Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, kumtia mtu alama kunakotajwa kwenye 2 Wathesalonike 3:14 ni hatua inayochukuliwa na wazee wa kutaniko au Mkristo mmoja-mmoja?

Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo jijini Thesalonike hivi: “Ikiwa yeyote hatii maneno yetu kupitia barua hii, mtieni alama.” (2 The. 3:14) Zamani tulisema kwamba huo ulikuwa mwongozo kwa wazee wa kutaniko. Ikiwa mtu angeendelea kupuuza kanuni za Biblia licha ya kushauriwa tena na tena, huenda wazee wa kutaniko wangetoa hotuba ya kuonya kutanikoni. Baada ya hapo, wahubiri hawangeendelea kushirikiana na mtu aliyetiwa alama katika mambo kama vile tafrija, bali wangeshirikiana naye katika mambo ya kiroho tu.

Hata hivyo, tunahitaji kubadili uelewaji wetu. Inaonekana kwamba shauri la Paulo linarejelea hatua ambayo Mkristo mmoja-mmoja anapaswa kuchukua chini ya hali fulani. Hivyo, wazee hawahitaji kutoa hotuba ya kuonya. Kwa nini tumebadili uelewaji huo? Fikiria muktadha wa shauri hilo la Paulo.

Paulo alitambua kwamba baadhi ya watu katika kutaniko hilo walikuwa ‘hawafuati utaratibu.’ Walikataa kutii shauri lililokuwa limeongozwa na roho. Katika ziara yake iliyopita, alikuwa amewaagiza hivi: “Mtu yeyote asiyetaka kufanya kazi, asile chakula.” Hata hivyo, bado baadhi ya watu walikataa kufanya kazi ili kujitegemeza ingawa walikuwa na uwezo wa kufanya hivyo. Pia, walikuwa wakijiingiza katika mambo yasiyowahusu. Wakristo walipaswa kuwatendeaje watu hao wasiofuata utaratibu?—2 The. 3:​6, 10-12.

Paulo alisema, “mtieni alama.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mtieni alama” lina wazo la kumtambua mtu huyo na kuwa mwangalifu ili kuepuka kuathiriwa naye. Paulo alitoa maagizo hayo kwa kutaniko lote, si tu kwa wazee wa kutaniko. (2 The. 1:1; 3:6) Hivyo, Mkristo mmoja-mmoja ambaye huenda alimwona Mkristo mwenzake akikosa kutii shauri lililoongozwa na roho angechagua ‘kuacha kushirikiana’ na mtu huyo asiyefuata utaratibu.

Je, Paulo alimaanisha kwamba mtu huyo alipaswa kutendewa kama mtu aliyeondolewa kutanikoni? Hapana. Paulo aliendelea kusema hivi: “Endeleeni kumwonya kama ndugu.” Hivyo, Mkristo mmoja-mmoja bado angeendelea kushirikiana na mtu huyo aliyetiwa alama kwenye mikutano na katika huduma, lakini hangeshirikiana na mtu huyo katika pindi za tafrija au burudani. Kwa nini? Paulo alisema, “ili aone aibu.” Kwa kuwa ametiwa alama, huenda Mkristo huyo asiyefuata utaratibu akaona aibu kwa sababu ya mwenendo wake na kubadili njia zake.—2 The. 3:​14, 15.

Wakristo leo wanawezaje kutumia shauri hilo? Kwanza, tungependa kuhakikisha kwamba kwa kweli mwenendo wa mtu huyo unaonyesha ‘hafuati utaratibu,’ kama Paulo alivyosema. Hakuwa akizungumzia kuhusu wale ambao tunatofautiana nao katika mambo yanayohusu dhamiri au mapendezi yetu ya kibinafsi. Na hakumaanisha wale ambao wametuumiza kihisia. Badala yake, Paulo alikuwa akizungumzia kihususa wale ambao wanaamua kutotii kimakusudi shauri lililo wazi kutoka kwa Mungu.

Leo, ikiwa tunatambua kwamba Mkristo mwenzetu ana mtazamo wa kutotii, a tutafanya uamuzi wa kibinafsi wa kuacha kushirikiana naye kwenye pindi za tafrija au burudani. Kwa kuwa huo ni uamuzi wa kibinafsi, hatungependa kuuzungumzia na watu wengine ambao si wa familia yetu. Na bado tutaendelea kushirikiana na mtu huyo kwenye mikutano na katika huduma. Anapobadili mtazamo na mwenendo wake, tutaanza kushirikiana naye tena kwenye pindi za tafrija au burudani.

a Kwa mfano, huenda Mkristo mwenzako akakataa kufanya kazi ili kujitegemeza ingawa ana uwezo wa kufanya hivyo, huenda anaendeleza uchumba na mtu asiyeamini, au huenda anaeneza mazungumzo yanayosababisha migawanyiko au porojo zenye kuumiza. (1 Kor. 7:39; 2 Kor. 6:14; 2 The. 3:​11, 12; 1 Tim. 5:13) Wale wanaoendelea na mwenendo kama huo ‘hawafuati utaratibu.’