Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

WALIFAULU KUUNG’OA MZIZI

Simulizi la Ricardo na la Andres

Simulizi la Ricardo na la Andres

Elimu ya Biblia ina uwezo mkubwa wa kubadili maisha ya watu. Acheni tuchunguze simulizi la Ricardo na la Andres.

RICARDO: Nilikuwa na umri wa miaka 15 tu, nilipojiunga na kundi la wahalifu. Marafiki hao wapya waliniathiri sana. Hata nilijiwekea lengo la kukaa miaka kumi gerezani! Huenda hilo likaonekana kuwa wazo la kipumbavu. Lakini kwenye eneo tuliloishi, watu waliowahi kuwa gerezani waliheshimiwa sana. Nilitamani kuwa kama wao.

Nilishiriki mambo yote yanayofanywa na wahalifu—kutumia dawa za kulevya, kufanya uasherati, na ukatili. Siku moja usiku, kundi letu lilishambuliana kwa bunduki na kundi lingine. Nilifikiri nitauawa, lakini niliponyoka bila kujeruhiwa. Baada ya tukio hilo, nilianza kufikiria kwa kina kuhusu maisha na malengo yangu, na nikaamua kufanya mabadiliko. Lakini jinsi gani? Nilijiuliza, nitapata wapi msaada?

Kwenye ukoo wetu, wengi hawakuwa na furaha. Maisha yao yalikuwa na matatizo chungu nzima. Lakini familia ya mjomba wangu mmoja ilikuwa tofauti. Nilijua walikuwa watu wazuri na walifuata kanuni za Biblia. Wakati fulani, hata walinifundisha kwamba Mungu anaitwa Yehova. Hivyo, muda mfupi baada ya lile tukio la kushambuliana, nilisali kwa Yehova, nikitumia jina lake, na kumwomba anisaidie. Siku iliyofuata Shahidi wa Yehova alibisha mlango wangu. Nilishangaa sana! Alianza kunifundisha Biblia.

Baada ya muda, changamoto kubwa ilijitokeza. Rafiki zangu wa zamani walianza kunipigia simu na kuniomba nijiunge nao. Nilikataa, ingawa haikuwa rahisi kufanya hivyo. Nilikuwa nimeazimia kuendelea kujifunza Biblia. Huo ulikuwa uamuzi wa hekima! Maisha yangu yalibadilika kabisa, na nikawa na furaha ya kweli.

Nakumbuka niliwahi kumwambia Mungu kwamba wakati fulani nilikuwa tayari kukaa gerezani kwa miaka kumi ili niheshimiwe. Hivyo, nikamwomba anipatie fursa ya kumtumikia kwa angalau miaka kumi nikiwa mwalimu wa Biblia wa wakati wote, ili niwasaidie wengine kama mimi nilivyosaidiwa. Mungu alijibu sala yangu kwa kuwa kwa miaka 17 sasa, nimekuwa nikitumikia kwenye utumishi huo! Na unajua nini, sikuwahi kwenda gerezani!

Kwa upande mwingine, rafiki zangu wengi wa zamani wanatumikia vifungo virefu gerezani. Na wengine wamekufa. Ninapofikiria maisha yangu, ninamshukuru sana mjomba na familia yake, ambao ni Mashahidi. Walikuwa tayari kuishi maisha tofauti yaliyotegemea Biblia. Ninawaheshimu sana kuliko mtu yeyote kwenye kundi nililoshirikiana nalo. Zaidi ya yote, ninamshukuru Mungu kwa kunifundisha njia bora ya maisha.

ANDRES: Nililelewa katika eneo maskini, ambapo mambo kama vile matumizi ya dawa za kulevya, wizi, mauaji, na ukahaba yalikuwa ya kawaida. Baba alikuwa mlevi na mraibu wa dawa za kulevya. Yeye na mama walifokeana na kupigana mara kwa mara.

Nikiwa na umri mdogo tu, nilianza kutumia dawa za kulevya na kunywa pombe. Muda mwingi nilikuwa mitaani, nikiiba na kuuza vitu nilivyoiba. Kadiri nilivyozidi kukua, baba alianza kunifundisha jinsi ya kuingiza nchini dawa za kulevya na vitu vingine vya magendo na kuviuza. Alifikiri kwa kufanya hivyo, angeweza kusitawisha uhusiano wa karibu na mimi. Kwa muda mfupi tu, nilipata pesa nyingi sana. Lakini siku moja, askari walikuja nyumbani. Walinikamata na nikahukumiwa kifungo cha miaka mitano gerezani kwa kosa la kujaribu kuua.

Asubuhi moja, nilisikia tangazo gerezani kwamba wafungwa wote wanakaribishwa kwenye mazungumzo ya Biblia yaliyokuwa yanaongozwa na Mashahidi wa Yehova. Niliamua kuhudhuria. Mambo niliyosikia yalinigusa moyo, na hivyo nikaanza kujifunza Biblia na Mashahidi. Hawakupindisha Maandiko, bali walinionyesha waziwazi viwango vya juu vya maadili ambavyo Mungu ameweka.

Hata hivyo, nilitambua kwamba kwa uwezo wangu pekee, nisingefaulu kufanya mabadiliko maishani, hasa baada ya kuanza kupata vitisho kutoka kwa wafungwa wenzangu ambao hawakufurahishwa na uamuzi wangu. Hivyo nilimwomba Yehova anipe nguvu na hekima, na alijibu sala zangu. Nilipata ujasiri hivi kwamba, badala ya kuogopa, nilifaulu hata kuwahubiria wafungwa wengine.

Nilipoachiliwa, nilikuwa na wasiwasi sana hivi kwamba nilitamani kuendelea kukaa gerezani! Nilipokuwa nikiondoka, wafungwa wengine walinipungia mkono wakiniaga. Baadhi yao walisema kwa utani, “Mchungaji, nenda nyumbani.”

Huwa sipendi hata kufikiria jinsi ambavyo maisha yangu yangekuwa iwapo ningekataa kufundishwa na Mungu. Ninamshukuru sana kwa kunionyesha upendo na kutoniona kama mtu aliyeshindikana. *

^ Unaweza kupata masimulizi zaidi ya jinsi Biblia ilivyo na uwezo wa kubadili maisha ya watu kwenye jw.org. Tafuta kwenye MAKTABA, mfululizo wa makala za “Biblia Inabadili Maisha.”