchi ambayo imejaa matendo ya kikatili, anasema: “Wanasiasa huahidi kwamba watarekebisha mambo, lakini hawawezi. Kwa kweli, hekima iliyo kwenye Biblia huonekana kila mara wanaposhindwa kutimiza mambo wanayoahidi.”

Daniel, aliyetajwa awali, anasema: “Mambo yanayotendeka kila siku hunithibitishia kwamba wanadamu hawawezi kuongoza vizuri. . . . Kuwa na pesa kwenye akaunti au kupata malipo ya pensheni hakumaanishi utaishi vizuri wakati ujao. Nimeona watu wengi wakitamaushwa sana.”

Zaidi ya kutusaidia kuepuka kutumaini ahadi ambazo haziwezi kutimia, Biblia pia hutupatia tumaini la kweli. Makala zinazofuata zitafafanua jambo hilo.

^ Baadhi ya majina katika makala za toleo hili yamebadilishwa.