Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SERIKALI ITAKAYONG’OA MZIZI WA TATIZO

“Amani . . . Haitakoma”

“Amani . . . Haitakoma”

Umoja wa Mataifa unawachochea watu wajione kuwa raia wa dunia nzima na si raia wa nchi hususa tu. Baadhi ya malengo ya mpango huo ni kuwachochea watu wa mataifa mbalimbali washirikiane, waheshimu haki za binadamu, na kutunza mazingira. Kwa nini mpango huo ulianzishwa? Kwenye jarida la UN Chronicle, Maher Nasser aliandika kwamba “mabadiliko ya hali ya hewa, matendo mabaya yanayofanywa na mashirika makubwa ya wahalifu, kuongezeka kwa upotoshaji wa haki, mizozo isiyo suluhishwa, idadi kubwa ya watu wanaokimbia maeneo yao, ugaidi ulioenea kotekote, magonjwa ya kuambukiza na mambo mengine kama hayo hayatambui . . . mipaka [ya nchi].”

Zaidi ya hilo, wengine hata walipendekeza kuwe na serikali inayotawala dunia nzima. Watu hao wanatia ndani mwanafizikia Albert Einstein (1879-1955) na mwanafalsafa Mwitaliano aliyeitwa Dante (1265-1321) ambaye pia alikuwa mtunzi wa mashairi na mwanasiasa. Dante aliamini kwamba ulimwengu uliogawanyika kisiasa hauwezi kuwa na amani. Akimnukuu Yesu Kristo, alisema kwamba “ufalme uliogawanyika dhidi yake wenyewe utaangamia.”—Luka 11:17.

Muda mfupi baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, ambapo mabomu mawili ya atomu yalitumika, Albert Einstein aliliandikia barua Kongamano Kuu la Umoja wa Mataifa. Katika barua hiyo iliyochapishwa kwenye gazeti, Einstein alisema: “Umoja wa Mataifa unahitaji kuchukua hatua haraka sana na kuweka msingi wa kuwa na serikali moja inayotawala dunia yote ili kuleta usalama ulimwenguni pote.”

Lakini ikiwa serikali hiyo yenye nguvu itaanzishwa, tuna uhakika gani kwamba viongozi wake watakuwa na uwezo unaohitajika na hawatakuwa wafisadi na wakandamizaji? Au je, watakuwa na sifa mbaya tu kama za viongozi ambao wamekuwepo? Maswali hayo yanatukumbusha ukweli huu ambao umeonekana katika historia ya wanadamu: Wanadamu hutumia mamlaka vibaya. Na inaonekana kadiri mamlaka yao yanavyoongezeka ndivyo wanavyoyatumia vibaya zaidi.

Ingawa hivyo, ili wanadamu wafurahie amani ya kweli na umoja, wanapaswa kuungana. Lakini lengo hilo linaweza kufikiwaje? Je, kweli hata inawezekana kulifikia? Kulingana na Biblia, jibu ni ndiyo. Inawezekana kulifikia na litatimia. Jinsi gani? Kupitia serikali iliyosimamishwa na Mungu, na si serikali za wanadamu zilizojaa ufisadi. Na hata zaidi, serikali hiyo itakapokuwa ikitawala, kwa haki, Yehova atakuwa mtawala wa viumbe vyake. Ni serikali gani hiyo? Biblia huiita serikali hiyo “Ufalme wa Mungu.”​—Luka 4:43.

“UFALME WAKO NA UJE”

Katika sala yake ya kielelezo, Yesu Kristo alikuwa akirejelea Ufalme wa Mungu aliposema hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani.” (Mathayo 6:9, 10) Naam, Ufalme wa Mungu utahakikisha kwamba mapenzi ya Mungu yanatendeka duniani, na si mapenzi ya wanadamu wabinafsi walio na uchu wa madaraka.

Ufalme wa Mungu pia unaitwa “Ufalme wa mbinguni.” (Mathayo 5:3) Kwa nini? Kwa sababu, ingawa Ufalme huo utaitawala dunia, utatawala kutoka mbinguni na si duniani. Unajua hilo linamaanisha nini? Serikali hiyo itakayotawala dunia nzima, haitahitaji kuomba pesa au kuwatoza wananchi ushuru. Kwa kweli, wanadamu watakuwa wametua mzigo mzito!

Ufalme wa Mungu ni utawala wa kifalme. Yesu Kristo ndiye Mfalme wa utawala huo na alipokea mamlaka aliyo nayo kutoka kwa Mungu. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu:

  • “Atapewa mamlaka ya kutawala. . . . Utawala wake utasitawi daima, amani ya ufalme wake haitakoma.”—Isaya 9:6, 7, Biblia Habari Njema.

  • “Naye akapewa utawala, heshima, na ufalme, ili watu wa makabila, mataifa, na lugha zote wamtumikie. Utawala wake . . . hautapitilia mbali.”—Danieli 7:14.

  • “Ufalme wa ulimwengu umekuwa Ufalme wa Bwana [Mungu] wetu na wa Kristo wake.”—Ufunuo 11:15.

Ufalme wa Mungu utatimiza kikamili mapenzi ya Mungu duniani, kama Yesu alivyoomba katika sala ya kielelezo. Ufalme huo utakapokuwa ukitawala, wanadamu wote watajifunza jinsi ya kuitunza dunia ili irudie ubora wake na kujaa viumbe wenye afya.

Zaidi ya yote, Ufalme wa Mungu utawaelimisha raia wake. Wote watafundishwa kanuni zilezile. Hakutakuwa na migawanyiko wala malumbano. “Hawatasababisha madhara yoyote wala uharibifu wowote . . . kwa maana kwa hakika dunia itajaa ujuzi kumhusu Yehova kama maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:9.

Hatimaye wakaaji wa dunia nzima wataungana na kuishi kwa amani, maisha ambayo Umoja wa Mataifa unatamani watu waishi leo. Andiko la Zaburi 37:11 linasema: “Nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani.” Baada ya muda, maneno kama vile “uhalifu,” “uchafuzi wa mazingira,” “umaskini,” na “vita” yatatoweka vinywani mwetu. Lakini mambo hayo yatatokea wakati gani? Au kwa maneno mengine, Ufalme wa Mungu utaanza kutawala lini? Utachukua mamlaka jinsi gani? Na utawala huo utakunufaishaje? Acheni tuone.