Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Watu Hawawaheshimu Wengine?

Kwa Nini Watu Hawawaheshimu Wengine?

KWA NINI NI MUHIMU KUWAHESHIMU WENGINE

Tunapowaheshimu wengine, tunaepuka kutoelewana na tunadumisha amani na watu.

  • Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Jibu la upole hutuliza hasira, lakini neno kali huchochea hasira.” (Methali 15:1) Maneno na matendo yasiyo na heshima husababisha kutoelewana na madhara makubwa.

  • Yesu alisema hivi: “Kinywa husema mambo yaliyojaa moyoni.” (Mathayo 12:34) Tunapowakosea watu heshima kupitia maneno yetu, tunaonyesha tatizo tulilo nalo, yaani, hisia zetu kuelekea watu wa rangi, kabila, malezi, au nchi tofauti na yetu.

    Katika uchunguzi uliofanywa hivi karibuni uliohusisha washiriki zaidi ya 32,000 katika nchi 28, asilimia 65 walisema kwamba hawajawahi kushuhudia ukosefu mkubwa wa heshima kama ule wanaojionea miongoni mwa watu leo.

JAMBO UNALOWEZA KUFANYA

Heshimu kila mtu, iwe ni shuleni au kazini hata kama hukubaliani na maoni yake. Tambua mambo ambayo mnaweza kukubaliana. Kufanya hivyo kutakusaidia kutowachambua au kuwahukumu watu.

“Acheni kuhukumu ili msihukumiwe.” —Mathayo 7:1.

Watendee wengine kama ambavyo wewe ungependa kutendewa. Ukiwatendea wengine kwa fadhili na haki, huenda wao pia wakakutendea vivyo hivyo.

“Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni vivyo hivyo.”—Luka 6:31.

Uwe mwenye kusamehe. Amini kwamba mtu hana nia mbaya licha ya maneno au matendo yake yasiyo na fadhili.

“Ufahamu wa mtu hakika hutuliza hasira yake, na ni fahari kwake kuachilia kosa.”—Methali 19:11.

MAMBO TUNAYOFANYA

Mashahidi wa Yehova wanawasaidia watu wanaoshirikiana nao kazini na katika maeneo wanayoishi wawe na heshima.

Tunawafundisha watu wote Biblia bila malipo lakini hatulazimishi watu wakubali mafundisho au maoni yetu. Badala yake, tunajitahidi kufuata shauri la Biblia kwa kuwaambia wengine ujumbe wetu “kwa upole na heshima kubwa.”—1 Petro 3:15; 2 Timotheo 2:24.

Tunakataa ubaguzi na tunawakaribisha katika mikutano yetu watu kutoka malezi mbalimbali wanaotaka kujifunza kile ambacho Biblia inafundisha. Tunajitahidi kuwakubali na ‘kuwaheshimu watu wa namna zote.’—1 Petro 2:17.

Tunaheshimu mamlaka ya serikali katika maeneo tunayoishi. (Waroma 13:1) Tunatii sheria na tunalipa kodi. Pia, ingawa hatuungi mkono upande wowote kisiasa, tunaheshimu haki za wengine za kufanya maamuzi inapohusu mambo ya siasa.